Virusi vya korona: maswali na majibu

Orodha ya maswali

231. Aina mpya ya virusi vya korona iliyobainika mara ya kwanza nchini India.

Shirika la Afya Duniani - WHO lilisema kwenye mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika Mei 10 mwaka huu kuwa, taarifa zinaashiria kwamba aina mpya ya virusi vya korona iliyobainika kwanza nchini India inaambukiza kwa kasi. Shirika hilo limebadilisha uainishaji wa aina hiyo kuwa “inayotia wasiwasi” kutoka “inayovutia nadhari,” na litaongeza ufuatiliaji wake.

India imeshuhudia wimbi kubwa la maambukizi ya virusi vya korona tangu mwezi Aprili. Wimbi hilo linahusishwa na aina hii mpya ya virusi pamoja na mikusanyiko mikubwa ya watu kwa ajili ya sherehe za kidini, kampeni za siasa na hatua finyu za kuzuia maambukizi kama vile watu kutokaribiana.

WHO inasema aina ya virusi ya India ina mabadiliko matatu muhimu ambayo ni L452R, P681R na E484Q ama hayo mawili bila ya E484Q.

Mabadiliko hayo yana mfanano kwenye muundo wa asidi ya amino wa ule uitwao “spike protein”. Mabadiliko hayo yanaweza kuvifanya virusi kuwa vinaambukiza mno na kusababisha kudhoofika kwa kingamwili. Utafiti zaidi kwa sasa unafanyika kuhusiana na aina hiyo.

Mamlaka za afya za Uingereza zilisema Mei 7 mwaka huu kwamba huku aina hii ya virusi ya India ikionekana kuwa na kiwango sawa cha kuambukiza kama aina iliyobainika nchini Uingereza, hazijabaini uthibitisho wowote kuwa aina hiyo inasababisha dalili kali zaidi za ugonjwa ama kuathiri ufanisi wa chanjo.

Watafiti katika Taasisi ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi nchini Japani na wengineo wanasema aina hii ya virusi vya korona yenye mabadiliko ya L452R imeripotiwa kuwa na uwezo wa kuambukiza kwa karibu asilimia 20 zaidi ya aina za awali za virusi. Aina hiyo imeenea hususan nchini Marekani kwenye Jimbo la California.

Lakini watafiti wanasema bado haijabainika iwapo aina hii ya virusi kiuhalisia inaambukiza zaidi ya aina zingine, wakisisitizia umuhimu wa kuendelea kufanya tafiti.

Sio nadra kwa aina mpya ya virusi vya korona kubeba aina mbili ama zaidi za mabadiliko. Swali ni je, mabadiliko hayo yana athari kwenye uwezo wake wa kuambukiza?

Mathalan, aina iliyobainika kwanza nchini Uingereza na imekuwa ikienea katika maeneo kadhaa likiwemo eneo la Kansai nchini Japani, ina walau aina tano za mabadiliko kwenye “spike protein.”

Moja ya mabadiliko hayo, N501Y, inaaminika kuvifanya virusi hivyo kuambukiza zaidi na hivyo kuzua wasiwasi.

Aina mpya za virusi vya korona zilizobainika Afrika Kusini na Brazil pia zina mabadiliko ya aina kadhaa ikiwemo N501Y, pamoja na mabadiliko ya E484K, yanayoweza kupunguza viwango vya kingamwili.

Taarifa hii ni sahihi hadi Mei 14. Inapatikana kwenye tovuti ya NHK World Japan.

228. Ufanisi wa chanjo za Pfizer na Moderna – 3

Chanjo za Pfizer na Moderna zimethibitishwa kuwa na ufanisi mkubwa katika majaribio ya kitabibu. Ufanisi wa chanjo hizo pia umeonekana miongoni mwa watu waliochanjwa nazo.

Kwa mujibu wa makala yaliyoandikwa kwa kuzingatia matokeo ya majaribio ya kitabibu, chanjo ya Pfizer inapunguza hatari ya kupata dalili za virusi vya korona kwa asilimia 95. Kulingana na utafiti unaoangazia matokeo ya mpango wa utoaji chanjo nchini Israel, unaosifiwa kama mojawapo ya mipango inayotoa chanjo kwa kasi zaidi duniani, chanjo ya Pfizer inapunguza hatari ya kupata dalili za virusi hivyo kwa asilimia 94. Vilevile, inapunguza uwezekano wa kupata dalili kali kwa asilimia 92, na uwezekano wa maambukizi, ikiwa pamoja na yale yasiyoonesha dalili kwa asilimia 92.

Chanjo ya Moderna inapunguza hatari ya kupata dalili kwa asilimia 94.1, kwa mujibu wa tasnifu iliyojumuisha matokeo ya majaribio ya kitabibu.

Chanjo zote zimeonekana kuwa na ufanisi mkubwa dhidi ya aina mpya ya virusi iliyogundulika kwanza Uingereza ambayo kwa sasa inaenea kwa kasi nchini Japani na nchi zingine nyingi.

Makala yaliyochapishwa na Pfizer, BioNTech na kampuni zingine, yanasema majaribio ya maabara yalionesha kwamba chanjo ya Pfizer-BioNTech ina ufanisi wa kukabiliana na aina mpya za virusi hivyo ambazo ziligunduliwa kwa mara ya kwanza Uingereza na Brazil sawia na ilivyo kwa aina za awali. Yanasema chanjo hiyo pia ilifanikiwa kutoa kinga dhidi ya aina ile iliyogundulika kwanza Afrika Kusini, ingawa kwa ufanisi mdogo.

Kampuni ya Pfizer inasema chanjo hiyo imethibitishwa kuwa na ufanisi mkubwa nchini Israel ambako aina ya virusi ya Uingereza ilikuwa ikisambaa. Kadhalika inasema matokeo ya majaribio ya kitabibu nchini Afrika Kusini yanaashiria kuwa chanjo hiyo inasaidia vya kutosha kutoa kinga dhidi ya aina ile iliyobainika nchini humo.

Kwa mujibu wa makala yaliyochapishwa na Moderna na kampuni zingine, majaribio ya maabara yalionyesha kwamba chanjo ya Moderna inafanya kazi vizuri dhidi ya aina ile ya Uingereza sawia na ilivyo kwa aina za awali.

Hata hivyo, kwa aina ya virusi ya Afrika Kusini, kiwango cha kingamwili za kukabiliana na virusi zilizozalishwa na chanjo hiyo kilipungua hadi karibu moja ya sita ya viwango vilivyoonekana kwenye aina za awali, na hadi karibu theluthi moja kwa aina ya Brazil. Lakini Moderna inasema viwango hivyo bado vinatosha kupambana na aina hizo.

Kundi la utafiti la Wizara ya Afya na Kazi nchini Japani liliripoti takwimu iliyotathminiwa kuhusu chanjo ya Pfizer katika mkutano wa jopo la wataalam la wizara uliofanywa Aprili 30 juu ya athari za chanjo hiyo.

Ripoti hiyo inasema miongoni mwa waliopewa chanjo hiyo kwa mara ya kwanza, asilimia 23.2 walihisi uchovu, wakati idadi ilikuwa asilimia 69.6 miongoni mwa waliopatiwa dozi ya pili.
Aidha takwimu hizo zinaonesha asilimia 21.2 walipata maumivu ya kichwa baada ya dozi ya kwanza, na asilimia 53.7 baada ya dozi ya pili.
Na asilimia 3.3 ya waliochanjwa waliripotiwa kupata homa ya sentigredi 37.5 na zaidi baada ya dozi ya kwanza. Idadi ilikuwa asilimia 38.4 baada ya dozi ya pili.

Kuhusu chanjo ya Moderna, Kituo cha Kuzuia na Kudhibiti Magonjwa nchini Marekani kilitoa matokeo ya majaribio ya kitabibu yaliyohusisha watu wa umri wa miaka 18 hadi 64.

Kinasema asilimia 38.5 kati yao walihisi uchovu baada ya dozi ya kwanza na asilimia 67.6 baada ya dozi ya pili. Takwimu zinaonesha asilimia 35.4 walipata maumivu ya kichwa baada ya dozi ya kwanza na asilimia 62.8 baada ya dozi ya pili. Asilimia 0.9 ya waliochanjwa waliripoti kupata homa baada ya dozi ya kwanza wakati asilimia ilikuwa 17.4 baada ya dozi ya pili.

Taarifa hii ni sahihi kufikia Mei 12. Inapatikana kwenye tovuti ya NHK World Japan.

226. Mfanano wa chanjo kulingana na taarifa kutoka wizara ya afya ya Japani, Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa nchini Marekani, CDC pamoja na kampuni za kutengeneza dawa.

Serikali ya Japani imesaini mikataba ya kupokea chanjo kutoka kampuni za Pfizer na Moderna za Marekani pamoja na kampuni ya AstraZeneca ya Uingereza.

Miongoni mwa hizi, chanjo iliyoendelezwa na Pfizer-BioNTech na Moderna imetokana na ‘messenger RNA’, aina ya nyenzo za vinasaba. Zinajulikana kama chanjo za messenger RNA ama kwa kifupi, “chanjo za mRNA.”

Chanjo zote hizi hutolewa kwa kudungwa sindano ndani ya misuli.

Udungaji huo ni njia ya kudunga sindano kwenye misuli chini ya mafuta katika ngozi. Sindano hudungwa sehemu ya juu ya mkono, karibu na bega.

Nchini Japani, udungaji sindano wa ngozi unaofanywa kati ya ngozi na misuli hutumika kwenye utoaji chanjo kama zile za mafua makali. Mwili unaaminika kunyonya chanjo haraka kupitia udungaji sindano kwenye misuli tofauti na ule unaofanyika chini ya ngozi.

Chanjo ya Pfizer hutolewa kwa dozi mbili. Dozi ya pili kwa kawaida hutolewa majuma matatu baada ya ile ya kwanza.

Chanjo ya Moderna pia hutolewa kwa dozi mbili. Dozi ya pili kwa kawaida hutolewa baada ya majuma manne.

Chanjo zote hizi hutokana na dutu zinazobeba taarifa za kijenitiki ziitwazo mRNA. mRNA imekuwa ikifungashwa kwenye tabaka jembamba la mafuta kwenye chanjo hizi, lakini hazina uthabiti na zinaweza kuharibiwa kwa urahisi. Hali hii husababisha chanjo hizi kuhitajika kuhifadhiwa katika maeneo yenye uthabiti wa hali ya juu.

Awali, Pfizer ilisema kuwa chanjo yake inahitaji kutunzwa kwenye majokofu yenye nyuzijoto kati ya 90 na 60 hasi za selsiasi. Lakini tangu wakati huo, wizara ya afya ya Japani imepunguza hitaji hilo kwa kuzingatia data zilizowasilishwa na Pfizer. Wizara ilisema chanjo hiyo inaweza kuhifadhiwa kwenye joto kati ya 25 na 15 hasi kwa hadi siku 14. Pale uyeyushaji unapofanyika kabla ya mtu kudungwa, chanjo hizo zinapaswa kutunzwa kwenye jokofu lenye nyuzijoto kati ya mbili na nane na zinapaswa kutumika ndani ya siku tano.

Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa nchini Marekani, CDC kinasema kuwa chanjo ya Moderna inapaswa kuhifadhiwa kwenye majokofu yenye nyuzijoto kati ya 50 na 15 hasi. Kwenye taasisi za tiba, inaweza kutunzwa kwenye majokofu yenye nyuzijoto kati ya mbili na nane kwa siku 30. Inapaswa kuyeyushwa mathalan kwenye halijoto ya kawaida ya chumba kabla ya kudungwa. Chanjo ambazo bado hazijafunguliwa zinaweza kuhifadhiwa kwenye halijoto ya kawaida ya chumba iliyo kati ya nyuzi nane hadi 25, kwa hadi saa 24 kabla ya kutumika.

Taarifa hii ni sahihi hadi Mei 7. Inapatikana kwenye tovuti ya NHK World Japan.

211. Muda unaochukua kwa chanjo ya virusi vya korona kuanza kufanya kazi mwilini baada ya mtu kuchanjwa.

Timu ya utafiti ya Wizara ya Afya ya Japani imepokea ripoti kutoka kwa taasisi ya utabibu inayosema kuwa mfanyakazi wa afya mwenye umri wa miaka ya 20 aliambukizwa virusi baada ya kupatiwa chanjo ya Pfizer mwishoni mwa mwezi Februari, 2021.

Ripoti hiyo ilikuja siku sita baada ya mfanyakazi huyo kupewa dozi ya kwanza. Maafisa wanasema kuna uwezekano mkubwa kwamba aliambukizwa baada ya kuchanjwa. Alikuwa tayari ameruhusiwa kuondoka hospitalini baada ya kupona.

Timu hiyo inasema hakuna ongezeko la haraka la kingamwili baada ya mtu kuchanjwa. Kadhalika inasema inaaminika kuwa inachukua takribani siku 14 ili kuwa na kiwango fulani cha kingamaradhi baada ya kutolewa kwa dozi ya kwanza. Timu hiyo inatoa wito kwa watu kuendelea kuchukua hatua za kuzuia maambukizi hata baada ya kupatiwa chanjo.

Mwezi Machi mwaka huu, Kituo cha Udhibiti na Uzuiaji wa Magonjwa nchini Marekani kilipendekeza kwamba watu waliochanjwa bado wanakabiliwa na hatari ndogo ya kuambukizwa, na bado wanahitajika kuvaa barakoa wakiwa katika maeneo ya umma.

Chanjo, mbali na zile zilizotengenezwa kupambana na virusi vya korona, zina ufanisi katika kuchochea kuzalishwa kwa kingamwili ya watu. Lakini inachukua muda fulani kwa chanjo hizo kuwa na ufanisi baada ya mtu kuchanjwa.

Kampuni ya kutengeneza dawa ya Marekani ya Pfizer na mshirika wake BioNTech ya Ujerumani, zilitoa matokeo ya jaribio la kitabibu la chanjo yao ya virusi vya korona lililofanyika mwaka 2020.

Kampuni hizo ziliandaa makundi mawili kwa ajili ya jaribio hilo. Moja lilipatiwa chanjo bandia na lingine lilipatiwa chanjo hiyo. Jaribio hilo lilitathmini tofauti juu ya namna maambukizi yalivyoongezeka kati ya makundi haya mawili.

Ilibainika kuwa baada ya kupatiwa dozi ya kwanza ya chanjo, kiwango cha maambukizi mapya kilikuwa sawa kwa muda katika makundi yote mawili. Lakini katika muda wa takribani siku kumi na mbili baada ya kuchanjwa, ilibainika kuwa idadi ya visa vipya iliendelea kuongezeka katika kundi lililopewa chanjo bandia, ilhali idadi ya maambukizi mapya kwa kundi lililochanjwa ilikuwa ya wastani na ilipungua baadaye.

Utafiti huo unasema chanjo hiyo ina kiwango cha ufanisi cha asilimia 52.4 wakati wa kipindi cha kupokea dozi ya kwanza hadi ya pili. Kiwango cha ufanisi kiliongezeka hadi asilimia 94.8 siku saba baada ya kutolewa kwa dozi ya pili.

Profesa Nakayama Tetsuo ni mtaalam wa virolojia katika Chuo Kikuu cha Kitasato. Anasema chanjo za mRNA, kama ile iliyoendelezwa na kampuni za Pfizer na BioNTech, zinazifanya seli kutengeneza protini. Inachukua muda kwa protini kuzalisha kinga ndani ya mwili.

Profesa Nakayama anasema inaaminika kuchukua siku zisizopungua 10 hadi 14 tangu kutolewa kwa dozi ya kwanza kwa mfumo wa kinga kuanza kufanya kazi. Hadi hilo litakapojiri, hakuna kinga inayozalishwa hivyo hakuna kinga kabisa ya kupambana na maambukizi. Chanjo huanza kufanya kazi taratibu. Kingamwili ya uzimuaji inaendelezwa karibu juma moja baada ya kutolewa kwa dozi ya pili ili kutoa kingamaradhi thabiti dhidi ya maambukizi na kuzidhibiti dalili kali.

Hata hivyo, Profesa Nakayama anasema kudungwa sindano mbili za chanjo hakuzuii maambukizi kwa asilimia 100. Anaonya dhidi ya kufanya matembezi ya mara kwa mara na kuwasihi watu kuendelea kuchukua hatua za kuzuia maambukizi hata baada ya kuchanjwa.

Taarifa hii ni sahihi hadi Aprili 13. Inapatikana kwenye tovuti ya NHK World Japan.

209. Je, chanjo ya Sinopharm ina ufanisi kiasi gani?

Kampuni ya kitaifa ya kutengeneza dawa nchini China, Sinopharm inaendeleza chanjo zenye virusi vilivyouawa, ambapo virusi vinauawa wakati wa mchakato wa uendelezaji chanjo.

Kwa mujibu wa tovuti ya kampuni hiyo, mpango wa utoaji chanjo hiyo unatekelezwa nchini China na katika nchi zingine, na upo katika awamu za mwisho za majaribio ya kitabibu. Imeonesha ufanisi wa kiwango cha asilimia 86 katika Umoja wa Milki za Kiarabu, na asilimia 79.34 nchini China.

Taarifa hii ni sahihi kufikia Aprili 7. Inapatikana kwenye tovuti ya NHK World Japan.

208. Je, chanjo ya Sputnik V ya Urusi ina ufanisi kiasi gani?

Kituo cha Taifa cha Magonjwa ya Mlipuko na Mikrobiolojia cha Gamaleya kilitangaza matokeo ya majaribio ya kitabibu ya chanjo iliyotengenezwa nchini Urusi ya Sputnik V.

Kilisema miongoni mwa washiriki 19,866, dalili za virusi vya korona zilithibitishwa kwa watu 16 kati ya 14,964 waliopewa chanjo hiyo, na 62 kati ya 4,902 waliopatiwa chanjo bandia. Aidha kituo hicho kinasema chanjo hiyo ina kiwango cha ufanisi wa asilimia 91.6.

Kituo hicho kinasema watu wote 20 waliopata dalili kali walipatiwa chanjo bandia. Kwa mujibu wa kituo hicho, chanjo hiyo ina ufanisi wa asilimia 100 katika kuzuia dalili kali siku ya 21 baada ya kuchanjwa nayo. Mpango wa utoaji chanjo ya Sputnik V unaendelea nchini Urusi na nchi zingine.

207. Je, chanjo ya Novavax ina ufanisi kiasi gani?

Kampuni hiyo ya bioteknolojia ya Marekani ilitangaza matokeo ya majaribio yake ya kitabibu yaliyofanyika nchini Uingereza.

Inasema miongoni mwa watu zaidi ya 15,000 walioshiriki, dalili za virusi hivyo zilithibitishwa kwa watu 6 waliopewa chanjo hiyo na 56 waliopatiwa chanjo bandia. Aidha kampuni hiyo inasema chanjo hiyo ina kiwango cha ufanisi wa asilimia 89.3.

204. Je, ufanisi wa chanjo ya AstraZeneca ukoje?

Kampuni ya kutengeneza dawa ya Uingereza inasema chanjo yake ina ufanisi wa asilimia 76 katika kuzuia dalili za virusi vya korona. AstraZeneca ilitangaza Machi 25 kwamba ilithibitisha dalili katika watu 190 kati ya 32,449 walioshiriki awamu ya mwisho ya majaribio ya kitabibu nchini Marekani, Chile na Peru na kulinganisha data za wale waliopewa chanjo na chanjo bandia.

AstraZeneca ilipunguza kiwango cha ufanisi kwa alama 3 baada ya idara ya afya ya Marekani kuiasa kutoa data mpya. Taasisi ya Taifa ya Mzio na Magonjwa Ambukizi nchini Marekani ilisema uchambuzi wa muda wa AstraZeneca inawezekana ulijumuisha taarifa zilizopitwa na wakati ambazo “huenda zilitoa mtazamo usiokamilika wa data za ufanisi.”

AstraZeneca inasema kulikuwa na visa vinane hatari, lakini vyote vilitokea katika kundi la waliopewa chanjo bandia, na hivyo, chanjo yake ina ufanisi wa asilimia 100 katika kuzuia ugonjwa hatari.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Machi 31. Inapatikana katika tovuti ya NHK World Japan.

203. Chanjo ya Moderna imefanikiwa kwa kiasi gani?

Matokeo yaliyotolewa na kampuni ya bioteknolojia ya Marekani ya Moderna yanaonyesha kwamba watu 30,420 walishiriki awamu ya mwisho ya majaribio ya kitabibu ya chanjo yake ya virusi vya korona.

Inasema washiriki 15,210 walipatiwa chanjo na 11 kati yao kuonyesha dalili za virusi vya korona, ilhali watu 15,210 walipewa chanjo bandia na 185 kati yao kuwa na dalili.

Kwa hiyo, kampuni hiyo inasema kiwango cha ufanisi wa chanjo yake ni asilimia 94.1.

201. Baadhi ya chapa za chanjo na ufanisi wake.

Watengenezaji wengi wa chanjo za virusi vya korona wametoa matokeo ya majaribio yao ya kitabibu ili kuonyesha ni kwa namna gani chanjo zao zina ufanisi.

Ufanisi wa chanjo unatathminiwa kwa kulinganisha kundi la watu waliopatiwa chanjo hiyo na lingine la watu waliopatiwa placebo, yaani chanjo bandia.

Ikiwa uwiano wa watu waliopata dalili za virusi vya korona ni mdogo kwa kundi la watu waliopatiwa chanjo kuliko ule wa kundi lililopatiwa chanjo bandia, chanjo hiyo inachukuliwa kuwa fanisi katika kuzuia ugonjwa.

Chanjo iliyotengenezwa kwa ushirikiano wa kampuni kubwa ya famasia ya Marekani ya Pfizer na kampuni mshirika wake ya BioNTech kutoka Ujerumani, na chanjo iliyotengenezwa na kampuni nyingine ya Marekani ya Moderna, zote zilibainika kuwa na kiwango cha ufanisi cha zaidi ya asilimia 90 katika majaribio ya kitabibu yaliyolenga makumi ya maelfu ya watu. Chanjo hizo mbili ni zile ambazo wizara ya afya ya Japani imezisainia mikataba.

Kiwango cha ufanisi wa zaidi ya asilimia 90 kina maana gani?

Wacha tuchukulie kwamba watu 100 wamepata dalili baada ya kipindi fulani baada ya kupewa dawa bandia, huku chini ya watu kumi miongoni mwa waliopatiwa chanjo wakipata dalili baada ya kipindi sawia. Kwa kulinganisha takwimu hizi mbili, chanjo inabainika kuchangia kuzuia maambukizi ya virusi vya korona kwa zaidi ya asilimia 90 ya watu.

Lakini tunapaswa kuzingatia kuwa wale waliochanjwa bado wanaweza kuambukizwa virusi. Hivyo, ni muhimu kuendelea kuchukua tahadhari kama vile kuvaa barakoa na kuepuka kile kinachoitwa “Three Cs”, yaani maeneo ya ndani, maeneo yenye msongamano wa watu na yale yenye kukaribiana na watu, hata baada ya mpango wa utoaji chanjo kukamilika kabisa.

Katika sehemu zifuatazo, tutaangalia kila chanjo kubwa zinazotumika duniani kuona namna zinavyoweza kuwa fanisi.

Kwanza, tunaangalia ufanisi wa chanjo iliyotengenezwa na kampuni ya Marekani ya Pfizer na kampuni mshirika wake ya BioNTech ya Ujerumani.

Tathmini ya matokeo ya majaribio ya kitabibu ya chanjo hiyo inasema watu 43,448 walishiriki awamu ya mwisho ya majaribio.

Ufanisi wa chanjo ulitathminiwa kwa kulinganisha kundi la watu waliopata chanjo na lingine la watu waliopewa chanjo bandia.

Katika uchambuzi wa watu 18,198 kati ya watu 21,720 ambao awali hawakuambukizwa virusi vya korona na kupata chanjo, watu wanane walipata dalili baada ya majaribio.

Miongoni mwa watu 18,325 kati ya 21,728 waliopewa chanjo bandia, watu 162 walipata dalili. Hii ina maana kuwa chanjo ilikuwa na ufanisi wa asilimia 95 katika kuzuia dalili za virusi hivyo.

199. Tunaendelea kuangazia sifa za aina mpya za virusi na ufanisi wa chanjo. Tuziangazie kwa kuzilinganisha sifa za aina mpya za virusi vya korona.

Nchini Japani, mtu aliyeingia nchini humo kutoka Ufilipino Februari 25 mwaka huu, alithibitika kuambukizwa aina mpya ya virusi vipya vya korona vilivyo tofauti na vile vilivyoenea kwenye nchi za Uingereza, Afrika Kusini au Brazil. Aina hii ya virusi ina mabadiliko yajulikanayo kama N501Y pamoja na mabadiliko makubwa yaitwayo E484K, yanayoviwezesha virusi kuepuka kushambuliwa na kingamwili.

Taasisi ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi ya Japani imesema kuwa aina iliyoripotiwa awali nchini Ufilipino, inaweza kuambukiza zaidi kulinganisha na aina iliyoenea mwanzoni, na kwamba inaweza kuwa tishio zaidi kama aina zingine mpya za virusi zinazoenea kote ulimwenguni.

Japani pia imebaini karibu visa 400 vya aina nyingine ya virusi vyenye mabadiliko ya E484K hadi kufikia Machi 3 mwaka huu. Virusi hivi havina mabadiliko ya N501, hali inayomaanisha kuwa hakuna uwezekano wa virusi hivyo kuambukiza kirahisi kulinganisha na vile vya awali. Lakini watafiti wanasema mabadiliko kadhaa yaliyopo kwenye virusi hivyo yanaweza kutokea nchini Japani.

Taasisi ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi imevitenga aina hii kama “aina inayovutia nadhari.” Watafiti wanaichunguza zaidi aina hii kupitia tathmini ya jeni na njia zinginezo.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Machi 24 mwaka huu. Pia inapatikana kwenye tovuti ya NHK World Japan.

198. Aina mpya ya virusi vilivyobainika kwanza nchini Brazil

Virusi hivyo viliripotiwa kwa mara ya kwanza nchini Japani Januari 6 mwaka huu kutoka kwa msafiri aliyetokea nchini Brazil.

Virusi hivyo vinaaminika kubainika kwanza huko Manaus kaskazini mwa Brazil Disemba 4, 2020. Hadi kufikia mwezi Januari mwaka huu, asilimia 91 ya visa vilivyoripotiwa huko Manaus vinasemekana kuwa ni maambukizi yaliyotokana na aina hiyo.

Shirika la Afya Duniani - WHO linasema aina hiyo “inaambukiza zaidi kulinganisha na ile iliyokuwa ikienea awali” na kwamba nchi na maeneo 32 kote duniani zimeripoti visa vya maambukizi yatokanayo na aina hiyo hadi kufikia Machi 9. Lilisema kuwa madhara yayokanayo na hiyo yamekuwa na “athari ndogo.”

WHO inasema kuambukizwa tena kutokanako na aina hii kumekuwa kukiripotiwa. Hii ni kwa sababu aina hii, pamoja na ile iliyoripotiwa kwanza nchini Afrika Kusini, imeibua mabadiliko ya muonekano yajulikanayo kama E484K, yanayoviwezesha virusi kuepuka mashambulizi ya kingamwili.

WHO imesema kuwa uwezekano wa madhara kwenye chanjo unaendelea kufanyiwa uchunguzi.

197. Swali lingine ni juu ya ufanisi wa chanjo dhidi ya aina mpya ya virusi na linauliza, “Tunafahamu nini kuhusiana na aina mpya ya virusi iliyothibitishwa kwanza nchini Afrika Kusini?”

Aina mpya ya virusi vya korona ya Afrika Kusini inaaminika kuibuka kwanza mapema mwezi Agosti mwaka jana. Katika tathmini ya kina iliyofanywa na mamlaka za afya za Afrika Kusini katikati ya mwezi Novemba, aina hiyo ilihusishwa na visa vingi vya maambukizi ya virusi vya korona.

Shirika la Afya Duniani - WHO lilisema kuwa aina hiyo ya Afrika Kusini ina uwezo wa kusababisha maambukizi kwa asilimia 50 zaidi kulinganisha na aina iliyokuwa ikienea awali, na imebainika katika nchi na maeneo 58 hadi kufikia Machi 9. Hata hivyo, WHO ilisema hakuna uthibitisho wowote unaoashiria kuwa aina hiyo inasababisha watu walioambukizwa kuumwa sana.

Virusi hivyo vya Afrika Kusini vina mabadiliko yaitwayo E484K, yanayoviwezesha kukwepa shambulio la kingamwili zinazozalishwa kwenye miili yetu na kuashiria uwezekano wa hatari kubwa za kuambukizwa tena.

Pia kuna tafiti zinazoonyesha kuwa kingamwili zilizoongezwa na chanjo zina ufanisi mdogo dhidi ya aina mpya ya virusi vya Afrika Kusini. Watengenezaji wa chanjo wanasema bidhaa zao zimesalia kuwa na ufanisi wa kiutendaji dhidi ya virusi hivyo, lakini bado wanaendelea kuutafiti ufanisi huo.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Machi 22. Pia inapatikana kwenye tovuti ya NHK World Japan.

196. Swali linalofuata ni juu ya ufanisi wa chanjo dhidi ya aina mpya ya virusi na linauliza, “Nini tunachokifahamu kuhusiana na aina ya virusi iliyothibitishwa kwanza nchini Uingereza?”

Aina hii mpya ya virusi inaaminika kwanza kuibukia nchini Uingereza mapema mwezi Disemba mwaka jana. Lakini tathmini ya taarifa za kina imedhihirisha kuwa kulikuwepo na wagonjwa walioambukizwa aina hiyo mapema Septemba 20.

Kituo cha Kuzuia na Kudhibiti Magonjwa Barani Ulaya kimesema kuwa tafiti kadhaa zimebaini kwamba aina hii mpya ya virusi ina uwezo zaidi wa kuambukiza kwa asilimia 36 hadi 75 kulinganisha na aina za awali za virusi hivyo.

Mwanzoni mwa mwezi Disemba mwaka jana, Uingereza ilishuhudia visa vipya kati ya 10,000 na 20,000 kwa siku. Lakini takwimu hizo ziliongezeka hadi juu ya kiwango cha 50,000 mwishoni mwa mwezi Disemba. Mwezi Januari mwaka huu, takwimu hizo zilipita 60,000 katika baadhi ya siku. Watafiti wanaamini ongezeko hilo kwa kiasi kikubwa limetokana na kuenea kwa aina mpya ya virusi.

Shirika la Afya Duniani lilisema kuwa aina hii mpya ya virusi imethibitishwa kwenye nchi na maeneo 111 kote duniani kufikia Machi 9.

Serikali ya Uingereza inashuku aina hii mpya inaweza kuhusika kwa kiasi kikubwa katika kuongezeka kwa idadi ya watu wanaolazwa hospitalini na hatari za vifo kulinganisha na virusi vya kawaida. Watafiti wanafanya tafiti kuthibitisha nadharia hii. Habari njema ni kwamba aina hii mpya ya virusi inaaminika kutokuwa na madhara makubwa katika ufanisi wa chanjo.

195. Je, ni aina ipi mpya ya virusi ambayo tunapaswa kuchukua tahadhari ya kipekee dhidi yake?

Aina mpya ya virusi vipya vya korona imethibitishwa kwenye nchi na maeneo zaidi ya 100 kote duniani. Kwenye virusi vipya vya korona, mabadiliko hutokea katika takribani maeneo mawili ya taarifa za maumbile yake ndani ya mwezi mmoja. Hata hivyo, kwa kawaida, mabadiliko haya hayana athari kwenye uwezo wa virusi kuambukiza na kusababisha magonjwa.

Lakini mabadiliko hayo yanaweza kufanya baadhi ya aina ya virusi kuweza kuambukizwa zaidi au kuwa sugu dhidi ya shambulizi la mfumo wa kinga. Shirika la Afya Duniani na serikali za duniani kote zimevitambua kama “virusi vyenye kuzua wasiwasi mkubwa” na kuongeza jitihada katika ufuatiliaji.

Kuna aina tatu mpya za virusi zilizowekewa tahadhari kubwa. Mojawapo ni iliyoibukia nchini Uingereza, nyingine iliyothibitishwa Afrika Kusini na kisha ile inayoenea nchini Brazil. Virusi hivyo vina mabadiliko sawa yaitwayo N501Y. Watafiti wanaamini kuwa vimejiletea mabadiliko ya muonekano wake, kuvisaidia kuingia kwenye seli za binadamu, hivyo vinaweza kuingia kiurahisi kwa watu wengine.

Katika maswali yanayofuata, tutaangazia sifa ya kila aina mpya ya virusi hivyo na ufanisi wa chanjo dhidi yake.

194. Swali linalofuata ni, nini maana ya kingamaradhi ya kundi?

Pale zaidi ya idadi fulani ya watu inapokuwa na kingamaradhi dhidi ya virusi ama kijidudu, basi hata ikiwa mtu ataambukizwa, maambukizi hayo hayasambai kwa wengine na hivyo kupata hali inayofahamika kama “kingamaradhi ya kundi.”

Lazima ifahamike kwamba kwa kutegemea aina ya ugonjwa ulioambukizwa, asilimia ya watu wanaohitaji kupatiwa chanjo ili kufikia kingamaradhi ya kundi inatofautiana. Wataalam pia wanasema kuna visa ambapo chanjo inasaidia kumzuia mtu kutoumwa sana, lakini si fanisi katika kudhibiti msambao wa virusi. Hii ina maana kwamba kingamaradhi ya kundi haiwezi kufikiwa hata ikiwa watu wengi wamechanjwa. Wanasema bado haijawa wazi ikiwa kingamaradhi ya kundi inaweza kupatikana kupitia utoaji wa chanjo, inapokuja kwa virusi vya korona.

193. Swali linalofuata ni kwa namna gani tunapaswa kujilinda dhidi ya udanganyifu na ulaghai unaotokana na chanjo?

Shirika la Masuala ya Mlaji la serikali ya Japani linasema limepokea maombi ya ushauri kutoka kwa watu waliopokea simu za udanganyifu ama baruapepe zenye mashaka zinazohusiana na chanjo za virusi vipya korona. Katika kisa kimoja, mtu mmoja alipokea simu kutoka kwa mtu aliyesingizia kuwa afisa wa serikali ya eneo, akimtaka mtu huyo atume yeni 100,000 kwa akaunti maalum ya benki haraka ili apatiwe chanjo. Iliripotiwa kuwa mpigaji simu alisema fedha hizo zingerudishwa baadaye.

Katika kisa kingine kilichoelezewa na Kituo cha Taifa cha Masuala ya Mlaji, mtu mmoja alipokea ujumbe mfupi wenye jina la waziri wa taifa, ukimtaka atumie tovuti fulani ili kupewa kipaumbele katika utoaji chanjo.

Maafisa wa shirika hilo wanasema serikali za maeneo hazitaitisha malipo ama taarifa binafsi kupitia kwa simu ama baruapepe zinazohusiana na chanjo ya virusi vya korona. Utafiti uliofanywa na shirika hilo unaonyesha kuwa asilimia 80 ya watu walioathiriwa ama waliopatwa na matatizo yanayohusiana na udanganyifu unaohusu virusi vya korona walisema, walidhania hawatalaghaiwa kwa sababu walichukua tahadhari ya kutosha dhidi ya udanganyifu.

Kituo cha Taifa cha Masuala ya Mlaji kinatoa huduma ya ushauri bila malipo kwa njia ya simu kwa watu waliopokea simu ama baruapepe za kutilia shaka zinazoonekana kuchochewa na mpango wa utoaji chanjo ya virusi vya korona. Ushauri unatolewa kwa lugha ya Kijapani pekee. Namba ya simu ni 0120 797 188. Huduma hiyo inapatikana kuanzia saa nne kamili asubuhi hadi saa kumi alasiri Jumatatu hadi Ijumaa na Jumamosi na Jumapili.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Machi 16.

192. Tunaweza kuambukizwa virusi vya korona kwa kupewa chanjo ya virusi hivyo?

Haiwezekani tuambukizwe virusi vya korona kutokana na aina ya chanjo inayotumika nchini Japani, ambayo ni “chanjo ya jeni.”

Chanjo hiyo ina tando za nyenzo ya jeni inayoitwa “mRNA,” inayojumuisha taarifa za jeni kutoka “protini inayochomoza kwenye membreni ya nje ya virusi. “mRNA inafanya kazi ya uongozaji ndani ya seli ya binadamu ili kutengeneza protini hizo.

mRNA inasemekana kuwa salama zaidi kwa sababu inakosa uthabiti na pale inapotumika kama chanjo inayeyuka mara moja na haibaki kwenye mwili. Pia inadhaniwa kuwa salama kwa sababu haiingii kwenye kiini cha seli kilicho na jeni za binadamu.

Kuna visa vichache ambapo chanjo husababisha ugonjwa endapo chanjo yenye kirusi hai kilichodhoofishwa kama vile chanjo dhidi ya polio, inachomwa. Aina hii inatumia virusi hai vilivyodhoofishwa.

Chanjo zote za virusi vya korona zinazotumika kwa sasa ni salama dhidi ya hatari kwa sababu hakuna yoyote iliyo na kirusi hai.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Machi 15.
Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Machi 17. Inapatikana kwenye tovuti ya NHK World Japan.

191. Swali linalofuata ni ikiwa kudungwa sindano kwenye misuli, ambayo ni njia inayotumiwa kutoa chanjo za virusi vya korona, husababisha maumivu makali?

Nyingi ya chanjo za virusi vya korona zimetengenezwa ili kutolewa kwa kudunga sindano ndani ya misuli. Lakini wataalam wanasema kwa sababu tu chanjo inatolewa kwa kudunga sindano ndani kabisa ya misuli, haimaanishi ni lazima inasababisha maumivu makali zaidi. Katika udungaji sindano kwenye misuli, chanjo zinaingizwa kwenye msuli chini ya mafuta yaliyo chini ya ngozi. Sindano inaingizwa katika pembe ya nyuzi 90 kwenye upande wa juu wa mkono.

Nchini Japani, udungaji sindano chini ya ngozi, hii ikiwa ni sindano inayodungwa kwenye tabaka lililopo kati ya ngozi na msuli, ni njia inayotumiwa mno katika utoaji wa chanjo, zikiwemo zile za mafua. Lakini sindano zinazodungwa ndani ya misuli zinaaminika kuruhusu chanjo kufyonzwa haraka.

Okada Kenji ni Profesa wa Chuo cha Uuguzi cha Fukuoka na Rais wa Chama cha Masuala ya Chanjo nchini Japani. Anasema nje ya Japani, udungaji sindano ndani ya misuli kwa kawaida hutumika kwa utoaji wa chanjo za mara kwa mara. Anasema si sindano zote zinazodungwa ndani ya misuli zinazosababisha maumivu makali kuliko zile zinazodungwa chini ya ngozi. Anaongeza kuwa inategemea vitu vilivyotumiwa kuitengeneza chanjo hiyo.

Pia anasema kuwa ile dhana ya maumivu hutofautiana sana miongoni mwa watu. Lakini Profesa Okada pia anasema kumekuwepo na ripoti kutoka mataifa mengine kuwa chanjo za virusi vya korona zinasababisha maumivu makali mno kwenye eneo palipodungwa sindano, kuliko sindano zingine za chanjo. Anasema wafanyakazi wa afya wanapaswa kutoa maelezo ya kina kuwaandaa watu kudungwa sindano hiyo, ilhali wale wanaodungwa wanashauriwa kujaribu na kuepuka kuiangalia sindano kwa kuelekeza shabaha ya mawazo yao kwa kitu kingine.

Taarifa hii ni sahihi hadi Machi 12. Inapatikana kwenye tovuti ya NHK World Japan.

190. Nawazia iwapo napaswa kupewa chanjo ya virusi vya korona. Napaswa kufanya nini?

Okabe Nobuhiko ni Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Afya ya Umma Mjini Kawasaki. Yeye pia ni mwanachama wa jopo la ushauri la serikali ya Japani la kukabiliana na virusi vya korona. Anasema hadi kufikia sasa, inaonekana hakuna athari za kutia hofu sana zitokanazo na chanjo hizo, kwa kuangalia walau data za majaribio ya kitabibu na taarifa kutoka mataifa ambako mipango ya utoaji chanjo tayari inaendelea.

Anasema ikilinganishwa na influenza na chanjo zingine, chanjo za virusi vya korona zinaweza zikasababisha maumivu zaidi wakati wa kudungwa sindano, na eneo palipodungwa sindano kuvimba kwa muda mrefu. Lakini anasema data zilizokusanywa hadi sasa zinaonyesha kuwa katika visa vingi, dalili zinatoweka baada ya muda fulani.

Hata hivyo, Okabe pia anasema kunapaswa kuwepo mfumo unaowaruhusu watu kutafuta ushauri wa wataalam ama huduma za kitabibu pale wanapohisi kuhofu.

Okabe anasema iwapo mtu yeyote atamuuliza ikiwa atachanjwa, jibu lake ni ndiyo. Anasema unapoambukizwa virusi vya korona, unaweza tu kupatwa na dalili zisizokuwa kali, lakini pia huenda ukaumwa sana. Anasema kwa kulinganisha hatari za kuumwa sana kutokana na virusi vya korona na hatari za kupatwa na madhara makubwa kutokana na chanjo hizo, anaamini manufaa ya chanjo kuzuia dalili ni makubwa zaidi kuliko hatari za madhara yake.

Lakini anasema baadhi ya watu wanashindwa kupata chanjo hata kama wanataka, kutokana na hali zao, na baadhi ya watu wanakataa kuchanjwa bila kujali hali yoyote ile. Anasema uamuzi wa mtu binafsi unapaswa kuheshimiwa.

Taarifa hii ni sahihi hadi Machi 8.

189. Swali linalofuata ni je, ”Nawazia ikiwa napaswa kupatiwa chanjo ya virusi vya korona. Napaswa kufanya nini?”

Kuna taarifa lukuki zinazoenea kuhusu chanjo za virusi vya korona, zinazowaacha watu wakijiuliza iwapo wanapaswa kuchanjwa.

Profesa Ishii Ken wa Taasisi ya Sayansi Tiba ya Chuo Kikuu cha Tokyo ni mtafiti kinara wa chanjo, mwenye tajiriba ya kufanya kazi na Mamlaka ya Chakula na Dawa ya Marekani wakati wa kukagua majaribio ya kitabibu ya chanjo hizo. Hizi hapa fikra zake kuhusu chanjo zilizopangwa kutumika nchini Japani.

Anasema ufanisi na usalama wa chanjo zote, unaungwa mkono na data zenye uwazi. Anasema inaonekana hazina tatizo, na kwamba alikuwa na wasiwasi juu ya kasi ya uendelezaji wa chanjo hizo. Lakini baada ya kuona idadi ya watu walioshiriki majaribio ya kitabibu pamoja na usahihi wake, alifikia hitimisho kuwa hakuna tatizo kabisa.

Anasema hawezi kufutilia mbali kabisa uwezekano wa athari za muda mrefu kutokea kutokana na chanjo hizo, na kwamba bado haijabainika ikiwa athari zozote mbaya zitatokea katika kipindi cha miaka kadhaa ya utoaji chanjo. Lakini anasema, isipokuwa hatari kama hizo zinazoweza kutokea miaka kadhaa ijayo, kila kitu ni bayana. Anaongeza kuwa manufaa ya kuchanjwa yanazidi hatari za kuambukizwa virusi na kupata dalili kali.

Profesa Ishii anasema kwa sababu chanjo kwa sasa ziko tayari, watu binafsi pamoja na jamii, wanakabiliwa na swali la ikiwa wanapaswa kuchanjwa. Anasema, kwa mtazamo wa kisayansi, watu walio katika kundi lenye hatari kubwa ya kuambukizwa, hususan wale wenye umri wa miaka 65 na zaidi, wanapaswa kuchanjwa. Pia anapendekeza kuwa ndugu wa familia zenye wazee ama watu walio na matatizo ya kiafya, wanapaswa kuchanjwa ili kuwalinda.

Kulingana naye, hatari ya maambukizi bado itakuwepo ikiwa watu wataamua kutochanjwa. Anasema ni juu yako kuamua ikiwa utachanjwa au la, lakini uamuzi unapaswa kufanywa kwa kushauriana na ndugu wa familia na kwa kutilia maanani watu walio karibu nawe.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Machi 5. Inapatikana kwenye tovuti ya NHK World Japan.

188. Je, bado unahitaji kuvaa barakoa, kuepuka sehemu za ndani, zilizosongamana watu, ama kuchukua hatua zingine dhidi ya virusi vya korona hata baada ya kuchanjwa?

Wataalam wanasema watu wanapaswa kuendelea kuchukua hatua kama hizo kwa sasa, hadi pale ufanisi wa chanjo uthibitishwe katika jamii zao.

Chanjo inayotumika nchini Japani, ilithibitishwa kuwa na ufanisi wa asilimia 95 katika kuzuia dalili wakati wa majaribio ya kitabibu. Lakini hiyo haimaanishi chanjo zinaweza kuzuia kikamilifu kuanza kwa dalili.

Pia bado haifahamiki iwapo chanjo inaweza kuzuia watu kuambukizwa virusi. Hata baada ya kuchanjwa, bado unaweza kuambukizwa ikiwa unalindwa dhidi ya kupata dalili. Hiyo ndio sababu, bila kuchukua hatua za kukabiliana na virusi, bado unaweza kuwa katika hatari ya kueneza virusi kwa watu walio karibu nawe.

Utoaji chanjo ulianza kote duniani muda mfupi uliopita. Kituo Udhibiti na Uzuiaji wa Magonjwa nchini Marekani, CDC kinasema data zaidi zitahitajika, ili kuthibitisha iwapo athari za chanjo zitadumu kwa muda mrefu.

CDC na wataalam wengine wanasema baada ya kuchanjwa, watu wanapaswa kuendelea kuvaa barakoa, kutumia viuaviini, kuepuka maeneo yenye watu wengi na kuchukua hatua zingine za kuzuia maambukizi ya virusi kwa wakati huu.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Machi 4.

187. Swali lingine linahusiana na iwapo inakubalika kutumia dawa zinazopunguza homa ama maumivu, ikiwa utapatwa na homa au kuhisi maumivu baada ya kupewa chanjo.

Inafahamika kuwa baadhi ya watu hupata homa au kuhisi maumivu baada ya kupewa chanjo ya virusi vya korona. Katika visa vingi, hali hiyo hutokea ndani ya siku moja ama mbili baada ya kuchanjwa. Dalili hizi kwa kawaida hudumu kwa siku chache tu. Tovuti ya wizara ya afya inasema watu wanaopatwa na dalili hizi “wanapaswa kutumia dawa sahihi za kupunguza homa au maumivu na kuona hali zao zinavyoendelea siku chache zinazofuata.”

Hata hivyo, hatua zinapaswa kuchukuliwa kutembelea taasisi ya tiba au kumwona daktari iwapo homa itaendelea kwa zaidi ya siku mbili. Mojawapo wa hatua hizi pia inapaswa kuchukuliwa pale hali zingine mbaya au dalili ambazo bado hazijaripotiwa zitatokea. Nakayama Tetsuo ni profesa aliyeteuliwa hasa katika Chuo Kikuu cha Kitasato ambaye ni mtaalam wa masuala ya chanjo. Anasema dalili kama vile homa na maumivu, hutokea pale kingamaradhi ya mwili inapofanya kazi. Alisema kutumia dawa za kupunguza homa au maumivu, hakutakuwa na athari kwa kingamaradhi.

Isitoshe, Nakayama alisema ikiwa mtu atapatwa na homa kali ya zaidi ya nyuzijoto 38.5 za selsiasi ama kukumbwa na maumivu makali, ingekuwa bora kutumia dawa za kupunguza homa au baadhi ya dawa za kupunguza maumivu.

Hata hivyo, Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa nchini Marekani, kinawasihi watu kuhadhari juu ya swala la iwapo wanapaswa kutumia dawa za kupunguza homa au zile za kupambana na maumivu yoyote kabla ya kuchanjwa. Kilisema hatua kama hizo “hazipendekezwi” kwani haijabainika ni kwa namna gani zinavyoweza kuiathiri chanjo yenyewe.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Machi 3. Pia inapatikana kwenye tovuti ya NHK World Japan.

186. Je, ni vema kwa kina mama wajawazito kuchanjwa?

Mnamo mwezi Januari mwaka huu, Chama cha Japani cha Magonjwa Ambukizi ya Uzazi na Jinakolojia na Chama cha Japani cha Uzazi na Jinakolojia, vilitoa taarifa ifuatayo kuhusiana na namna chanjo ya virusi vpya vya korona inaweza kuwaathiri wanawake wajawazito.

Taarifa hiyo inasema hakuna vifo vilivyoripotiwa wakati wa majaribio ya kitabibu. Lakini sera kuhusiana na chanjo zinatofautiana baina ya nchi. Huku Marekani ikisema wanawake wajawazito wanapaswa kuchanjwa, Uingereza haishauri wanawake kama hao kuchanjwa ikitaja kukosekana kwa data za kutosha kuwa sababu.

Vyama hivyo viwili vya tiba nchini Japani vilihitimisha kwamba kuhusiana na utoaji chanjo kwa wanawake wajawazito, usalama wa chanjo, athari za kati hadi muda mrefu, na ikiwa kuna athari zozote mbaya kwa kijusi na mtoto aliyezaliwa, bado hazijathibitishwa. Wanasema hawawazuii wanawake kama hao kupata chanjo, lakini kwamba iwapo watachanjwa, wataalam wa tiba wanapaswa kuwapa wanawake hao maelezo ya kina na kufuatilia hali ya kijusi kabla ya kuwachanja.

Vyama hivyo pia vinapendekeza kuwa wanawake wanaodhamiria kuwa wajawazito wapewe chanjo, ikiwezekana, kabla ya kupata ujauzito. Wanatoa wito kwa wanawake kama hao, kutangulia kutafuta ushauri kutoka kwa madaktari wao wa masuala ya uzazi na wanajinakolojia.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Machi 2.

185. Swali lingine ni je, unahitaji kupewa chanjo ikiwa tayari uliugua ugonjwa wa virusi vya korona?

Hapo awali katika kipindi hiki, tuliripoti kuwa Shirika la Afya Duniani, WHO lilishauri kupatiwa kinga katika visa kama hivyo. Kituo cha Udhibiti na Uzuiaji wa Magonjwa nchini Marekani, CDC pia kinatoa wito kwa wagonjwa waliopona kupata chanjo.

Kwenye tovuti yake, CDC inazungumzia chanjo aina ya mRNA iliyotengenezwa na Pfizer na Moderna zinazotolewa nchini Marekani. Inaeleza kwamba takwimu za majaribio ya kitabibu zinaonyesha chanjo hizo ni salama kwa watu ambao awali waliambukizwa virusi vya korona.

Inasema “Unapaswa kupata chanjo bila kujali iwapo uliugua virusi hivyo. Hiyo ni kwa sababu wataalam bado hawafahamu ni kwa muda gani hautaweza kuugua tena baada ya kupona.” Inasema kiwango cha kingamwili za asili kinachopatikana kutokana na maambukizi kinatofautiana kutoka kwa mtu hadi mwingine.

CDC imeongeza kuwa “Ikiwa ulitibiwa virusi vya korona kwa kingamwili za ‘monoclonal’ ama majimaji yaliyo kwenye damu yaliyorejea baada ya mtu kuugua, yaani convalescent plasma, unapaswa kusubiri kwa siku 90 kabla ya kupata chanjo ya virusi vya korona.” Tovuti hiyo inasema unapaswa kuzungumza na daktari wako.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Machi 1. Pia inaweza kupatikana kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

184. Je, Inawezekana chanjo kusababisha mzio mkali, yaani anaphylaxis?

Mzio mkali baada ya chanjo umekuwa ukiripotiwa nchini Marekani na maeneo mengine ambako mipango ya utoaji chanjo imeanza mapema.

Ripoti moja ya Kituo cha Udhibiti na Uzuiaji wa Magonjwa nchini Marekani, CDC inasema visa 21 vya mzio mkali vilibainika baada ya kutolewa dozi za kwanza takribani milioni 1.9 za chanjo aina ya Pfizer-BioNTech kipindi cha Disemba 14 na 23.

CDC pia iliripoti kuwa visa kumi vya mzio mkali vilibainika baada ya dozi za kwanza milioni 4 na ushei za chanjo aina ya Moderna katika kipindi cha Disemba 21 na Januari 10.

CDC inasema visa vingi vya mzio mkali vilitokea kwa watu wenye historia ya mzio na kwamba kila mmoja ambaye taarifa zake za ufuatiliaji zilipatikana alipona.
Kituo hicho kinasema ni nadra kutokea mzio mkali baada ya chanjo lakini unaweza kuhatarisha maisha na unahitaji tiba ya haraka.

CDC inasema maeneo ya kupatia chanjo yanapaswa kuwa na vifaa na wafanyakazi sahihi ili kuhakikisha yeyote anayeshukiwa kuwa na mzio mkali anatibiwa haraka kwa dawa, kwa mfano epinefirini. Kinasema watu wote wanaopata chanjo wanapaswa kushauriwa kutafuta haraka huduma ya kitabibu ikiwa wataonyesha dalili za mzio baada ya kuondoka kwenye eneo la kupata chanjo.

Mzio mkali ni kuwa na dalili kali za mzio. Lakini madaktari wanasema ni nadra kusababisha kifo endapo utatibiwa haraka, ikiwa ni pamoja na kuchomwa sindano ya epinefirini.

Wizara ya Afya ya Japani inaeleza kwenye tovuti yake kwamba maeneo ya chanjo na taasisi za tiba zimewekewa dawa zinazohitajika na vifaa vingine ili ziweze kutibu haraka mzio mkali baada ya chanjo.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Feb 26.

183. Swali lingine ni je, kuna hatua za usaidizi za kukabiliana na athari za chanjo?

Serikali ya Japani tayari imeweka mfumo wa kutoa usaidizi kwa watu wanaopata athari baada ya kuchanjwa.

Sheria ya utoaji chanjo ya taifa hilo inawajumuisha watu wanaopata chanjo za virusi vya korona, hivyo serikali itagharimia matibabu au kulipia pensheni za ulemavu kwa yeyote atakayekumbwa na athari kali.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Februari 25. Inapatikana kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

182. Swali lingine ni je, athari hutokea? Kumewahi kutokea vifo vyovyote?

Athari zinaweza kutokea kwa aina yoyote ya chanjo na zimeripotiwa pia kwenye chanjo za virusi vya korona. Kwa mujibu wa Kituo cha Udhibiti na Uzuiaji wa Magonjwa cha Marekani, athari zinazoripotiwa zaidi kutokana na chanjo zilizoendelezwa na kampuni ya kutengeneza dawa ya Marekani ya Pfizer na mshirika wake BioNTech ya Ujerumani, pamoja na kampuni ya Marekani ya Moderna, ni maumivu na uvimbe, uwekundu, kuhisi baridi, uchovu na kichwa kuuma. Athari hizi kwa kawaida hutokea ndani ya siku moja au mbili baada ya kuchanjwa na mara nyingi hutoweka katika siku chache. Licha ya kuwa nadra, kumekuwepo na ripoti za dalili za wastani hadi dalili kali zilizokuwa kubwa kiasi cha kutosha kuathiri maisha ya kila siku.

Kwa mujibu wa ripoti juu ya chanjo ya Pfizer na BioNTech, kwa kuzingatia taarifa iliyotolewa na kampuni hizo kwa vyombo vya habari na majaribio ya kitabibu, dalili kubwa zilijumuisha asilimia 3.8 za watu waliokuwa na uchovu na asilimia mbili walioumwa vichwa. Watu wawili waliopatiwa chanjo walifariki miongoni mwa watu 40,000 walioshiriki majaribio ya kitabibu. Lakini wengine wanne waliopewa chanjo bandia pia walifariki, hivyo ripoti hiyo inasema vifo hivyo huenda havihusiani na chanjo.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Februari 24.

181. Je, athari zipi zinazotokana na chanjo iliyoendelezwa na kampuni za kutengeneza dawa za Pfizer na BioNTech?

Kamati ya ushauri ya Marekani inayoshughulikia utoaji chanjo, imeandaa data juu ya athari zilizoripotiwa kutokana na chanjo iliyoendelezwa na kampuni za kutengeneza dawa za Pfizer na BioNTech. Utafiti huo uliohusisha watu takribani 997,000 waliopatiwa chanjo ulionyesha kuwa, baada ya kuchanjwa dozi zao za kwanza, asilimia 67.7 waliripoti kupata maumivu eneo walipochomwa sindano, asilimia 28.6 waliripoti uchovu, asilimia 25.6 kuumwa kichwa, asilimia 17.2 kukumbwa na maumivu ya misuli, asilimia 7.4 waliripoti kupatwa na homa, asilimia 7.1 maumivu ya viungo, asilimia 7.0 kuhisi baridi, wengine asilimia 7.0 waliripoti kuhisi kichefuchefu, na asilimia 6.8 kukumbwa na uvimbe. Athari kali za mzio baada ya chanjo pia zimeripotiwa.

Utafiti wa dozi 9,943,247 za Pfizer na BioNTech zilizotolewa hadi Januari 18, ulibaini visa 50 vya anaphylaxis ambayo ni athari kali ya mzio. Hii inawakilisha kiwango cha 1.0057 cha visa vya anaphylaxis kwa kila dozi 200,000 zilizotolewa. Anaphylaxis ilitokea miongoni mwa watu wenye umri wa kati ya miaka 26 hadi 63, huku umri wa kati ukiwa miaka 38.5.

Wanawake waliwakilisha asilimia 94 ya visa hivyo. Anaphylaxis ilianza ndani ya dakika 15 baada ya uchomaji sindano katika asilimia 74 ya visa hivyo, na ndani ya dakika 30 katika asilimia 90 ya visa. Asilimia 80 ya visa viliripotiwa kwa watu wenye historia ya kuwa na athari za mzio, ikiwemo kwa dawa na chakula.
Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Februari 22.

180. Swali lingine linahusu hali zipi za kiafya tupaswa kuziangalia kabla na baada ya kupata chanjo za virusi vya korona?

Huenda kukawa na visa ambapo watu wanaojihisi wagonjwa wanashauriwa kutopata chanjo. Wizara ya Afya inawasihi wale walio na homa ya nyuzijoto 37.5 za selsiasi ama zaidi, au wanajihisi wagonjwa kuepukana na kupata chanjo. Kwa watu walio na matatizo ya kiafya ama wale wanaotibiwa, wizara inapendekeza watafute ushauri kutoka kwa daktari wakati wa tathmini ya kabla ya chanjo.

Wizara pia inatoa wito kwa wanaopokea chanjo kusalia kwenye eneo la utoaji chanjo kwa dakika zisizopungua 15 baada ya kuchanjwa, ili kuhakikisha hawapati mzio. Wizara hiyo inasema endapo watabaini kitu fulani kisicho cha kawaida, wanapaswa kuwasiliana na daktari. Hakuna shida kuoga baada ya chanjo, lakini unapooga, unapaswa kuwa mwangalifu kutosugua sehemu uliopigwa sindano. Unapaswa kujizuia kufanya mazoezi yanayokuhitaji kutumia nguvu nyingi siku uliopewa chanjo. Nakayama Tetsuo ni Profesa katika Chuo Kikuu cha Kitasato aliyebobea katika maswala ya chanjo. Anasema hakuna shida kuoga au hata kunywa pombe ikiwa ni kiasi tu, ingawa unywaji pombe wa kiwango kikubwa, hakika, haupendekezwi kabisa.

Lakini tunapaswa kutilia maanani kuwa tunaweza kuhisi kizunguzungu ama kupumua kwa kasi isiyokuwa ya kawaida, kutokana na hofu ya chanjo. Hali hii inaweza ikawafanya watu wengine wanaopata chanjo kuwa na hofu, ikiwa itatokea eneo panapotolewa chanjo kwa kundi. Okabe Nobuhiko ni Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Afya ya Umma ya Mji wa Kawasaki, ambaye pia ni mjumbe wa jopo la serikali la virusi vya korona. Anasema ni muhimu kuweka mfumo wa kutoa ushauri kwa watu waliohofu kuhusiana na chanjo hiyo.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Februari 19. Inaweza pia ikapatikana kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

179. Je, chanjo inalenga kutukinga sisi dhidi ya virusi ama kuwakinga watu walioambukizwa virusi kutoumwa sana?

Inadhaniwa kuwa chanjo za virusi vipya vya korona zinasaidia kuwakinga wagonjwa kupata dalili ama kuumwa sana kuliko kutukinga sisi dhidi ya virusi. Wataalam wanasema kwa jumla, chanjo zinatarajiwa kusaidia kuzuia maambukizi, kuwazuia wagonjwa kupata dalili ama kuumwa sana, na kupata kile kinachoitwa kingamaradhi ya kundi. Ni vigumu kuthibitisha ikiwa chanjo fulani ni fanisi katika kuzuia maambukizi. Hii ni kwa sababu watu wengi wanaoambukizwa wanakosa kuonyesha dalili. Pia inahitaji tathmini ya kina ya seli ili kubaini virusi vimeingia kwenye mwili wa binadamu.

Shirika la Dawa na Vifaa Tiba ama PMDA, hutathmini dawa nchini Japani. Linasema inapokuja kwa swala la kutathmini chanjo za virusi vipya vya korona, tafiti za kitabibu zinahitajika, kimsingi, kutathmini ufanisi wa chanjo katika kuzuia watu walioambukizwa virusi dhidi ya kupata dalili. Majaribio ya kitabibu nchini Marekani na Ulaya yameashiria si tu ufanisi wa chanjo katika kuzuia wagonjwa kupata dalili, lakini pia ni kwa namna gani zinafanikiwa kuzuia kupata dalili kali. PMDA pia inajumuisha ufanisi wa kuzuia wagonjwa kuumwa sana katika vigezo vyake vilivyotumiwa kutathmini chanjo za virusi vya korona.

Kupata kingamaradhi ya kundi pia ni moja ya matarajio ya matokeo ya utoaji chanjo ya virusi vya korona. Shirika la Afya Duniani, WHO linakadiria kuwa ili dunia kufikia kingamaradhi ya kundi, zaidi ya asilimia 70 ya watu wake watahitaji kuchanjwa. WHO inasema kutokana na hali hii, inaonekana kuwa vigumu kuifikia kingamaradhi hiyo kufikia mwisho wa mwaka huu.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Februari 18.

172. Kwa nini chanjo ni muhimu?

Chanjo inalenga kuwapa watu kingamaradhi ama kuimarisha mifumo yao ya kinga. Inatarajiwa kuzuia watu kupata dalili kali ama kuugua sana. Mbali na hilo, pia inatarajiwa kudhibiti ueneaji wa ugonjwa huo katika jamii.
Wizara ya Afya ya Japani inasema matokeo ya majaribio ya kitabibu yaliyofanyika nje ya nchi, yameonyesha kuwa chanjo za virusi vipya vya korona, zinafaa katika kuzuia hali na dalili mbaya kama vile homa.
Ikiwa utoaji chanjo kwa watu wengi unaweza kusaidia kupunguza idadi ya wagonjwa wanaougua sana, na vifo vinavyotokana na ugonjwa huo, mzigo kwa mfumo wa huduma ya afya utapungua.
Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Februari 2. Inaweza kupatikana katika tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

171. Utoaji chanjo kwa raia wa kigeni wanaoishi nchini Japani.

Raia wa kigeni wanaoishi nchini Japani wanaweza kupata chanjo ya virusi vya korona katika manispaa walikojiandikisha kama wakazi.

Mpango wa utoaji chanjo nchini Japani umepangwa kuanza Februari 17. Chanjo hizo zitatolewa kwanza kwa wafanyakazi wa tiba, na kwa taratibu wanaopewa kuongezwa kwa kuwachanja wazee, wakifuatwa na watu walio na matatizo ya kiafya na wengineo.

Utoaji chanjo kwa wazee unatarajiwa kuanza wakati fulani mwezi Aprili.

Kuhusu mahali pa kupata chanjo, maeneo ya utoaji chanjo kimsingi, yatawekwa katika manispaa walikojisajili watu kama wakazi.

Serikali inapanga kutuma kuponi zinazohitajika kwa watu kupokea chanjo, wakiwa katika makazi yao. Chanjo hizo zinatolewa bila malipo.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Februari 15.

166. Je, ni sawa kupewa chanjo tofauti katika awamu ya kwanza na ya pili ya utoaji chanjo?

Mkurugenzi wa Idara ya Kingamaradhi, Chanjo na Biolojia ya Shirika la Afya Duniani, WHO Kate O’Brien, alitoa maoni yafuatayo kwenye mkutano wake na wanahabari kwa njia ya mtandao uliofanyika Januari 7.

Alisema chanjo zaidi ya moja tayari zinatumika kwenye baadhi ya nchi. Alikiri kuwa WHO haina data juu ya kuchanganya na kufananisha chanjo za aina tofauti. Lakini alisema iwapo mtu amechanjwa dozi ya kwanza kwa kutumia chanjo ya Pfizer, atapaswa kuchanjwa chanjo ya pili kwa kutumia aina hiyo hiyo. Alisema WHO inafahamu kuwa katika baadhi ya nchi, aina tofauti za chanjo zimekuwa zikitumika kwa dozi ya kwanza na ya pili. Alisema suala hili ni eneo muhimu sana la utafiti na WHO itatoa kipaumbele kwa utafiti wa aina hii ili kutoa maoni yake.

Swali lingine linahusu utoaji chanjo ya virusi vya korona ya Pfizer kwa watoto wenye umri wa miaka 15 kurudi chini.

Mkrugenzi wa Idara ya Kingamaradhi ya WHO, Kate O’Brien, alitoa maoni yafuatayo kwenye mkutano wake na wanahabari kwa njia ya mtandao uliofanyika Januari 7.

Alisema kamati kwa ujumla haipendekezi watoto wa umri chini ya miaka 16 kupatiwa chanjo hizo kwa sababu WHO haina data.
Alisema majaribio ya kitabibu hadi sasa hayawahusishi watu wenye umri chini ya miaka 16, lakini utafiti unaendelea kuangazia ufanisi wa chanjo kwa watoto wenye umri kati ya miaka 12 na 16, hivyo taarifa zaidi zitakuja siku zijazo.

Lakini pia alisema watu wanaosimamia chanjo wanaweza kuchagua kuwachanja watoto wenye matatizo ya kiafya ya muda mrefu au hatari ya kupatwa na madhara makubwa ya virusi vya korona baada ya kuwasiliana na wanafamilia wao. Hata hivyo alisisitiza kuwa kwa ujumla, hawapendekezi watoto wa umri wa chini ya miaka 16 kuchanjwa.

Taarifa hii ni sahihi hadi Januari 27. Pia inapatikana kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

164. Watu walioambukizwa virusi vya korona na kupona wanapaswa pia kupata chanjo?

Hiki ndicho alichokisema Mwenyekiti wa Jopo la Wataalam Wanaotoa Ushauri kuhusu Kingamaradhi katika Shirika la Afya Duniani - WHO, Alejandro Cravioto, wakati wa mkutano na wanahabari uliofanyika kwa njia ya mtandao Januari 7 mwaka huu.

Alisema hilo lilikuwa miongoni mwa mapendekezo makuu ya WHO, kwa kuwa inaona kwamba watu walioambukizwa virusi vya korona na kuthibitishwa kwa kipimo cha PCR au kipimo cha Antijeni, hawapaswi kutengwa katika utolewaji wa chanjo hiyo.

Cravioto alibainisha kuwa, bado wataalam hao hawafahamu kingamwili ya asili inayopatikana baada ya mtu kuambukizwa virusi vya korona, inayoweza kumkinga dhidi ya maambukizi mapya, inadumu mwilini kwa muda gani. Alisema, chapisho moja lililotolewa Januari 6 mwaka huu linaripoti kuwa, watu walioambukizwa na kupona ugonjwa huo wanakuwa na kinga asili kwa hadi miezi minane, lakini takwimu za utafiti huo hazitoshelezi kuwafanya watu wa aina hiyo kutopata chanjo.

Aliongeza kusema kuwa, kwa upande mwingine, ikiwa mtu aliyeambukizwa virusi hivyo atapenda kusubiri kidogo ili kutoa fursa kwa watu walio kwenye hatari kubwa zaidi ya kuambukizwa kupata chanjo kwanza, huo utakuwa uamuzi wa hiari wa mtu.

Mkurugenzi wa Idara ya Kingamaradhi, Chanjo na Biolojia wa WHO Kate O’Brien alitoa pia maoni yake wakati wa mkutano huo na wanahabari.

Alisema dunia kwa sasa ipo katika hatua za awali za chanjo hiyo, na kila nchi inajitahidi kulipa suala hilo kipaumbele cha juu. Kuna uwezekano mdogo sana kwa mtu aliyeambukizwa virusi hivyo na kupona, kuambukizwa tena katika kipindi cha miezi sita. Lakini O’Brien aliongeza kuwa, Shirika la Afya Duniani halishauri kutowapa au kuchelewesha utoaji chanjo kwa watu wa aina hiyo.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Januari 21. Inaweza kupatikana kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

157. Nini sababu za ongezeko la hivi karibuni la visa vipya vya virusi vya korona nchini Japani?

Profesa Oshitani Hitoshi wa Chuo Kikuu cha Tohoku ni mmoja wa wanajopo wataalamu wanaoishauri serikali ya Japani. Aliwaambia wanahabari Januari 8 kwamba ongezeko la hivi karibuni la idadi ya visa vipya si la kawaida kabisa na kuwa wataalamu wanahitaji kutathmini data kwa kina ili kufahamu kilichosababisha ongezeko hilo.

Oshitani alisema takwimu za hivi karibuni za maambukizi kama vile ongezeko la ghafla la idadi ya visa vipya jijini Tokyo Disemba 31 mwaka jana si la kawaida kwa mtazamo wa elimu ya magonjwa ya mlipuko.

Alisema si kawaida kabisa kwa visa vya kila siku Tokyo vilivyokuwa chini ya 1,000 mwishoni mwa mwezi Disemba, kuongezeka kwa karibu siku kumi hadi zaidi ya visa 2,000.

Maambukizi mapya yanayowahusisha vijana kati ya umri wa miaka 18 na 39 yanaongezeka siyo tu Tokyo pekee bali pia Osaka. Oshitani alisema kwa kiasi fulani, hii ni kwa sababu watu wengi walifanya matembezi wakati wa sikukuu za mwisho wa mwaka na mwaka mpya.

Aliongeza kwamba matokeo ya vipimo vilivyofanywa wakati wa sikukuu hizo pengine yalitolewa kwa mkupuo baada ya likizo hizo. Profesa huyo ameashiria uwepo wa sababu nyingine. Alisema vijana waliokuwa wakisita kupimwa, walienda kupimwa baada ya ripoti za kifo cha mbunge mwishoni mwa mwaka na vifo vingi vya watu waliokuwa kwenye karantini nyumbani.

Aidha Oshitani alifikia hitimisho kwamba wataalamu wanapaswa kuchunguza chanzo cha ongezeko hilo na kutathmini sababu zinazolichangia.

Swali lingine ni je, “Tufanyeje kuhusu chanjo na uchunguzi wa afya wa kawaida wakati bado kukiwa na hali ya dharura?”

Wizara ya Afya ya Japani inaonya katika tovuti yake na kwingineko kwamba ikiwa watu watajizuia mno kwenda katika taasisi za tiba, hilo linaweza kuongeza hatari za kiafya. Hususan, kushindwa kuwapeleka watoto wachanga na wadogo kuchanjwa katika umri unaotakiwa kunaweza kuwasababishia hatari kubwa za kupata magonjwa hatari ya kuambikizwa.

Pia, wizara hiyo inawataka wazazi kuhakikisha watoto wao wanafanyiwa uchunguzi wa afya wa mara kwa mara kwani hutoa fursa nzuri ya kupata ushauri wa kitaalamu kuhusu ukuaji wa watoto wao. Kadhalika, wizara hiyo inashauri watu wafanye vipimo vya saratani mara kwa mara kwa kuwa saratani inaweza isionyeshe dalili katika hatua ya mapema.

Wizara hiyo ya afya inasema hatua madhubuti za kukabiliana na maambukizi za utakasaji na uzungushaji wa hewa safi zinatekelezwa katika taasisi za tiba na maeneo ya uchunguzi wa afya. Kwa hivyo, inashauri watu kutafuta usaidizi stahiki wa tiba licha ya janga linaloendelea kwa kuwasiliana na madaktari wanaozuru nyumbani na wataalamu wengine, badala ya kujizuia kutumia huduma hiyo kwa uamuzi wao.

Taarifa hii ni sahihi kufikia Januari 14 na inapatikana katika tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

155. Hali ya dharura nchini Japani.

Jopo la wataalam linaloishauri serikali ya Japani juu ya namna ya kukabiliana na virusi vya korona, liliandaa mapendekezo ya dharura mnamo Januari 5. Yalisisitiza umuhimu wa kupunguza hatari ya maambukizi kwenye baa na migahawa.

Msingi wa pendekezo la jopo hilo ulikuwa ripoti iliyochapishwa na timu ya wanasayansi wa Chuo Kikuu cha Stanford na vinginevyo kwenye jarida la sayansi la Nature mwezi Novemba mwaka jana.

Kwa kutumia modeli ya kihisabati, timu hiyo ilitathmini data za simu za mkononi zilizokusanywa kutoka kwa watu takribani milioni 98 kwenye majiji makubwa ya Marekani kuanzia mwezi Machi hadi Mei mwaka jana. Lengo lilikuwa kuchunguza maeneo yenye uwezekano wa virusi kuenea.

Timu hiyo ilichunguza maduka yaliyo katika hatari kubwa pale yatakapofunguliwa tena baada ya kufungwa kwa muda. Ilibaini kuwa hatari ilikuwa juu kwenye migahawa inayotoa huduma zote. Ilifuatwa na kumbi za mazoezi, migahawa na hoteli.

Timu hiyo ilisema, ikilinganishwa na maeneo mengine, hatari ni kubwa zaidi kwenye migahawa kwa sababu inapokea wateja wengi, ambao huenda wakakaa hapo kwa muda mrefu.

Kwenye ripoti hiyo, watafiti pia walishauri namna migahawa inaweza kuboresha mazingira yao ili kuzuia ueneaji wa virusi pale itakapofunguliwa tena. Wataalam hao walisema migahawa na maduka mengine itaweza kupunguza idadi ya maambukizi kwa asilimia 80 kwa kupunguza idadi ya wateja wanaoruhusiwa kwa wakati mmoja hadi asilimia 20 ya uwezo wao.

Timu hiyo ilibainisha kwamba ni vizuri zaidi, kupunguza idadi ya watu kwenye maduka badala ya kuweka vizuizi sawia kwa matembezi yao.

Jopo la serikali limesema kwa kuzingatia ripoti pamoja na tathmini nyinginezo za maambukizi ya makundi yaliyotokea nchini Japani, lilihitimisha kwamba baa na migahawa ni maeneo muhimu yanayopaswa kuangaziwa na serikali katika hatua za mapambano dhidi ya virusi.

Hiyo haimaanishi kuachwa kwa maeneo mengine katika hatua hizo. Hatari ya maambukizi inaaminika kuongezeka mahali popote watu wanapokutana na kula. Wanapokula, walaji hulazimika kuondoa barakoa zao na uwezekano wa kuzungumza ni mkubwa zaidi. Pale pombe inapouzwa, wanaweza kuzungumza kwa sauti kubwa ama kuzembea katika kuchukua hatua za kujilinda dhidi ya maambukizi ya virusi.

Hivyo, kuhusu virusi vya korona, ni muhimu sana kupunguza hatari ya kuenea virusi hivyo kwenye baa, migahawa na kwingineko ambako watu wanapata milo kwa pamoja.

Taarifa hii inaweza kuthibitishwa kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

152. Hali ya dharura inamaanisha nini nchini Japani?

Tangazo la hali ya dharura ni hatua inayochukuliwa kwa mujibu wa sheria maalum ili kukabiliana na virusi vya korona. Waziri Mkuu anaweza kutoa tangazo hilo ikiwa virusi vitaenea kwa kasi kote nchini na vinaweza kuathiri pakubwa maisha ya watu au uchumi. Muda na maeneo patakapotekelezwa hatua hiyo yatatengwa.

Magavana wa mikoa wa maeneo yaliyotengwa wanaweza wakawaomba raia kujizuia kwenda matembezini na kushirikiana ili kuzuia maambukizi kuenea. Hii haijumuishi hali zinazohitajika ili kuendeleza maisha ya watu.

Magavana wanaweza wakaomba au kuelekeza kufungwa kwa shule au kuweka ukomo wa matumizi ya majengo kama vile maduka makubwa ya uuzaji bidhaa wanakokusanyika watu wengi. Wanaweza pia kuwa na mamlaka ya kutumia ardhi na majengo kama vituo vya muda vya tiba bila idhini ya wamiliki wake, ikiwa hatua kama hizo hasa zinahitajika.

Katika hali za dharura, wanaweza kuomba au kuelekeza kampuni za uchukuzi kuwasilisha bidhaa na vifaa tiba au kutaifisha bidhaa tiba panapokuwepo na haja ya kufanya hivyo.

Mwezi Aprili mwaka jana, aliyekuwa Waziri Mkuu wa Japani Abe Shinzo alitangaza hali ya dharura katika mikoa 7 ambayo ni Tokyo, Kanagawa, Saitama, Chiba, Osaka, Hyogo na Fukuoka. Kisha hali hiyo ilitekelezwa kote nchini humo. Swali ni je, “Ni kwa namna gani hali ya dharura ya kwanza ilifanikiwa?”

Wakati wa kipindi hicho, serikali iliwarai watu kupunguza kukutana ana kwa ana kwa asilimia zisizopungua 70, na kwa asilimia 80 ikiwezekana, kutokana na ushauri uliotolewa na jopo la wataalam la serikali.

Katika maeneo yaliyokuwa na maambukizi mengi, watu walitakiwa kufanyia kazi nyumbani kadiri iwezekanavyo na walisihiwa mno kujizuia kuondoka nyumbani isipokuwa wanapoenda kununua chakula au kutembelea madaktari.

Hii ilisababisha baa, migahawa, kumbi za tamthilia, kumbi za sinema, maduka makubwa ya uuzaji bidhaa, hoteli, makumbusho na maktaba kufungwa kwa muda, na pia kufutwa na kuahirishwa kwa matukio mbalimbali. Shule kote nchini Japani zilikuwa zimefungwa tangu mwezi Machi na nyingi ya shule hizo ziliendelea kufungwa baada ya kutolewa kwa tangazo hilo.

Kutokana na hatua hizo, idadi ya wageni katikati ya jiji la Tokyo ilipunguzwa kwa zaidi ya asilimia 60 wakati wa siku za wiki na karibu asilimia 80 wakati wa wikendi ikilinganishwa na mwezi Januari mwaka huo.

Idadi ya visa vipya nchini Japani ilifikia kilele cha karibu visa 700 katikati ya mwezi Aprili na kuanza kupungua. Maeneo kulikotekelezwa hali ya dharura yalipunguzwa taratibu. Hali hiyo hatimaye iliondolewa mikoani Hokkaido na Tokyo na mikoa mitatu jirani Mei 25. Visa vipya 21 vilithibitishwa siku hiyo.

Taarifa hii inaweza kuthibitishwa kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

151. Je, watoto wanapaswa kuepuka kwenda nje ya nyumba ama kucheza na marafiki zao?

Wataalamu wanasema hakuna haja ya kuwazuia watoto kwenda nje ya nyumba na kucheza na marafiki zao ilimradi wachukue hatua za kujilinda dhidi ya maambukizi. Kucheza ni muhimu sana kwa ukuaji wa kiakili na kimwili wa mtoto. Kwa hivyo, iwapo hatua za kupunguza maambukizi zitafuatwa ipasavyo, ni sawa kwao kwenda nje na kucheza na marafiki zao.

Unapopanga safari wakati shule zinapofungwa, kumbuka kufuatilia hali ya maambukizi kwenye manispaa yako na eneo unalotaka kutembelea. Pia, hakikisha mamlaka za maeneo yote hazijawaomba watu kujizuia kusafiri.

Kuchezea nje kunaaminika kusababisha hatari ndogo ya maambukizi kulinganisha na kuchezea ndani ya nyumba. Lakini unapaswa kuwa makini kuhusu masuala yafuatayo.

-Watoto wanapaswa kujizuia kuchezea nje ya nyumba wanapokuwa na dalili kama za mafua kama vile mwasho wa koo, kikohozi au homa.
-Watoto wanapaswa kunawa mikono baada ya kushika vitu vinavyoshikwa na watu wengi mara kwa mara.
-Watoto pia wanapaswa kunawa mikono kabla ya kula au kunywa.
- Watoto wanapaswa kuepuka kutazamana wanapokula.

Kuchezea ndani ya nyumba kunasababisha hatari kubwa, kwa hivyo, hatua zifuatazo zinapaswa kufuatwa.
-Hakikisha hakuna mtu aliye karibu ambaye ni dhahiri kuwa ameambukizwa.
-Hakikisha hakuna wazee au watu wenye matatizo ya kiafya walio karibu.
-Hakikisha watoto na pia familia zao, hawana dalili kama za mafua.
-Wacheze tu wakiwa kwenye kundi ndogo.
-Hakikisha watoto wanacheza baada ya kuruhusiwa na wazazi wao.
-Watoto wanapaswa kunawa mikono baada ya kushika vitu vinavyoshikwa mara kwa mara na watu wengi.
-Watoto wanapaswa pia kunawa mikono kabla ya kula au kunywa.
-Watoto wanapaswa kuepuka kutazamana wanapokula.
-Hakikisha unaruhusu hewa kuingia katika eneo husika walau mara moja kila baada ya saa moja.

150. Je, wazazi wanapaswa kuwazuia watoto nyumbani kwao badala ya kuwaacha waende shuleni au vituo vya kulelea watoto?

Wataalam wanasema hakuna mantiki kwa mzazi kuamua kwa hiari kumruhusu mwanawe aende shuleni au vituo vya malezi ya watoto labda pale mtoto atakapokuwa hajihisi vema au amekutana kwa karibu na mtu aliye na maambukizi ya virusi vya korona.

Katika maeneo ambayo hayajashuhudiwa milipuko mikubwa ya maambukizi, wengi wa watoto walioambukizwa, walipata virusi kutoka kwa watu wazima wanaoishi nao kwenye nyumba moja, mathalani wazazi. Lakini visa vya usambazaji virusi kwenye maeneo ambako watoto wanakutana kwa pamoja pia vimekuwa vikiripotiwa. Hivyo, shule na vituo vya malezi ya watoto, zinaweza kufungwa kwa muda fulani iwapo mtoto hapo atathibitika kuambukizwa virusi.

Hatua tofauti zitahitajika kwa kuzingatia mazingira ya mlipuko, hivyo tafadhali fuatilia maelekezo kutoka kwa serikali ya manispaa unapoishi. Iwapo mtu ataambukizwa kwenye kaya, mtoto au watoto wa kaya husika watachukuliwa kama waliokuwa karibu na mgonjwa mwenye virusi. Hivyo, wanalazimika kusalia nyumbani. Pia, wizara ya afya ya Japani inapendekeza kwamba watoto wajiepushe kuhudhuria shuleni au vituo vya malezi ya watoto pale wanapokuwa na homa ya kiwango kidogo ama dalili za magonjwa mengine ya mafua. Ni muhimu kwamba kila mmoja afuate ushauri huo.

Imefahamika kuwa watoto wenye virusi vya korona wenye umri chini ya miaka mitano ambao wanaonyesha dalili wanatoa kiwango kikubwa cha virusi. Pia inafahamika kuwa watoto wengi walioambukizwa husalia kutoonesha dalili na kwamba virusi huendelea kutolewa kwa njia ya kinyesi kwa kipindi kirefu. Watu wazima wanaotumia muda wao mwingi wakiwa karibu na watoto, wanapaswa kuchukua hatua madhubuti kama vile kunawa mara kwa mara mikono yao na kuvaa barakoa.

149. Je, wazazi wanapaswa kufanya nini kwa watoto wasioweza kuvaa barakoa?

Wataalam wanasema huku uvaaji wa barakoa ukiwa na tija kwa muktadha wa kujilinda dhidi ya hatari ya moja kwa moja ya matone ya wagonjwa wenye maambukizi kwa njia ya kukohoa au kupiga chafya, ni jambo lisilo na uhalisia kwa mtoto wa miaka chini ya miwili kuzivaa.

Kwa upande wa watoto wenye umri wa miaka minne hadi mitano, licha ya kwamba inategemeana na mtu binafsi, inawezekana kwa kundi la watoto wa umri huu kuvaa barakoa wakiwa makwao. Wazazi wanapaswa kuwafundisha namna ya kuvaa na kuvua.

Wataalam wanasema watoto wengi wameambukizwa virusi vya korona kutoka kwa wazazi wao nyumbani. Ili kuepusha watoto kuambukizwa, ni muhimu kwa wazazi kuchukua hatua za kuzuia maambukizi ili wao wenyewe wasiweze kuambukizwa virusi. Iwapo mwanafamilia ataambukizwa, ni muhimu sana kujitenga kwa umbali wa zaidi ya mita mbili kutoka kwa mtu aliyeambukizwa.

Wataalam wanasisitiza kunawa mikono na kutumia vitakasa pia ni muhimu, kwani watoto wanaweza kuambukizwa kwa kugusa midomo, pua, macho baada ya kugusa wanasesere na vitabu vilivyo na virusi.

148. Kina mama wanapaswa kuacha kuwanyonyesha watoto pale wanapobaini kuambukizwa?

Wataalam wanasema mama hapaswi kuacha kunyonyesha kabisa hata kama atagundulika kuwa na maambukizi. Wanasema anaweza kuchagua iwapo aendelee kumnyonyesha mtoto wake kutegemea na hali zake na anavyopendelea.

Pale mama anapokuwa ameambukizwa, kuna hatari kwamba anaweza kumwambukiza virusi mtoto wake kupitia kugusana ama kukohoa. Kuna ripoti kwamba vinasaba vya virusi vya korona vilibainiwa kwenye maziwa ya mama. Lakini bado haipo wazi ikiwa maziwa hayo yana virusi vinavyoambukiza. Maziwa ya mama yana faida nyingi kwa watoto na haishauriwi kuacha kuwanyonyesha kwa hofu ya maambukizi.
Kuna mbinu mbili za mama aliyeambukizwa kuendelea kunyonyesha. Moja ni kunyonyesha moja kwa moja na nyingine ni kutumia chupa ya kunyonyeshea maziwa ya mama.

Kabla ya kumnyonyesha mtoto moja kwa moja, mama anapaswa kunawa mikono yake vizuri, kuitakasa na kuvaa barakoa.

Mama anapaswa pia kuhakikisha ananawa mikono yake na kutakasa mikono, matiti na pampu ya kukamulia maziwa kabla ya kukamua maziwa yake. Mtu ambaye hajaambukizwa anapswa kuweka maziwa kwenye chupa na kumnyonyesha mtoto.

147. Je, tuahirishe kulazwa kwa watoto hospitalini kwa ajili ya vipimo ama upasuaji wa magonjwa mbali na virusi vya korona?

Wataalam wanasema unapaswa kuweka kipaumbele kwenye vipimo na matibabu ya ugonjwa wa watoto, na kuwa makini na hali za afya za watoto kabla ya kulazwa hospitalini.
Hospitali nchini Japani zinashughulika na wagonjwa wa virusi vya korona na watu wenye magonjwa mengine kwa kuwatenganisha. Utakapothibitisha hili kwenye hospitali ambayo mtoto wako anatarajia kulazwa, kimsingi unaweza kuhakikishiwa tena kuwa mtoto wako atakuwa salama kwenye hospitali hiyo.

Maambukizi ya virusi vya korona yanatarajiwa kuendelea, hivyo unapaswa kuweka kipaumbele tiba na vipimo vya ugonjwa wa mtoto wako.

Ikiwa tarehe ya mtoto kwenda hospitalini tayari imeshapangwa, unapaswa kuwa mwangalifu hasa na hali ya afya ya mtoto wiki mbili kabla ya kwenda hospitalini na epuka tabia ambazo zitaongeza hatari ya maambukizi. Vikwazo vinaweza kuwekwa kwa watoto kulazwa hospitalini ikiwa hali zao si nzuri ama wamekutana na watu wanaoonyesha dalili za homa ya mafua.

146. Je, watoto wanapaswa kulazwa hospitalini iwapo wataambukizwa virusi vya korona? Na je, wazazi wanapaswa kuruhusiwa kuwatembelea ama kukaa na watoto wao wanapokuwa wamelazwa hospitalini?

Majibu ya wataalam ni kwa mujibu wa hali ilivyo nchini Japani. Wataalam wanasema watoto wanapoambukizwa virusi vya korona, visa vingi huhusisha dalili zisizokuwa kali na havihitaji mtoto kulazwa hospitalini kwa mtazamo wa kitabibu. Hata hivyo, kuna hali zinazohitaji watoto kulazwa hospitalini kwa mujibu wa sheria.

Iwapo mtoto ataambukizwa virusi kutoka kwa wazazi wake akiwa nyumbani, wazazi na watoto wanaweza kulazwa hospitalini kwa wakati mmoja. Iwapo mzazi hajaambukizwa virusi hivyo, watoto wanaweza kulazwa peke yao kwa ajili ya karantini.

Kuhusiana na kuwaruhusu wazazi kuwahudumia watoto wao wakiwa wamelazwa hospitalini, hii itabainishwa kwa msingi wa kisa kimoja hadi kingine kwa kuzingatia vigezo kama umri wa mtoto na hali ilivyo hospitalini.

Iwapo itashauriwa mtoto asalie nyumbani ama kwenye kituo kilichotengwa wakati akipata nafuu, wazazi watalazimika kuwasiliana na kituo cha afya cha umma na kuendelea na uchunguzi wa afya kwa kutumia simu hata baada ya mtoto kupona.

Vigezo vya dalili zisizokuwa kali ni sharti viamuliwe na mtaalam wa tiba. Vinajumuisha mtu kuwa na nguvu, kuwa na maji ya kutosha, na kupumua bila tatizo lolote.

Iwapo mtoto atahisi kuumwa na kuhitaji kulazwa hospitalini, kutakuwa na uwezekano mkubwa kuwa wazazi wameambukizwa virusi hivyo ama watatengwa kwa kuwa katika hali inayoweza kufanya waambukizwe virusi. Katika hali kama hizo, inawezekana mzazi asiruhusiwe kufika hospitalini au kukutana na mtoto wake.

Wataalam wanawashauri wazazi kuwasiliana na daktari juu ya namna ya kuchukua hatua, kwani yaweza kutofautiana kulingana na vigezo mbalimbali vikiwemo; hali mahususi ya mzazi kama vile iwapo tayari wamepona kutokana na virusi hivyo, hali hospitalini, na hali ya eneo husika na kadhalika.

145. Uchunguzi wa afya wa mara kwa mara pamoja na chanjo kwa watoto wachanga unapaswa kucheleweshwa?

Wataalam wanasema kuwa, uchunguzi wa afya wa mara kwa mara kwa watoto wachanga nchini Japani unalenga kubaini mapema magonjwa na matatizo mengine yanayowapata watoto wa umri fulani. Hii ni kuhakikisha kuwa watoto wanaanza kupatiwa matibabu wanayohitaji mapema iwezekanavyo.

Hali kadhalika, ni muhimu sana kuwapa watoto chanjo ili kuwakinga kabla hawajaambukizwa magonjwa ya kuambukiza. Ni muhimu kuzingatia kanuni na njia za kuwakinga dhidi ya virusi vya korona. Lakini wataalam wanasema kuwa, ikiwa tutajiepusha kuwapeleka watoto hospitalini, hilo litawaweka kwenye hatari ya kuambukizwa magonjwa mengine hatari yanayozuilika, hivyo basi, hilo halipaswi kutokea.

Wataalam hao wanabainisha kuwa, tutaendelea kushuhudia ongezeko la visa vipya kila baada ya miezi michache. Iwapo wazazi watajiepusha kuwapeleka watoto wao hospitalini kwa uchunguzi na chanjo kila hali hiyo inapotokea, hilo litakuwa ni tatizo kubwa.

Wizara ya Afya ya Japani imesema kuwa, baadhi ya manispaa nchini humo zimebadili namna zinavyotoa huduma ya uchunguzi wa afya wa mara kwa mara kutokana na hali ya maambukizi ya virusi vya korona kwenye maeneo yao.

Baadhi ya visa vimeripotiwa pia ambapo chanjo hutolewa kwa muda mrefu zaidi ya muda uliopangwa awali ili kuwawezesha watoto walioikosa katika muda wa kawaida. Wataalam hao wanatoa wito kwa wazazi kuwasiliana na ofisi ya afya ya umama ya eneo lao ili kupata taarifa.

Lakini, iwe ni kwa makundi au mmoja mmoja, watoto na walezi wao wanapaswa kufuata kanuni za kuzuia ueneaji wa maambukizi ya virusi vya korona wanapokwenda hospitalini au kituo cha afya kufanyiwa uchunguzi wa mara kwa mara au kupatiwa chanjo.

Wanapaswa kuhakikisha kuwa hawana homa au dalili zingine kama vile kukohoa, kabla hawajaondoka nyumbani. Kunawa mikono kwa maji yanayotiririka na sabuni pamoja na kuvaa barakoa ni sharti kwa wakubwa wanaoambatana na watoto. Pia, ni muhimu kuepuka kadiri iwezekavyo kuwapeleka ndugu wengine wa watoto hao pamoja na babu zao kwenye eneo hilo.

Watafiti tayari wameripoti kuwa virusi vya korona vinaweza kuishi pia kwenye kinyesi cha mgonjwa. Kwa hiyo, tafadhali usiwabadilishe watoto nepi mahali wanapofanyiwa uchunguzi wa afya au chanjo pamoja na kwenye maeneo mengine ya hospitalini.

143. Tunapaswa kuwapeleka watoto kwa daktari mara tu tunaposhuku kuwa dalili walizonazo huenda zimesababishwa na maambukizi ya virusi vya korona?

Wataalam wanasema kuwa, idadi ya watoto waliombukizwa virusi vya korona nchini Japani imekuwa ikiongezeka. Wanasema kuwa, katika visa vingi, watoto hao waliambukizwa virusi hivyo wakiwa nyumbani kutoka kwa walezi wao, au nje wakati walipokuwa wakishiriki shughuli za makundi.

Wataalam wanatoa ushauri kwa walezi kutoa taarifa katika kituo cha afya cha umma kwanza wakati watoto wanapoonyesha dalili au kuwa na historia ya kukutana kwa karibu na mtu aliyeambukizwa virusi hivyo.

Wanashauri pia kutowapeleka zahanati au kwenye huduma ya dharura watoto wanaohisiwa kuambukizwa virusi vya korona kwa sababu huenda wakashindwa kupata vipimo kwenye maeneo hayo kuthibitisha iwapo wameambukizwa virusi.

Ni kwa namna gani na wapi mtu anaweza kupata vipimo vya PCR kuthibitisha maambukizi ya virusi vya korona, hutofautiana kulingana na eneo watu wanapoishi, kwa hiyo, watu wanashauriwa kuzingatia zaidi taarifa zinazotolewa na vituo vya afya vya umma vya maeneo yao.

Wakati watoto wanapokuwa na homa kwa siku kadhaa bila sababu iliyobainishwa, wakawa wanapumua kwa taabu na kushindwa kula au kunywa, au kuwa wachovu, kuna uwezekano mkubwa kuwa wanaugua aina fulani ya ugonjwa kama sio ugonjwa wa COVID-19. Wataalam wanatoa wito kwa walezi kutoa taarifa kwa wataalam wa afya mara tu waonapo hali kama hiyo.

142. Je, ni mambo gani hasa tunayopaswa kuzingatia wakati watoto wanapokuwa na ugonjwa wa pumu au matatizo mengine ya kiafya?

Wataalam wanasema kuwa, kwa ujumla, watoto wanapokuwa na matatizo mengine ya kiafya, wanaweza kuzidiwa na kuwa katika hali mbaya sana wanapoambukizwa magonjwa yanayoathiri mfumo wa upumuaji yanayosababishwa na virusi. Lakini, inafahamika pia kuwa asilimia ndogo ya walioambukizwa virusi vya korona wanaugua ugonjwa wa pumu.

Hatari itokanayo na kuwa na ugonjwa au matatizo mengine ya kiafya, na namna ya kushughulika nayo hubadilika kutegemeana na aina ya ugonjwa, kwa hiyo watu wanashauriwa kupata ushauri wa madaktari wao. Ni muhimu pia kwa wanafamilia na wale wanaoishi na watoto wenye matatizo mengine ya kiafya kuwa waangalifu na kuzingatia njia za kujikinga wasiambukizwe virusi vya korona.

140. Unawezaje kuzuia watoto wako kuambukizwa virusi vipya vya korona?

Tuliwauliza wataalam katika Chama cha Madaktari wa Watoto Nchini Japani na Kituo cha Kitaifa cha Afya na Maendeleo ya Watoto kuhusiana na dalili ambazo watoto huenda wakaonyesha wakiambukizwa virusi hivyo.

Wataalam hao wanasema wamegundua kuwa watoto wanakabiliwa na hatari ya kuambukizwa virusi hivyo sawa tu na watu wazima, ingawa visa vyao vilikuwa vichache kuliko vile vya watu wazima kufikia Agosti 1.

Watoto wengi nchini Japani wameambukizwa virusi hivyo wakiwa nyumbani kwao. Walipatwa na homa na vikohozi vikavu. Lakini ikilinganishwa na watu wazima, idadi ndogo ya watoto walionyesha dalili zinazohusiana na mfumo wa juu wa kupumulia kama kutiririkwa na makamasi na makamasi hayo kujaa puani.

Watoto huugua homa kwa muda mrefu kama tu watu wazima. Kumekuwa na ripoti za baadhi ya watoto kuugua nimonia.

Baadhi ya watoto pia walitapika, kuumwa na tumbo, kuendesha na kukumbwa na dalili zingine zinazohusiana na mfumo wa mmeng’enyo.

Ni idadi ndogo tu ya watoto waliokumbwa na tatizo la kushindwa kunusa au kukosa ladha ambalo kwa kawaida limeshuhudiwa miongoni mwa watu wazima.

Lakini wazazi wanashauriwa kuendelea kutahadhari dhidi ya matatizo kama hayo kwa watoto wao. Baadhi ya wagonjwa walio chini ya umri wa miaka 20 wanaoweza kuelezea malalamiko yao, wameripoti dalili kama hizo.

Wataalam wanasema kuwa baadhi ya watoto walioambukizwa huenda wakakosa kuonyesha dalili. Wanawashauri wazazi kuwafuatilia watoto wao kwa makini kwa sababu huenda wakashindwa kuelezea hali zao barabara.

Pia tuliuliza ikiwa kumekuwa na visa ambapo mtoto amekuwa katika hali mahututi baada ya kuambukizwa virusi vya korona.

Wataalam wanasema kumekuwa na visa vichache vya hali kuwa mahututi miongoni mwa watoto ikilinganishwa na watu wazima. Hata hivyo, sawia na watu wazima, watoto wanaweza wakakumbwa na matatizo ya kupumua. Watoto chini ya umri wa miaka 2 huonekana kukumbwa na dalili kali na ni lazima wafuatiliwe kwa uangalifu.

Barani Ulaya na nchini Marekani, kumekuwa na ripoti za watoto walio na umri wa karibu miaka 10 kukumbwa na matatizo ya moyo baada ya siku chache za kuwa na homa yakifuatwa na maumivu ya tumbo, kuendesha na vipele. Kufikia sasa, visa vichache kama hivyo vimeripotiwa nchini Japani.

127. Ni zipi hali tano hatari zaidi ambazo zimetajwa mara nyingi katika ripoti za habari? -2-

Jopo linaloishauri serikali ya Japani kuhusu janga la virusi vya korona hivi karibuni limeonya juu ya hali tano hatari zaidi zinazoweza mara nyingi kusababisha maambukizi ya makundi.

Hali hizo ni zifuatazo;
Mikusanyiko inayohusisha unywaji pombe.
Idadi kubwa ya watu wanaokula na kunywa kwa muda mrefu.
Kuzungumza na mwenzio bila kuvaa barakoa.
Watu wengi kuishi ama kutumia pamoja eneo la ndani lenye nafasi ndogo.
Kutangamana au kuvuta sigara wakati wa mapumziko sehemu za kazi.

Tuanze na hali ya kwanza ambayo ni mikusanyiko inayohusisha unywaji pombe.
Huwa tunaonekana kuchangamka tunapokunywa pombe na kutufanya tuzungumze kwa sauti kubwa. Na wengi wanaweza kukaa kwa muda katika eneo la ndani lenye nafasi ndogo wakati wa mikusanyiko kama hiyo. Mbali na hilo, katika hali kama hizo, wahudhuriaji mara nyingi hutumia kwa pamoja vikombe vya pombe na vijiti vya kulia. Hali hizi husababisha hatari kubwa ya maambukizi.

Hebu sasa tuzungumzie hali ya idadi kubwa ya watu wanaokula na kunywa kwa muda mrefu. Kwa kawaida, hatari ya maambukizi ni kubwa kwenye baa na vilabu vya usiku ama wakati wa kuhama baa moja kwenda nyingine usiku ikilinganishwa na kupata mlo wa haraka. Pia inajulikana kwamba watu huonekana kuzungumza kwa sauti kubwa zaidi na kutoa vitone vingi wakiwa watano au zaidi wakiwa wameketi kwa kuzunguka meza.

Kuzungumza na mwenzio kwa karibu bila kuvaa barakoa kunaongeza hatari ya maambukizi kwa kuwatemea wengine vitone na vijitone. Pia watu wanaombwa kujihadhari na mazungumzo ya ndani ya magari au mabasi wanaposafiri.

126. Ni zipi hali tano hatari zaidi ambazo zimetajwa mara nyingi katika ripoti za habari? -1-

Jopo linaloishauri serikali ya Japani kuhusu janga la virusi vya korona hivi karibuni limeonya juu ya hali tano hatari zaidi zinazoweza mara nyingi kusababisha maambukizi ya makundi.

Hali hizo ni zifuatazo;
Mikusanyiko inayohusisha unywaji pombe.
Idadi kubwa ya watu wanaokula na kunywa kwa muda mrefu.
Kuzungumza na mwenzio bila kuvaa barakoa.
Watu wengi kuishi ama kutumia pamoja eneo la ndani lenye nafasi ndogo.
Kutangamana au kuvuta sigara wakati wa mapumziko sehemu za kazi.

Tuanze na hali ya kwanza ambayo ni mikusanyiko inayohusisha unywaji pombe.
Huwa tunaonekana kuchangamka tunapokunywa pombe na kutufanya tuzungumze kwa sauti kubwa. Na wengi wanaweza kukaa kwa muda katika eneo la ndani lenye nafasi ndogo wakati wa mikusanyiko kama hiyo. Mbali na hilo, katika hali kama hizo, wahudhuriaji mara nyingi hutumia kwa pamoja vikombe vya pombe na vijiti vya kulia. Hali hizi husababisha hatari kubwa ya maambukizi.

Hebu sasa tuzungumzie hali ya idadi kubwa ya watu wanaokula na kunywa kwa muda mrefu. Kwa kawaida, hatari ya maambukizi ni kubwa kwenye baa na vilabu vya usiku ama wakati wa kuhama baa moja kwenda nyingine usiku ikilinganishwa na kupata mlo wa haraka. Pia inajulikana kwamba watu huonekana kuzungumza kwa sauti kubwa zaidi na kutoa vitone vingi wakiwa watano au zaidi wakiwa wameketi kwa kuzunguka meza.

Kuzungumza na mwenzio kwa karibu bila kuvaa barakoa kunaongeza hatari ya maambukizi kwa kuwatemea wengine vitone na vijitone. Pia watu wanaombwa kujihadhari na mazungumzo ya ndani ya magari au mabasi wanaposafiri.

123. Kwa nini Australia haikuwa na majanga sambamba ya mafua na virusi vipya vya korona msimu huu wa baridi?

Msimu wa baridi katika ncha ya kusini ya dunia hudumu kuanzia mwezi Juni hadi Agosti. Hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Mei, serikali ya Australia ilikuwa imepata dozi milioni 18 za chanjo ya influenza, ambazo ni milioni tano zaidi ya mwaka jana. Maafisa walitoa wito kwa watu kupata chanjo ili kuzuia huduma za afya kuzidiwa na majanga yatokeayo kwa wakati mmoja.

Eneo la New South Wales palipo na jiji kubwa zaidi nchini Australia la Sidney, lilikuwa katika hali ya juu ya tahadhari dhidi ya uwezekano wa kutokea milipuko ya mafua katika makazi ya kuwatunza wazee. Liliwataka wafanyakazi wote na wageni kama vile ndugu wa familia kuchanjwa.

Kupitia juhudi kama hizo, nchi hiyo haikuripoti vifo vyovyote vilivyotokana na influenza kuanzia mwezi Mei hadi Septemba 20. Idadi ya watu walioambukizwa katika kipindi hicho ilikuwa ni asilimia 7.3 ya idadi ya mwaka jana. Kulikuwa na vifo 36 vilivyotokana na mafua kuanzia mwanzoni mwa mwaka hadi Septemba 20. Hiyo ilikuwa ni asilimia 5.1 ya idadi ya kipindi kama hicho mwaka jana.

Daktari Jeremy McAnulty wa New South Wales Health anasema kiwango cha chanjo dhidi ya mafua kilikuwa juu sana msimu huu wa baridi kwa sababu ya wasiwasi wa kutokea majanga mawili sambamba, na anaamini hali hiyo ilichangia pakubwa.

Aliashiria kuwa hatua za kukabiliana na maambukizi ya virusi vya korona kama vile kutokaribiana, matukio makubwa kuwekewa vizuizi na uelewa zaidi kuhusu kunawa na kutakasa mikono, zilikuwa na ufanisi mkubwa katika kudhibiti kuenea kwa mafua.

122. Taasisi za tiba za Japani zitakabiliana vipi na uwezekano wa kutokea kwa maambukizi ya virusi vya korona na influenza kwa wakati mmoja?

Virusi vipya vya korona na vya mafua ya msimu vina dalili zinazofanana, kama vile homa na kukohoa, hivyo kuna wasiwasi kuwa kliniki za maeneo zitakuwa na wakati mgumu kuwashughulikia wagonjwa iwapo milipuko itatokea wakati mmoja. Ili kuzisaidia kliniki kujiandaa kwa milipuko inayoweza kutokea wakati mmoja, Chama cha Magonjwa Ambukizi cha Japani, kimeandaa mwongozo juu ya utambuzi wa magonjwa.

Mwongozo huo unashauri kuwa katika maeneo ambapo kumetokea mlipuko wa virusi vya korona, wagonjwa kimsingi wanapaswa kupimwa aina zote mbili za virusi, yaani vile vya mafua na korona, ili kuepuka kutozingatia visa vya virusi vipya vya korona.

Mwongozo huo unatoa ushauri kwa kuzingatia kipimo cha alama nne ili kutathmini hali ya maambukizi katika eneo husika. Unasema kuwa katika kiwango cha kwanza, pale hakuna visa vya korona vilivyoripotiwa mkoani, upimaji wa virusi vya korona kimsingi hauhitajiki, isipokuwa kwa wale waliotembelea maeneo yenye maambukizi, katika kipindi cha majuma mawili yaliyopita.

Unaendelea kusema kuwa katika kiwango cha nne, pale kisa cha virusi vya korona kisichofahamika njia ya maambukizi kinaporipotiwa katika eneo majuma mawili yaliyopita, upimaji wa virusi vya korona unashauriwa kufanyika kwa wagonjwa wote wenye homa.

Kuhusu watoto, mwongozo huo unapendekeza sana wapewe chanjo dhidi ya mafua msimu huu wa baridi, kwa sababu huwa wanakabiliwa na maambukizi ya mara kwa mara na kueneza virusi. Mwongozo huo pia unasema ni muhimu kwa watoto kupimwa mafua na virusi vya korona kwa wakati mmoja. Lakini pia unasema ikiwa upimaji wa virusi vya korona hauwezi ukafanyika haraka, wagonjwa wanaweza kupimwa na kutibiwa mafua kwanza, na kupimwa virusi vya korona siku mbili baadaye, iwapo hali zao hazitaimarika.

Chama hicho kinasema kinawataka madaktari kote nchini Japani kuutumia mwongozo huo hadi msimu huu wa baridi utakapomalizika. Kinasema taarifa mpya zitawekwa kwenye mwongozo huo zipatikanapo.

121. Kwa namna gani chanjo zinazotengenezwa na Pfizer na taasisi zingine zinatofautiana na zile za influenza.

Inasemekana ni vigumu kutengeneza chanjo za virusi ambavyo vinasababisha maambukizi ya mfumo wa upumuaji. Vyanzo vya habari ikiwa ni pamoja na wizara ya afya ya Japani vinasema kwamba chanjo za mafua zenyewe haziwezi kutulinda dhidi ya maambukizi. Lakini chanjo hizo zinatarajiwa kwa kiasi fulani kupunguza hatari ya kupata dalili, ama hata ikiwa dalili zitatokea, chanjo zinaaminika kuweza kuzuia dalili hizo kuwa kali.

Tafiti nchini Japani zimeripotiwa kuonyesha kwamba katika watu walio na umri wa miaka 65 au zaidi, chanjo za mafua zina ufanisi katika kuzuia dalili kwa asilimia 34 hadi 55 na kuzuia vifo kwa asilimia 82. Pia baadhi ya tafiti zimeripotiwa kubaini kwamba katika watoto walio chini ya umri wa miaka sita, chanjo zinazuia hatari ya kupata dalili kwa takribani asilimia 60.
Kwa upande mwingine, katika visa vingi, utengenezwaji wa chanjo za virusi vya korona unatumia teknolojia tofauti kabisa na zile zilizotumika katika chanjo za kawaida za mafua. Bado hatujui ni kwa kiasi gani tunaweza kutarajia ufanisi kutoka kwa chanjo hizo mpya.

Chanjo za mafua zinatengenezwa kutokana na virusi vyenyewe. Vinakuzwa na kisha kudhoofishwa kwa kutumia kemikali ili visiweze kusababisha maambukizi.

Chanjo zinazotengenezwa na Pfizer zinatumia jeni inayoitwa mRNA, ambazo zina taarifa juu ya virusi vipya vya korona. Mara zitakapokuwa ndani ya mwili, zitafanya kazi kama mwongozo katika kutengeneza sehemu ya virusi ambavyo vitaanzisha mfumo wa kinga.

Nakayama Tetsuo, profesa wa mradi katika Chuo Kikuu cha Kitasato, anafahamu vizuri utengenezaji wa chanjo. Anasema kwamba katika chanjo ya Pfizer, mRNA imekuwa ikiambatanishwa katika chembechembe za lipidi. Anasema kwamba hili linaweza kuongeza uzalishaji wa kingamwili.

120. Hatari gani zinazowakabili wanawake wajawazito kutokana na maambukizi ya virusi vya korona?

Utafiti uliofanywa hadi mwishoni mwa mwezi Juni na Chama cha Madaktari wa Uzazi na Wanajinakolojia nchini Japani, kinachojumuisha madaktari katika nyanja hiyo ya utabibu, ulionyesha kuwa asilimia ya wanawake walioambukizwa virusi vya korona wanaougua sana, iliongezeka kwa wanawake wajawazito walio katika awamu ya mwisho ya ujauzito wao. Madaktari wanasema ingawa hatari za hali zao kuzorota huwa haziongezeki sana kwa wanawake wajawazito walioambukizwa, wale walio katika awamu za mwisho za ujauzito wanapaswa kuwa makini.

Chama hicho kiliwafuatilia kwa karibu wanawake 58 waliopatwa na dalili kama vile homa. Picha za CT scan zilionyesha kuwa baadhi yao walianza kuonyesha dalili za nimonia. Walibaini kuwa kati ya wanawake 39 waliokuwa na ujauzito wa chini ya wiki 29, 4 walibainika kuwa na nimonia au asilimia 10 ya idadi ya jumla.

Hii ikilinganishwa na wanawake 19 waliokuwa na ujauzito wa majuma 29 ama zaidi. Kumi walikutwa na nimonia ama asilimia 53 ya idadi ya jumla.

Kadhalika, watatu kati ya wanawake waliokuwa na ujauzito wa chini ya wiki 29 walipatiwa oksijeni, ama asilimia 8 ya idadi ya jumla. Hii ikilinganishwa na saba walio katika awamu za mwisho za ujauzito wao waliopatiwa oksijeni, au asilimia 37 ya idadi ya jumla. Data zinaonyesha kuwa hali ya wanawake walio katika awamu za mwisho za ujauzito wao ilionekana kuzorota.

Wengi wa wanawake wajawazito walioambukizwa virusi hivyo walipona bila kukumbwa na dalili zozote za muda mrefu. Chama hicho kinasema mtalii wa kigeni alifariki baada ya kuonyesha dalili muda mfupi baada ya kuwasili nchini Japani.

Kinasema kuwa hakuna ripoti za kuambukizwa zilizoripotiwa kwa watoto waliozaliwa.

Profesa Sekizawa Akihiko wa Chuo Kikuu cha Showa alisimamia utafiti huo. Alisema ni wanawake wachache wajawazito wameambukizwa virusi hivyo, kuonyesha kuwa wengi wao walifanikiwa kuchukua hatua za kujikinga. Anasema matokeo yanaonyesha kuwa wanawake wajawazito hawakabiliwi na hatari kubwa za kipekee za kuugua sana, lakini aliongeza kuwa wanapaswa kuwa waangalifu, kwani wanawake wanaokaribia kujifungua huonekana kupatwa na dalili kali zaidi.

Chama cha Magonjwa Ambukizi ya Uzazi na Jinakolojia nchini Japani kimeweka kwenye tovuti yake taarifa ya namna ya kuzuia maambukizi ya virusi vya korona. Tovuti hiyo imebuniwa kwa ajili ya wanawake wajawazito na wale wanaotamani kujaaliwa watoto.

Kwa mujibu wa tovuti hiyo, kasi ya ugonjwa baada ya kuambukizwa haitofautiani baina ya wanawake wajawazito na wasio wajawazito nchini Japani. Hata hivyo, kilisema kwamba kumekuwepo na visa vya wanawake wajawazito kuonyesha dalili kali na kuugua nimonia.

Satoshi Hayakawa ni Profesa wa idara ya tiba katika Chuo Kikuu cha Nihon, aliyeandaa hoja muhimu za utafiti huo. Anasema mapafu ya wanawake katika awamu za mwisho za ujauzito huwa yanaonekana kushinikizwa wakati kijusi kinapokua, na iwapo wataugua nimonia, dalili zao zinaweza kuwa kali.

Hayakawa anasema matokeo ya utafiti wao yanaunga mkono kile walichokitarajia. Aliongeza kuwa kumekuwepo na visa vichache vya wanawake wajawazito kuugua sana nchini Japani, na kwamba hakuna haja ya kuogopa sana. Hata hivyo, Hayakawa aliongeza kuwa uangalifu unapaswa kuzingatiwa ili kuzuia maambukizi ya virusi.

119. Je, athari hizo hutokea kwa kiwango gani?

Visa vya athari za muda mrefu zinazoendelea kwa miezi kadhaa vimeripotiwa nchini Japani na maeneo mengine ulimwenguni baada ya wagonjwa kupimwa na kuonekana hawana tena maambukizi na kisha kuruhusiwa kutoka hospitalini. Watu wengi wanasemekana kupata homa, uchovu, kushindwa kupumua vizuri au matatizo ya viungo kiasi kwamba maisha yao ya kila siku yanaathiriwa.

NHK ilifanya utafiti kwenye taasisi za afya zilizotengwa kutibu magonjwa ambukizi pamoja na hospitali za vyuo vikuu jijini Tokyo kuhusu hali za wagonjwa wa korona baada ya kukamilisha matibabu. Taasisi 18 kati ya 46, bila kujumuisha hospitali ambazo hazikuwahi kulaza mgonjwa wa korona, zilishiriki utafiti huo.

Taasisi hizo zilisema kuwa, kufikia mwishoni mwa mwezi Mei mwaka huu, watu 1,370 walipimwa na kutokutwa tena na virusi hivyo, na walikuwa ama wameruhusiwa kutoka hospitalini au kuhamishiwa hospitali zingine baada ya afya zao kuimarika au dalili kupungua. Watu takribani 98, sawa na asilimia saba ya wagonjwa wote walioruhusiwa kutoka hospitalini, waliripotiwa kuwa na matatizo yaliyoathiri maisha yao ya kila siku.

Watu 47 walikuwa na matatizo ya kushindwa kupumua vizuri kutokana na athari za muda mrefu za nimonia na shida zingine zinazosababishwa na virusi hivyo. Watu sita walihitaji vifaa vya kuwasaidia kuvuta oksijeni nyumbani.

Watu 46 walipoteza nguvu za misuli au walishindwa kujongea vizuri kutokana na kulazwa hospitalini kwa muda mrefu. Watu 27 walikumbwa na tatizo la kupoteza kumbukumbu kutokana na uzee na sababu zinginezo.

Taasisi zilizojibu zilisema kuwa, baadhi ya watu walipatwa na tatizo la kushindwa kutambua harufu pamoja na tatizo la ubongo kushindwa kufanya kazi kikamilifu.

Wengi miongoni mwa watu waliosumbuliwa na athari hizo walikuwa wametibiwa kwa kuwekewa mashine ya kusaidia kupumua au mashine zingine za kusaidia ufanyaji kazi wa mfumo wa upumuaji pamoja na moyo.

Taasisi moja miongoni mwa zilizojibu utafiti huo ilibainisha kuwa, kwa baadhi ya visa, hata baada ya wagonjwa kutokutwa tena na virusi hivyo, bado walihitaji kiwango cha juu cha huduma za uuguzi, na kuwa idadi ya wagonjwa wa aina hiyo inaweza kuathiri uwezo wa utoaji huduma za afya. Tasisi hiyo imesema kuwa, ni muhimu kuwepo na mpango mkakati utakaozingatia wagonjwa wazee kuruhusiwa kutoka hospitalini.

Taasisi nyingine iliyojibu utafiti huo ilieleza kuwa, itahitaji kukuza uelewa kuhusu matatizo mbalimbali ambayo huendelea baada ya wagonjwa kuruhusiwa kutoka hospitalini na kupanua mtandao wa usaidizi.

117. Iwapo kweli baadhi ya watu huendelea kupata dalili hata baada ya kupona COVID-19?

Timu ya watafiti kutoka Kituo cha Taifa cha masuala ya Afya na Tiba ya Kimataifa cha Japani kilifanya utafiti wa kuwafuatilia wagonjwa wa virusi vya korona waliokuwa wamepona ugonjwa huo na kuruhusiwa kutoka hospitalini. Walibaini kuwa, baadhi ya watu hao walipata tatizo la kunyonyoka nywele. Baadhi walilalamika kushindwa kupumua vizuri na kupoteza uwezo wa kuhisi ladha au harufu, hata baada ya miezi minne. Timu hiyo inasema kuwa, itaendelea na utafiti huo kwa lengo la kubainisha sababu zinazopelekea dalili endelevu.

Tatizo la kunyonyoka nywele limewahi kuripotiwa pia kwa baadhi ya watu waliopona ugonjwa wa Ebola na homa ya dengi. Daktari Morioka Shinichiro, ambaye ni miongoni mwa watafiti wa timu hiyo anasema pia inawezekana kuwa tatizo la kunyonyoka nywele huenda limechochewa na msongo wa mawazo kutokana na matibabu ya muda mrefu.

116. Hatua za kujilinda dhidi ya maambukizi ya mara nyingine.

Jitihada katika viwango vyote zinaendelea za kufanya chanjo zipatikane hivi karibuni. Lakini wataalamu wanaonya tusibweteke. Wanatutaka kuendelea na utekelezaji wa hatua za msingi, ikiwemo kunawa vizuri mikono, kuepuka kinachoitwa 3Cs--- “crowded places” yaani maeneo yenye watu wengi, “close-contact settings” yaani maeneo yenye nafasi ndogo na “confined and enclosed spaces” yaani maeneo yenye mzunguko mdogo wa hewa--- pamoja na kutokaribiana.

Ripota wa NHK wanaoangazia virusi vipya vya korona wanasema bado kuna mambo mengi tusiyoyajua kuhusu virusi hivyo. Wanasema kwamba tunapaswa kufuatilia kwa karibu maendeleo ya tafiti mbalimbali. Lakini wanasisitiza kuwa ni muhimu kwetu kuendelea kuchukua hatua za msingi kwa kina.

115. Namna ya kukabiliana na kirusi hiki kigumu ambacho hakioneshi dalili ya kutoweka.

Matsuura Yoshiharu, Profesa katika Chuo Kikuu cha Osaka na Mwenyekiti wa Chama cha Wataalamu wa Virusi nchini Japani, anasema tunapaswa kuwa na makisio kwamba maambukizi ya mara nyingine yanawezekana kama tu inavyotokea kwa virusi vya korona vya kawaida vinavyosababisha mafua, na kusababisha maambukizi ya kujirudia. Profesa Matsuura anasema kuwa kirusi kisichasababisha maambukizi ya kujirudia ni nadra sana. Pia anasema kwamba virusi haviwezi kuishi kama vitamuua mwenyeji wao. Historia ndefu kati ya binadamu na virusi inaonesha kuwa kadiri maambukizi yanavyojirudia, ndivyo dalili zinavyokuwa dhaifu. Profesa huyo amesema hatupaswi kuviogopa sana virusi.

114. Je, kuna chanjo zingine zozote fanisi? -2-

Tulimuuliza Profesa Sasaki Hitoshi wa Chuo Kikuu cha Nagasaki, anayefanyia kazi uendelezaji wa chanjo inayowezesha uzalishaji kingamwili kwenye utando laini uliopo mapafuni. Wakati virusi vinaponasa kwenye utando uliopo kwenye mapafu hayo, vinaweza kusababisha nimonia.
Chanjo hii inalenga kuzuia maambukizi ya virusi kwenye sehemu ya kuingia mwilini.

Imeundwa kwa chembe ndogo zisizo halisi zilizosanisiwa za RNA ya virusi vipya vya korona. Chanjo hii huvutwa ndani kupitia mdomoni, kwa hivyo inafika moja kwa moja kwenye utando laini wa mapafu. Watafiti wanaamini kwamba chanjo hii inaweza kuwa na ufanisi mkubwa kwa sababu inawezesha uzalishaji wa kingamwili katika sehemu ambayo virusi vinafanya kazi.

113. Je, kuna chanjo zingine zozote fanisi? -1-

Chanjo nyingi zimesanifiwa kutengeneza kingamwili kwenye mkondo wa damu. Lakini utafiti na uendelezaji pia unaendelea kuhusiana na chanjo zinazosaidia mwili kuzuia maambukizi.

Profesa Katayama Kazuhiko wa Chuo Kikuu cha Kitasato, anafanyia kazi aina mpya ya chanjo ya kupuliza puani. Kwa kuiweka chanjo hiyo puani, anaamini kuwa kingamwili zinaweza kubuniwa kwenye sehemu ya juu ya mfumo wa upumuaji na virusi vinaweza kuzuiwa kwenye sehemu ya kuingilia mwilini. Anasema amenuia kuendelea na utafiti katika kipindi cha miaka kadhaa ijayo.

Profesa Katayama anasema iwapo kingamwili za immunoglobin-A zinaweza kutengenezwa kwenye tando laini za pua, maambukizi yanaweza kukomeshwa kabla ya virusi kuzaliana kwa idadi kubwa, hivyo virusi vinaweza kuzuiwa kufikia mapafu.

112. Uhusiano kati ya matukio ya kuambukizwa tena na ufanisi wa chanjo zinazotengenezwa hivi sasa.

Ni muhimu kutathmini maambukizi ya mara ya pili kwani yanaweza kushawishi utengenezaji wa chanjo. Chanjo zinalenga kutoa kingamaradhi kwa magonjwa ambukizi kwa kutoa hali dhaifu ya virusi na kuchochea mwili kutengeneza kingamwili. Hata hivyo, kuna maswali yanayohusu ufanisi wa chanjo ikiwa watu walioambukizwa waliozalisha kingamwili, wanaambukizwa tena.

Profesa Nakayama Tetsuo ni Mwanavirolojia katika Chuo Kikuu cha Kitasato. Anaonya watu kutokuwa wepesi wa kufikia hitimisho kwamba, chanjo hazifanyi kazi kwa sababu tu ya watu kuambukizwa tena. Nakayama anasema ingawa maambukizi ya mara ya pili yanawezekana hata baada ya chanjo kutengenezwa na kutolewa, kuna faida za kupewa chanjo.

Nakayama anasisitiza kuwa chanjo hazilengi tu kutoa uhakika wa kuzuia maambukizi, lakini zinadhaniwa kuwa na matokeo mengine, ikiwa ni pamoja na kuzuia wagonjwa kupata dalili kali.

111. Je, tunaweza kuzuia kuambukizwa tena?

Tulimuuliza Profesa Katayama Kazuhiko wa Chuo Kikuu cha Kitasato, aliyetuambia kwamba ni vigumu kuzuia watu kuambukizwa tena.

Virusi vya korona vinaingia mwilini mwetu kupitia utando laini uliopo juu ya njia ya mfumo wa upumuaji, inayohusisha pua na koo. Baadaye, kingamwili iitwayo “Immunoglobulin A, au IgA”, hutengenezwa kwenye utndo huo kupambana na virusi vinavyoingia.

Hata hivyo Katayama anasema kiwango hicho cha IgA huwa na tabia ya kupungua katika kipindi kifupi baada ya mtu kuambukizwa virusi na kuzalisha kingamwili. Hii ndiyo sababu ya yeye kusema tuna nafasi ndogo ya kuzuia virusi vya korona mpakani mara ya pili.

Katayama amepanga kuanzisha mradi wa utafiti kubaini kiwango cha IgA kinachozalishwa kwenye sehemu ya juu ya njia ya hewa kwa mtu aliyeambukizwa na hudumu kwa muda gani. Mradi huu unaweza kutoa mwanga juu ya swali letu, maambukizi ya mara zingine hutokea mara ngapi?

110. Iwapo dalili za maambukizi ya mara ya pili ni kali au la.

Wataalam wanasema kuwa, kwa virusi vya aina zingine nyingi mbali na virusi vya korona, dalili za maambukizi ya mara ya pili huwa si kali au wakati mwingine hakuna kabisa dalili yoyote

Mfano mzuri ni virusi viitwavyo “Respiratory Syncytial (sin-si-kchio)” au RSV vinavyosababisha dalili kama za mafua, lakini ambavyo pia vinapowapata watoto wadogo katika visa kadhaa vinaweza kuleta madhara zaidi na kusababisha nimonia na ugonjwa mkubwa.

Profesa Nakayama Tetsuo wa Chuo Kikuu cha Kitasato, alichunguza kingamwili za watoto 91 walioambukizwa virusi vya RSV. Kwa kawaida miili yetu hutengeneza kingamwili inaposhambuliwa na virusi ili kujaribu kuondoa virusi hivyo mwilini. Inaaminika kuwa, wakati kingamwili za kutosha zinapotengenezwa, mwili unaweza kujikinga na maambukizi.

Utafiti wa Profesa Nakayama ulibaini kuwa, wakati mtoto wa mwaka mmoja anapoambukizwa virusi hivyo, ni kiasi kidogo tu cha kingamwili kinachozalishwa. Ilibainika kuwa, kiwango cha kingamwili kiliongezeka baada ya maambukizi ya mara kadhaa.

Utafiti huo ulibaini kuwa, kadiri kiwango cha kingamwili kinavyoongezeka mwilini, dalili za ugonjwa huzidi kuwa hafifu. Katika visa vingi, watu walioambukizwa virusi hivyo walikuwa na mafua yaliyotiririka pekee.

Hatahivyo kwa upande wa homa ya dengi, maambukizi ya mara ya pili yanaweza kusababisha dalili kali zaidi. Homa ya dengi ni ugonjwa unaoenezwa na mbu ambao huweza kusababisha homa kali pamoja na maumivu makali ya kichwa.

Hivyo basi, vipi kwa upande virusi vya korona? Profesa Nakayama anasema kuwa, inawezekana baadhi ya watu hawaonyeshi dalili yoyote na wala hawafahamu iwapo wameambukizwa virusi vya korona kwa mara ya pili. Anatoa angalizo kuwa hali hiyo inapaswa kufuatiliwa kwa umakini kwa kuwa dalili za maambukizi ya mara ya pili bado sio bayana.

109. Kuhusu watu walioambukizwa virusi hivyo, wakapona, na kisha kuambukizwa tena.

Visa kama hivyo vya watu kuambukizwa tena vimekuwa vikiripotiwa maeneo mbalimbali duniani. Huenda watu wamekuwa wakijiuliza iwapo kweli hilo linatokea, au iwapo chanjo itafanya kazi. Leo tutaangazia visa vya aina hiyo vilivyoripotiwa.

Watafiti katika Chuo Kikuu cha Hong Kong ndio waliokuwa wa kwanza ulimwenguni kuripoti mwezi Agosti mwaka huu juu ya kisa cha mtu aliyeambukizwa tena virusi hivyo. Walisema kuwa, walithibitisha kwamba mwanamume mwenye umri wa miaka 33 mara ya kwanza aliambukizwa virusi vya korona mwishoni mwa mwezi Machi mwaka huu, akapona, lakini akaambukizwa virusi hivyo kwa mara ya pili zaidi ya miezi minne baadaye.

Watafiti hao walisema kuwa mpangilio wa jeni za virusi viligunduliwa katika awamu hizo mbili za maambukizi ulitofautiana kwa kiasi fulani, kwahiyo hicho kilikuwa ni kisa cha kwanza kabisa ulimwenguni cha maambukizi ya mara ya pili yaliyothibitishwa kisayansi.

Baada ya ripoti hiyo ya watafiti wa Chuo Kikuu cha Hong Kong, makundi mengine ya watafiti kutoka Marekani, India na kwingineko yalitangaza kuwepo kwa visa kama hivyo.

Jarida la kisayansi la “Nature” limechapisha makala kuhusiana na visa vya watu kuambukizwa tena, na suala hilo linazidi kuvutia angalizo.

Tulimuuliza Profesa Nakayama Tetsuo wa Chuo Kikuu cha Kitasato ambaye ni mtaalumu wa virusi, iwapo kweli watu wanaweza kuambukizwa tena virusi vya korona.

Profesa Nakayama alisema kuwa, maambukizi kwa mara ya pili hutokea kwa virusi vya aina zingine, kwahiyo watu wanaweza pia kuambukizwa virusi vipya vya korona kwa mara ya pili.

98. Je, unaweza kuambukizwa virusi hivyo ukiwa kwa daktari wa meno?

Chama cha Madaktari wa Meno cha Japani kinasema zahanati za meno zimeweka njia anuai za kuzuia maambukizi, hivyo watu wasio na homa, kikohozi ama dalili zingine wanaweza kutibiwa kama ilivyo ada.

Watu wenye dalili kimsingi huombwa kujizuia kutaka kuchunguzwa na madaktari.

Lakini chama hicho kinasema baadhi ya visa vinaweza kuwa vya dharura ama hata vinavyotishia maisha kama vitaachwa bila kushughulikiwa, hivyo watu wanapaswa kwanza kuwasiliana na madaktari wao wa meno.

Taarifa hii inaweza kuthibitishwa katika tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

97. Iwapo ni salama kusafiri kwenye ndege ama treni iyendayo kasi ya Shinkansen?

Ni kweli kwamba hakuna mzunguko mzuri wa hewa ndani ya mabehewa ya treni ama ndani ya ndege kama ilivyo katika sehemu za nje. Lakini abiria wengi walioabiri ndege au treni hawapigi kelele au kugombana.

Tulimuuliza Sakamoto Fumie wa Hospitali ya Kimataifa ya Mtakatifu Luke. Yeye ni mtaalama wa hatua za kukabiliana na maambukizi. Anasema mtu hahitaji kuwa na wasiwasi zaidi kuhusiana na kupata maambukizi akiwa kwenye ndege ama treni alimuradi asalie kimya na kutokaribiana na abiria wengine.

Hata hivyo, Sakamoto anaongeza kuwa ingawa kuna hatari ndogo ya kuambukizwa wakati unaposafiri, unaweza kukabiliana na hatari kubwa ya maambukizi ikiwa utaenda kufurahia tafrija na kuzembea au kufanya mambo ya kipumbavu katika sehemu maalum iliyotengwa katika nyumba ya kupanga au hoteli unayoishi. Anasema tabia kama hiyo inaweza kusababisha maambukizi ya watu wengi, kwa hivyo mtu anapaswa kuwa mwangalifu zaidi ili kuepukana nayo.

Taarifa hii inaweza kuthibitishwa katika tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

96. Iwapo kuna uwezekano wa kuambukizwa virusi hivyo kwenye mabwawa ya kuogelea ama mabafu ya umma.

Tumemuuliza Sakamoto Fumie wa Hospitali ya Kimataifa ya Mtakatifu Luka ambaye ni mbobezi wa hatua za kukabiliana na maambukizi. Sakamoto anasema mtu yoyote hapaswi kuhofia juu ya kuambukizwa kupitia mabwawa ya kuogelea au mabafu.

Hata pale maji yanapokuwa na virusi, yanaweza kuwa na viwango vidogo vya virusi. Sakamoto anasema kutumia bwawa la kuogelea ama mabafu ya umma kuna hatari kidogo.

Anasema, hata hivyo kunaweza kusababisha hatari ya maambukizi iwapo utagusa vitu kwenye vyumba vya kubadilishia nguo ambavyo vimeguswa na watu wengi wasiotambulika. Anawashauri watu kutoshika nyuso, midomo, pua na macho yao kwa mikono yao kabla ya kunawa vizuri.

Taarifa hii inaweza kuthibitishwa katika tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

95. Kula mbogamboga zinazouzwa kwenye supamaketi bila kuzipika ni salama?

Anasema kwa sasa kuna nafasi ndogo ya wewe kuambukizwa virusi vya korona kupitia vitu unavyokula.

Watafiti wametoa makisio kwamba watu waliambukizwa virusi vya korona katika soko moja nchini China, kupitia wanyama walio hai wanaouzwa sokoni hapo. Hata hivyo, Sakamoto anasema hii haimaanishi watu waliambukizwa virusi hivyo kwa kula chakula walichonunua sokoni hapo.

Anasema hatuhitaji kuogopa sana alimuradi tule vyakula vinavyouzwa kwenye supamaketi, vilivyowekwa katika mazingira bora ya usafi. Anasema tunaweza kuviosha tu kama tunavyofanya kawaida na kuvila.

Taarifa hii inaweza kuthibitishwa katika tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

94. Iwapo tunahitaji kuweka masharti ya utumiaji wa sehemu za wazi pia.

Tulimuuliza Sakamoto Fumie wa Hospitali ya Kimataifa ya Mtakatifu Luke ambaye ni mtaalam wa hatua za kupambana na maambukizi swali hili. Sakamoto anasema hatari ya maambukizi kwa kiasi fulani ipo chini katika sehemu za wazi, kwa sababu tofauti na mazingira ya ndani, kuna mzunguko wa hewa kila wakati.

Hata hivyo, Sakamoto anaongeza kuwa hata unapokuwa katika sehemu za wazi, hatari ya maambukizi inaongezeka kwa kiasi fulani, ikiwa unazungumza na mtu kwa karibu. Anasema vinginevyo, hauna haja ya kuogopa sana.

Pia anatushauri kuendelea kutokaribiana pale tunapokuwa pamoja na kula nje, kwa mfano, katika hafla ya kufurahia kuchanua kwa maua ya mcheri. Anasema hilo litapunguza zaidi hatari ya maambukizi ikiwa watu wasiojihisi vizuri, wataepuka kuhudhuria hafla kama hiyo.

Taarifa hii inaweza kuthibitishwa katika tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

93. Je, tunapaswa kufanya nini iwapo mmoja wa wanafamilia ataambukizwa?

Kundi la wataalam wa magonjwa ambukizi akiwemo Profesa Kaku Mitsuo wa Chuo Kikuu cha Tiba na Dawa cha Tohoku, ametoa kitabu kidogo cha maelekezo kilichoorodhesha hatua maalum za kusaidia kuzuia ueneaji wa maambukizi.

Kinasema ni mtu mmoja tu anayepaswa kumhudumia mgonjwa wa virusi vya korona kwenye familia husika. Wahudumiaji wanapaswa kuvaa glavu, barakoa na kunawa mikono mara kwa mara. Wanapaswa kupima jotomwili lao mara mbili kwa siku na kujifuatilia iwapo wanazo dalili za aina yoyote.

Kinasema ili kuzuia kuenea kwa virusi, vyakula havitakiwi kuandaliwa kwenye sinia na vyombo havipaswi kutumiwa na watu wengi. Sahani zinapaswa kulowekwa kwenye vitakasa kwa walau dakika tano na baadaye vioshwe. Nguo ama matandiko ambayo huenda yakawa na majimaji ya mwili, zinapaswa kulowekwa kwenye majimoto ya nyuzi 80 za selisiasi kwa walau dakika 10 kabla ya kufuliwa.

Kitabu hicho pia kinasema ni muhimu kuruhusu hewa kuingia na kutoka kwenye vyumba kwa kufungua madirisha kwa dakika tano hadi 10 kila baada ya saa moja au mbili.

Kaku anasema kwamba watu wengi huenda wakawa hawajui nini cha kufanya kama wao ama familia zao zitaonyesha dalili za kuambukizwa, hivyo anatumai kuwa kitabu hicho kitafaa katika kupunguza hatari za maambukizi na kusaidia watu kujihisi salama katika maisha yao ya kila siku.

Taarifa hii inaweza kuthibitishwa kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

92. Njia ipi sahihi ya kunawa mikono yetu?

Virusi vya korona, sawia tu na influenza na mafua mengine yanayosababishwa na virusi, vinaenea kupitia vitone vinavyotokana na upumuaji kama vile kukohoa na kupiga chafya. Hatua za uzuiaji zinazopendekezwa na Shirika la Afya Duniani, WHO za kupambana na virusi vya korona, zinajumuisha kunawa mikono, kufunika mdomo na pua yako unapokohoa au kupiga chafya, ambazo pia ni tahadhari za jumla zinazochukuliwa dhidi ya magonjwa ambukizi.

Unaponawa mikono yako, unapaswa kufanya hivyo kwa kutumia sabuni na maji yanayotiririka, ukichukua sekunde zisizopungua 20 kusugua mikono yako vilivyo, ikiwemo katikati ya vidole vyako na ndani ya kucha zako. Wakati hakuna sabuni na maji yanayotiririka, ni bora pia kutumia vileo na vitakasa vingine vya mkono. Virusi vinavyochukuliwa na mikono yako vitaingia mwilini mwako kupitia macho, mdomo na pua. Kwa hivyo, tafadhali usiguse uso wako hadi unawe mikono yako barabara.

Kobayashi Intetsu ni Profesa wa Chuo Kikuu cha Toho anayejikita katika udhibiti wa maambukizi. Tulimuuliza hoja muhimu za unawaji mikono. Hiki ndicho alichotuambia.

“Mosi, tumia sabuni nyingi, na kwa uangalifu mkubwa sugua kila kidole. Osha vifundo vya mikono yako. Ikiwa utatumia kiwango kinachostahili cha sabuni, unapaswa kusalia na povu baada ya kusugua sehemu zote za mikono yako.

Unaweza ukatumia ama maji baridi au moto yanayotiririka kusuuza mikono yako. Ni bora kuikausha ukitumia karatasi safi ya taulo na kufunga maji bila kugusa moja kwa moja sehemu ya kufungia mfereji.

Unapokuwa huwezi kunawa mikono yako kwa sabuni na maji, tumia vitakasa vyenye kileo. Kiwango cha kitakasa unachotumia ni muhimu. Hakikisha unaisukuma hadi chini pampu ya kutolea kitakasa.”

Anasema ni muhimu kusugua kitakasa kwenye sehemu zote za mikono yako wakati bado nyevu, na kwamba kuisukuma pampu kikamilifu huhakikisha unapata kitakasa cha kutosha kufanya hivyo.

Taarifa hii inapatikana kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

91. Unapaswa kufanya nini wakati mkazi wa jengo la majumui anapobainika kuambukizwa virusi vya korona?

Hali kama hii ilitokea kwenye jengo moja la majumui lililopo mjini Asahikawa mkoani Hokkaido. Bodi ya chama cha wakazi wa jengo hilo ilimuuliza Mizushima Yoshihiro ambaye ni naibu mwenyekiti wa Zenkanren jinsi ya kulitakasa jengo hilo. Zenkanren ni shirika lisilokuwa la kujipatia faida na ni shirikisho la kitaifa la vyama vya usimamizi wa majengo ya majumui.

Mizushima alitembelea kituo cha afya ya umma cha eneo hilo na kuuliza ikiwa kinaweza kutuma mfanyakazi wake kulitakasa jengo hilo. Lakini kituo hicho kilikataa ombi hilo kikisema jengo hilo ni mali inayomilikiwa kibinafsi na hawawezi wakalitakasa.

Hali hii iliwaacha wakazi wa jengo hilo na kazi ya kulitakasa. Tulimuuliza mfanyakazi wa kituo cha afya ya umma mjini Asahikawa tunachopaswa kuzingatia tunapolitakasa jengo wenyewe.

Kwanza kabisa, tunahitaji kuvitakasa vitu vilivyo katika maeneo yanayotumiwa pamoja vinavyoguswa mara kwa mara na watu kwa mkono, moja kwa moja. Vinajumuisha vitufe vilivyo kwenye kibodi ya kengele ya mlango wa jengo, vitufe vya eleveta, sehemu za kushika mikono kwenye ngazi, vitu vilivyo ndani ya mabafu yanayotumiwa na watu wengi, na vitasa vya kwenye milango ya kuelekea katika ngazi za dharura.

Wanasema hakuna haja ya kupuliza kitakasa hewani kwa sababu huenda virusi visielee hewani kwa muda mrefu.

Wanawashauri wasafishaji kulowesha karatasi za jikoni ikiwa na asilimia 0.05 ya mchanganyiko wa sodium hypochlorite na kupangusa kila uso wa kitu kwa uangalifu mkubwa.

Ni bora watu kutopuliza mchangayiko huo kwenye karatasi ya jikoni kwa sababu wakifanya hivyo, wasafishaji wanaweza kuvuta mvuke huo wenye madhara. Aidha kupuliza kusikowiana kunaweza kukaacha nafasi ndogo isiyoloweshwa na kitakasa kwenye karatasi, hali inayosababisha utakasaji usiokuwa bora.

Tafadhali kumbuka kuwa tunachokisema hapa kinastahili katika mantiki ya Japani. Vituo vya afya ya umma katika nchi zingine huenda vikaitikia hali sawia kwa namna tofauti.

Taarifa hii inapatikana kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

90. Je, watoto wanapaswa kuvaa barakoa?

Takayama Yoshihiro kutoka Idara ya Magonjwa Ambukizi ya Hospitali ya Okinawa Chubu amekuwa akiisaidia serikali ya Japani kuandaa mikakati ya kukabiliana na virusi vya korona. Anatahadharisha dhidi ya kuvalisha watoto barakoa akisema huenda wakagusa nyuso zao mara kwa mara wanapovaa barakoa na hiyo itaongeza hatari ya maambukizi. Takayama anasema inapokuja kwa watoto, hatua za msingi kama vile kunawa mikono mara kwa mara na kuangalia halijoto yao wanapoondoka na kurejea nyumbani zinapaswa kupewa kipaumbele.

Chama cha Madaktari wa Watoto nchini Japani kinapendekeza watoto chini ya umri wa miaka miwili kutovaa barakoa kikisema inaweza ikawafanya kupata ugumu wa kupumua. Wizara ya Afya, Kazi na Ustawi pia inasema haitoi ombi kwa raia wote kuvaa barakoa kwani baadhi ya watoto wanapata shida kuvalia barakoa itakikanavyo.

Takayama anawatahadharisha wazazi kuhusiana na kuwalazimisha watoto wao kuvaa barakoa kwa sababu tu watoto wengine wanaivaa. Anawarai wazazi kuchukua hatua za msingi na kuzingatia hatua za ukuaji wa watoto wao wanapoamua ikiwa wanapaswa kuvaa barakoa au la.

Taarifa hii inapatikana kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

88. Maendeleo ya utengenezaji wa dawa ya kutibu virusi vya korona.

Zaidi ya miezi sita imepita tangu Machi 11 pale Shirika la Afya Duniani WHO lilipotambua kuwa maambukizi yalikuwa janga la dunia. Leo mada yetu inazungumzia maendeleo ya utengenezaji wa dawa ya kutibu virusi vya korona.

Kwa sasa hakuna dawa ambayo inaweza kuelezewa kama “dawa ya maajabu” kwa virusi vya korona. Hata hivyo, maendeleo yamepigwa katika kutafuta dawa, iliyotengenezwa kutibu magonjwa mengine, ambayo pia inaonyesha ufanisi katika kutibu virusi vya korona. Katika miezi sita, mengi yamebadilika katika juhudi za kutengeneza tiba ya virusi vya korona tangu mlipuko huo ulipoelezewa kama “janga.”

Katika siku za mwanzo kilikuwa na dawa ambazo mwanzoni zilionekana kuwa na matumaini, lakini ufanisi ambao haukuthibitishwa. Moja ya hizo dawa ilikuwa dawa ambayo inafifisha dalili za UKIMWI. Kilikuwa na matumaini kuwa utaratibu ambao unazuia virusi vya UKIMWI kuzaliana pia ungesaidia kutibu virusi vya korona. Hata hivyo, matokeo ya majaribio ya kitabibu yaliofanywa nchini China na Uingereza yalionyesha dawa hiyo haikupunguza kiwango cha vifo kwa wagonjwa waliougua zaidi na virusi vya korona.

Dawa nyingine ambayo ilionekana kuonyesha matumaini ilikuwa hydroxycholoquine ambayo inatumika kutibu malaria. Hata hivyo Idara ya Chakula na Dawa ya Marekani (FDA) mnamo mwezi Juni ilitengua kibali cha matumizi ya dharura ya dawa hiyo kwa ajili ya kutibu virusi vya korona, ikisema vipimo havikuonyesha kwamba dawa hiyo ilikuwa na ufanisi wa kutibu ugonjwa wa COVID-19.

Kwa upande mwingine kuna dawa zingine ambazo zimethibitishwa kufanywa kazi kwenye virusi vya korona. Hizi ni pamoja na remdesivir, ambayo ilitengenezwa kutibu Ebola. Majaribio yaliyofanyika nchini Marekani yalithibitisha dawa hiyo ilikuwa na ufanisi katika virusi vya korona. Mwezi Mei, ilikuwa dawa ya kwanza kuidhinishwa kutibu virusi vya korona nchini Japani.

Ufanisi wa steroid dexamethasone katika kupunguza kiwango cha vifo pia kimethibitishwa katika utafiti nchini Uingereza. Dawa hiyo pia ilianza kutumika katika tiba nchini Japani.

Miezi sita iliyopita, ufanisi wa kutibu virusi vya korona ulikuwa haujulikani. Wizara ya afya na ustawi wa jamii hivi sasa inashauri dawa hizo mbili katika miongozo yake ya kutibu virusi vya korona.

Kuna dawa zingine ambazo zinatengenezwa na zinafanyiwa majaribio ili kuthibitisha ufanisi wake.

Kampuni ya kutengeneza dawa ya Japani ambayo ilitengeneza dawa ya kutibu mafua ya Avigan, kwa mfano, inafanya majaribio yenye lengo la kupata idhini ya serikali kwa ajili ya matumizi ya dawa hiyo kama tiba ya virusi vya korona. Majaribio ya kitabibu pia yanafanywa kwenye dawa ya Actemra, ambayo inatibu ugonjwa sugu unaoathiri viungo. Dawa zingine zinazoonyesha matumaini ni pamoja na Alvesco, dawa ya kutibu pumu, na Futhan ambayo kawaida inatumika kutibu ugonjwa wa kongosho. Ikiwa ufanisi na usalama utathibitishwa, kuna matumaini kwamba dawa hizo pia zitatumika kutibu virusi vya korona.

Morishima Tsuneo wa Chuo Kikuu cha Kitabibu cha Aichi ambaye ni mtaalam wa magonjwa ambukizi, anasema watafiti wamefahamu kuhusiana na asili ya magonjwa katika kipindi cha nusu mwaka iliyopita na tiba kadhaa zenye ufanisi zimegundulika. Sababu hizo zimechangia kupunguza kiwango cha vifo vinavyotokana na virusi katika wimbi la pili la mlipuko huo nchini Japani.

Taarifa hii inaweza kupatikana kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

82. Unawezaje kupata maambukizi?

Mbali na kupitia vijitone vya mfumo wa upumuaji, virusi hivyo vinaweza kuambukizwa kwa njia ya kutogusa moja kwa moja.

Maambukizi kwa njia ya kutogusa moja kwa moja inaweza kutokea ikiwa mtu atagusa kitu baada ya mtu aliyeathirika. Mara nyingi watu hugusa nyuso zao pamoja na pua na midomo yao kila siku za maisha yao, na ikiwa watafanya hivyo kwa mikono iliyogusa virusi, wanaweza kupata maambukizi. Macho pia yanaweza kuwa njia ya kupata maambukizi, hivyo watu wanaweza kuathirika kwa kusugua macho yao.

Vijitone vidogo mno vinaaminika kusambaza virusi hivyo. Ni vidogo kuliko vitone na huelea hewani katika sehemu zenye mzunguko mdogo wa hewa. Ili kuzuia maambukzi kutokana na vijitone hivyo, watu wanashauriwa kuepuka C tatu. Closed poorly ventilated spaces yaani maeneo madogo yenye mzunguko finyu wa hewa, Crowded areas yaani maeneo yenye watu wengi na Conversation in close proximity yaani kufanya mazungumzo kwa umbali mdogo. Kwa kawaida vijitone vinasemekana kuanguka kabla ya kufika umbali wa kama meta 2, hivyo kudumisha angalau umbali huo baina ya watu inadhaniwa kuwa salama.

Si kila kitu kinajulikana kuhusu kusambaa kwa virusi hivi vipya. Ila kwa sasa hatua zipo kwa matumaini kuwa tunaweza kuzuia maambukizi kwa kuepuka kabisa vijitone na kutogusa virusi hivyo.

Ili kupunguza hatari ya maambukizi kote Japani mamlaka zinatoa wito kwa kila mmoja kuvaa barakoa, ili kuepuka kusambaa kwa vijitone, na kukaa umbali wa angalau meta 2 kila mmoja ikiwa kuna vijitone. Watu pia wanashauriwa kunawa mikono, ili wasijiambukize ikiwa wamegusa sehemu zenye virusi hivyo kwa mikono yao na kushika mdomo, pua au macho yao bila kujua.

Taarifa hii inaweza kuthibitishwa kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japani.

80. Kumekuwa na aina ngapi za virusi vya korona tangu awali ambavyo binadamu anaweza kuambukizwa?

Zimepatikana zaidi ya aina 50 za virusi vya korona. Aina sita kati ya hizo zinaambukizwa kwa binadamu. Nne kati ya sita hizo kwa kawaida zinagunduliwa kama mafua.

Watu wengi wanaaminika kupata moja au zaidi ya aina hizo nne za virusi vya korona wakati wa utoto wao.

Aina mbili zinazobaki ni SARS na MERS. Aina hizi mbili zinaonesha dalili kali kulinganisha na zile nne. Wataalamu wanasema wakati wa mlipuko wa aina hizo virusi sumbufu viliibuka.

Mwishoni mwa mwezi wa 12 mwaka jana, mamlaka za China zilichunguza visa vya homa ya mapafu huko Wuhan. Huo ndio wakati walipogundua aina ya saba ya virusi vya korona ambayo ilikutwa kwa binadamu, na kufahamika kama virusi vipya vya korona.

Wataalamu wengi walitarajia kwamba virusi hivi vipya kuibuka, lakini isingekuwa kitu cha kusumbua kama hivi.

Kama ilivyotajwa awali, aina nne ni mafua ya kawaida. SARS ilidhibitiwa kwa ufaulu kwa kuwa dalili zake ziligunduliwa kirahisi, na MERS haikuwa janga.

Hivyo watu hawakuwa katika tahadhari. Iliaminika kuwa hata kama virusi vipya vya korona vingeibuka, vingedhibitiwa au visingesambaa sana.

Kulikuwa na vitabu vilivyoonya hatari ya virusi vipya vya korona vitakavyosababisha janga. Lakini si wataalamu wengi duniani waliodhani ni kweli.

Taarifa hii inaweza kuthibitishwa kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japani.

79. Kwa nini virusi vipya vya korona vinasambaa maeneo mengi na kwa haraka?

Kwa sasa hakuna chanjo dhidi ya virusi hivi vipya vya korona. Ni kwa kiasi gani virusi vinaambukiza inaweza kutathminiwa kwa wastani wa idadi ya watu waliopata maambukizi kwa mara ya kwanza kutoka kwa mtu aliyeathirika. Mathalani, ikiwa mtu mmoja aliyeathirika ataambukiza virusi kwa wastani wa watu 0.5, ina maana virusi sio vya kuambukiza san ana huenda visisambae katika maeneo mengi. Lakini virusi hivi vipya vya korona, vinaaminika kwamba mtu mmoja aliyeathirika anaweza kuambukiza karibu watu 2.5.

Hata hivyo jopo la wataalamu linaloishauri serikali ya Japani juu ya virusi vya korona, linaamini kuwa haimaanishi kila mtu mmoja aliyeathirika anaambukiza watu 2.5. wataalamu wanasema kama kuna waathirika 10 wa virusi hivyo, wanane kati yao huenda wasimwambukize yeyote, wakati wawili wanaosalia wanaambukiza virusi kwa karibu watu 10 kila mmoja.

Tatizo lingine ni kuwa si rahisi kuwatambua waathirika wa virus vya korona. Watu walipoambukizwa virusi vya SARS, ambayo ni aina nyingine ya virusi vya korona, walipata dalili haraka hivyo watu wengine waliwajua wameathirika. Watu walioathirika wanaweza kutengwa ili kuzuia ueneaji wa virusi hivyo kwa wengine.

Lakini waathirika wa virusi vya korona wanaweza kueneza virusi hata kama hawaoneshi dalili, na hilo linafanya kuwa vigumu kuzuia ueneaji wa virusi hivyo.

Taarifa hii inaweza kupatikana pia katika tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japani.

78. Yapi ni maadili mazuri ya kukohoa? Na ninapaswa kuzingatia nini ninaponawa mikono?

Virusi vya korona, sawa tu na virusi vya influenza na mafua huenea kupitia vitone vinavyotolewa wakati mtu aliyeambukizwa anapokohoa au kupiga chafya.

Shirika la Afya Duniani, WHO linawataka watu kunawa mikono mara kwa mara na kuzingatia “maadili ya kukohoa” ili kuzuia ueneaji wa virusi hivyo. Hatua hizo ni sawa na zile zilizochukuliwa kukabiliana na magonjwa mengine ambukizi.

Wakati unaponawa mikono, tumia sabuni na maji ya kutiririka. Tumia sekunde zisizopungua 20 kusafisha juu ya mikono yako yote, ikiwa pamoja na katikati ya vidole na chini ya kucha. Ikiwa hakuna sabuni na maji, safisha mikono yako kwa kutumia vitakasa vya kileo.

Unaweza ukaambukizwa virusi hivyo ikiwa utagusa macho yako, mdomo na pua kwa mikono michafu. Hakikisha haugusi uso wako kabla ya kunawa mikono.

Ikiwa una dalili kama vile kukohoa au kupiga chafya, usikose kuzingatia “maadili ya kukohoa” yafuatayo, ili usiwaambukize watu walio karibu nawe hata ikiwa umeambukizwa.

Funika mdomo wako kwa tishu au uuweke chini ya kiwiko cha mkono wako wakati unapokohoa au kupiga chafya. Ukitumia tishu, itupe punde baada ya kuitumia na unawe mikono. Usifunike mdomo kwa viganja vya mikono yako kwa sababu vitaambukizwa virusi hivyo.

Taarifa hii inapatikana kwenye tovuti ya NHK World Japan na mitandao ya kijamii ya NHK.

77. Je, nilisikia kwamba si rahisi kufanyiwa vipimo vya PCR nchini Japani. Ni kwa nini?

Vipimo vya PCR hutambua nyenzo za jeni ya pathojeni na kubaini ikiwa mtu huyo ameambukizwa wakati huo. Ni vipimo ambavyo matokeo yake huwa sahihi sana lakini yanachukua muda. Inasemekana kwamba Japani haifanyi vipimo vingi vya PCR kama nchi zingine. Hii ni kwa sababu imekuwa na fursa chache za kufanya vipimo hivyo kabla ya mlipuko wa virusi vipya ya korona.

Mojawapo wa sababu ni kwamba Ugonjwa Hatari Unaoathiri Mfumo wa Upumuaji, yaani SARS au Ugonjwa Hatari Unaothiri Mfumo wa Upumuaji wa Mashariki ya Kati, yaani MERS. Haya yote yakiwa ni magonjwa yanayohitaji vipimo vya PCR, hayakuathiri Japani. Na inapokuja kwa suala la influenza, vifaa rahisi vya kufanyia vipimo vinatumika pakubwa, kwa hivyo vipimo vya PCR vimetumika kwa nadra mno nchini Japani.

Kwa sasa matumizi ya vipimo hivyo yanaongezwa kwa taratibu, lakini bado havijafikia kiwango ambapo vinaweza vikaenea haraka, na hiyo inasemekana kuwa changamoto.

76. Jinsi ya kuhakikisha vyumba vyako vina hewa safi itakikanavyo.

Kampuni ya kutengeneza milango na madirisha ya YKK AP pia imezungumzia na kujibu swali la jinsi ya kuhakikisha vyumba vyako vina hewa safi itakikanavyo.

Kwenye tovuti yake, kampuni hiyo inaorodhesha mapendekezo ya namna unavyopaswa kuhakikisha vyumba vyako vina hewa safi kwa kufungua madirisha itakikanavyo, katika muktadha wa virusi vipya vya korona.

Kampuni ya YKK AP inapendekeza “ufunguaji wa madirisha mawili badala ya moja”, na kwamba madirisha hayo yanapaswa kufunguliwa “yakikinzana kwa mshazari.”

Katika vyumba viliyo na dirisha moja tu, kampuni hiyo inapendekeza ufunguaji wa milango ya ndani ili kutengeneza njia ya kupitisha hewa, na kutumia feni kuzungusha hewa.

Kadhalika kampuni hiyo inapendekeza kuyafungua madirisha kwa kuyasogeza hadi katikati ili yafunguke pande zote.

Unaweza ukaipata taarifa hii kwenye tovuti ya NHK World Japan na mitandao ya kijamii ya NHK.

75. Unaweza ukahakikisha vipi kuna hewa safi katika vyumba wakati unapotumia viyoyozi?

Kampuni kubwa ya utengenezaji wa viyoyozi ya Daikin Industries inasema viyoyozi vingi huzungusha tu hewa katika chumba wala havihakikishi uwepo wa hewa safi. Kampuni hiyo sasa inawataka watu nyakati zingine kufungua madirisha yao na kuhakikisha hewa safi inaingia katika vyumba hivyo, wanapokuwa wamewasha viyoyozi vyao.

Baadhi ya watu huenda wakahisi kuwa wanatumia vibaya umeme ikiwa watafanya hivyo. Afisa mmoja alielezea njia ya kudhibiti matumizi ya umeme wakati ukipitisha hewa safi chumbani. Kwa sababu viyoyozi hutumia umeme mwingi unapoviwasha, unapaswa kwa kweli kuhakikisha vimewashwa wakati ukifungua dirisha lako.

Katika hali za joto kali, matumizi ya umeme pia yataongezeka ikiwa hewa nyingi kutoka nje itasababisha halijoto ya chumbani kupanda, kwa hivyo ni muhimu kupandisha kidogo halijoto ya kiyoyozi chako kabla ya kufungua dirisha ili kuruhusu hewa safi kuingia chumbani.

Unaweza ukaipata taarifa hii kwenye tovuti ya NHK World Japan na mitandao ya kijamii ya NHK.

73. Miongozo ya ndani ya makampuni kwenye maeneo ya uzalishaji ambapo ni vigumu kuhamia kwenye ufanyaji kazi nyumbani.

Kampuni ya kutengeneza malori na basi ya Mitsubishi Fuso zimeweka miongozo ya kuzuia maambukizi kwa wafanyakazi waliopo sehemu za utengenezaji.

Katika kiwanda cha kampuni hiyo kilichopo mji wa Kawasaki karibu na Tokyo, wafanyakazi wanaombwa kukaa ama kusimama angalau umbali wa mita 1.5. Pale wanapohitaji kusimama karibu karibu, kwa mfano wanapobeba pamoja vitu vizito, wavae ngao za usoni juu ya barakoa kwa ajili ya majaribio.

Wafanyakazi wote wabadili glavu zao za kazi mara moja kila baada ya nusu siku, na kuweka vitakasa kwenye chumba cha makabati mara nyingi ili kuzuia kusambaa kwa maambukizi.
NHK ilimuuliza afisa wa Mitsubishi Fuso Baba Takashi. Alisema kuchukua hatua za kuzuia maambukizi ni muhimu zaidi kwenye sehemu za utengenezaji wa malori ambapo ni vigumu kuwa na mifumo ya kujiendesha yenyewe na kazi nyingi zinafanywa kwa mikono.

Alisema mapambano dhidi ya virusi huenda yakaendelea kwa kipindi fulani na kwamba anataka kusikia mapendekezo kutoka kwa wafanyakazi na kuboresha mazingira ya kazi ili wafanyakazi wote waweze kufanywa kazi kwa usalama zaidi na furaha.

Kampuni ya Toyota Motor inayoongoza kutengeneza magari Japani, mwishoni mwa mwezi Machi ilichelewa kuanza zamu za jioni kwa nusu saa katika viwanda vyake vya utengenezaji vilivyopo mkoani Aichi. Hilo liliwapa wafanyakazi wa zamu ya mchana na ya usiku takribani dakika tisini ili kubadili na kupunguza nafasi ya wafanyakazi kukutana katika zamu mbalimbali.

Kampuni ya kutengeneza mashine nkubwa ya IHI Corporation iliwagawa wafanyakazi kwenye makundi mawili katika kiwanda chake cha kutengeneza injini za ndege kilichopo katika mji wa Mizuho mkoani Tokyo. Kila kundi linapaswa kufika kazini kila wiki ingine.

Kampuni nyingine ya kutengeneza malori ya Isuzu Motors iliongeza mara tatu idadi ya huduma za mabasi kwenye kiwanda chake cha Fujisawa mkoani Kanagawa wakati wa asubuhi wa kwenda kazini ili kuzuia msongamano kwenye mabasi.

Taarifa hizi inaweza kupatikana kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

71. Miongozo ya kuzuia maambukizi iliyozinduliwa na sekta ya reli na usafiri wa anga.

Kwa mujibu wa miongozo ya kawaida iliyotolewa na mitungo ya kampuni za reli ikiwa ni pamoja na kampuni ya JR na makampuni mengine makubwa ya reli, waendeshaji wanashauriwa kuwaomba abiria kuvaa barakoa, kufanya kazi nyumbani ili kuzuia msongamano, na kuepuka usafiri wa umma nyakati za abiria wengi.

Waendeshaji wa reli pia wanashauriwa kuweka vitakasa kwa uangalifu na kufungua madirisha ili kuboresha uingiaji wa hewa.

Mbali na hilo, viti vilivyohifadhiwa kwenye treni isiyosimama vituo vyote vitapangwa kwa ajili ya abiria kukaa mbalimbali.

Wakati huo huo, miongozo iliyotolewa na Chama cha Kampuni za Usafiri wa Anga cha Japani inapendekeza kampuni za usafiri wa anga kuwaomba abiria kuvaa barakoa, na wafanyakazi kuweka vitakasa mara kwa mara ndani ya ndege. Kampuni pia zinashauriwa kutoa vinywaji vilivyofungashwa ndani ya ndege.

Miongozo kwa waendeshaji wa majengo ya uwanja wa ndege inayaomba makampuni kuanzisha njia za kuwaomba abiria kudumisha umbali baina ya mtu na mtu katika sehemu ya ukaguzi wa taarifa za usafiri na wakati wa taratibu za ukaguzi wa usalama. Waendeshaji pia wanaombwa kusafisha kwa uangalifu maeneo yanayoguswa mara kwa mar ana abiria kwa kutumia vitakasa.

Katika kaunta za ukaguzi wa taarifa za usafiri, vifaa vinavyowagawa mtoaji huduma na abiria vinaweza kuwekwa pale inapohitajika ili kuzuia kusambaa kwa matone ya mate. Halijoto ya mwili itaangaliwa kwa abiria yeyote anayejihisi vibaya.

Katika viwanja vikubwa sita vya ndege vya Japani ikiwa ni pamoja na Haneda, Narita na Kansai, halijoto ya mwili ya abiria itaendelea kufuatiliwa kwa kutumia themografia.

Taarifa hizi inaweza kupatikana kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World Japan.

65. Virusi vya korona vinaweza kuambukizwa kabla mtu hajaonyesha dalili, kama vile homa na kikohozi?

Kundi moja la watafiti nchini Singapore linasema linaamini hali hiyo imetokea katika visa kadhaa. Watafiti hao walitafuta namna maambukizi yalivyotokea nchini Singapore na kutoa matokea yao katika ripoti iliyotolewa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Magonjwa Ambukizi nchini Marekani. Baada ya tathmini ya kina walibaini visa katika makundi saba ya maambukizi ambayo wanaamini usambaaji wake wa binadamu kwa binadamu umetokea kutoka kwa watu ambao hawakuonyesha dalili.

Watu wasio na dalili walianza kupata homa, kukohoa au kuwa na mafua kwa siku kadhaa baada ya kukutana na wengine ambao baadaye walipata virusi hivyo. Watafiti hao wanaamini watu wasio na dalili wameeneza maambukizi wakati ambapo hawakuwa na dalili kupitia vitone na njia zingine.

Baadhi ya maambukizi mengine ya kundi yametokea wakati wa masomo ya uimbaji. Watafiti hao wanasema hata ikiwa mtu alikuwa hakohoi, virusi hivyo vinaweza kuambukizwa kupitia vitone wakati wa kuimba kwa sauti kubwa au namna zingine.

Watafiti hao wanaamini hilo linathibitisha kwamba virusi hivyo vipya vya korona vinaweza kuambukizwa wakati ambao mtu hajaanza kuwa na dalili. Wanasema kuwatenga watu walioanza kuonyesha dalili pekee haitoshi, na ni muhimu kuepuka mikusanyiko na umati wa watu.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Julai 20. Pia zinapatikana katika tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World JAPAN.

57. Baadhi ya watu huvaa barakoa bila kufunika pua. Wataalamu wanafikiria nini juu ya hili?

Lengo kuu la kuvaa barakoa ni kuzuia vitone vinavyotoka wakati wa kupumua ama kutoka kwa mfumo wa kupumua visisambae, na kuzuia kiasi kikubwa cha vitone vinavyotolewa na mwathirika. Ikiwa pua yako haijafunikwa, vitone vinavyotoka kwa njia ya chafya vitasambaa. Pia, binadamu avutapo pumzi, asilimia 90 ya hewa inayovutwa inavutwa kupitia pua, hivyo kutofunika pua kunaongeza hatari ya maambukizi.

Unapovua barakoa, unatakiwa kuhakikisha kuna umbali wa kutosha wa kimwili. Inasemekana kwamba vitone hivyo vinaweza kusambaa hadi karibu mita mbili. Kama hatua ya kuzuia kuzimia kutokana na joto kali, wizara ya afya ya Japani inapendekeza kuvua barakoa yako unapokuwa angalau umbali wa mita 2 kutoka mtu mwingine.

Mtaalamu wa magonjwa ambukizi Sakamoto Fumie kutoka Hospitali ya Kimataifa ya St. Luke nchini Japani anasema watu hawahitaji kuvaa barakoa wakati wote, isipokuwa inapokuwa na ulazima. Sakamoto anasema kuendelea kuvaa mara kwa mara barakoa kunasababisha hatari ya kupata ugonjwa wa kuzimia kutokana na joto kali.

Kuchagua aina ya kitambaa cha Barakoa pia ni muhimu, hususan katika miezi ya joto. Watu wengi wanatengeneza barakoa zao kwa vitambaa vya aina mbalimbali. Shirika la Afya Duniani linatoa taarifa juu ya ufanisi wa aina mbalimbali za vitambaa vya barakoa, kwa misingi ya uwezo wa kupumua vizuri na ubora wa kuchuja, ambapo ni uwezo wa kitambaa kuchuja vitone. Shirika hilo linasema nailoni ina ubora wa hali ya juu wa kuchuja lakini hutoa uwezo wa kupumua vizuri ni mdogo. Pamba inayotumika kwenye bendeji ni rahisi kupumua lakini ina ubora mdogo wa kuchuja. WHO inasema pamba inapaswa kuambatanishwa na aina nyingine ya kitambaa ili kuongeza ufanisi wake wa kuchuja.

Kundi moja la madaktari bingwa wa watoto linasema barakoa hazipaswi kuvaliwa na watoto walio chini ya miaka miwili kwa sababu ya hatari ya kushindwa kupumua.

Sakamoto wa Hospitali ya Kimataifa ya St. Luke anasema si tu kuvaa barakoa, bali pia ni muhimu kuchukua hatua za msingi za kujilinda kama vile kusafisha mikono na kuepuka kile kinachoitwa “C tatu” ambazo ni “Closed spaces” yaani maeneo yasiyo na nafasi kubwa, “Clowded places” yaani maeneo yenye watu wengi na “Close contact” yaani kukaa karibu.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Julai 8. Pia inapatikana katika tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK World JAPAN.

56. Unaoshaje barakoa za vitambaa?

Jibu. Kitu cha msingi ni kutozisugua.
Wizara ya afya ya Japani inasema kwanza unapaswa kuziloeka barakoa za vitambaa kwenye beseni lenye maji na sabuni kwa takribani dakika 10. Kiwango cha sabuni kinategemea na aina ya sabuni hiyo lakini kawaida, unaweza kuhitaji gramu 0.7, ama takribani nusu ya kijiko kwa kila lita mbili za maji. Kisha osha barakoa kwa kugandamiza kidogo na mikono yako. Suuza vizuri barakoa kwa maji kwenye beseni.

Kama unataka kutumia mashine ya kufulia, weka barakoa kwenye wavu ambao una ukubwa sawa na barakoa. Kausha maji yoyote yaliyozidi kwenye barakoa kwa kutumia taulo safi na anika kwenye kivuli.

Wizara hiyo imesema ni bora kuosha barakoa mara moja kwa siku na kushauri kutozitumia tena ikiwa hazitarudi katika umbo lake.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Julai 6 na inaweza kuthibitishwa kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK WORLD Japan.

55. Wataalam wa afya wanavalia barakoa. Lakini nasikia habari za wauguzi na madaktari kuambukizwa virusi vya korona. Je, barakoa hakika zinafaa katika kuzuia maambukizi?

Haijabainika ikiwa barakoa zinaweza kuzuia maambukizi. Hata hivyo, barakoa zinazovaliwa sana na watu wengi mara moja na kisha kutupwa hazizuii virusi kikamilifu, kwa hivyo kufaa kwake katika kuzuia maambukizi kunaaminika kuwa na ukomo hata ikiwa zinafaa.

Katika mazingira ya afya, wafanyakazi huvaa barakoa sambamba na hatua zingine za kujikinga zinazotokana na ufahamu wa kitaalam. Hata hivyo, inasemekana kwamba barakoa pekee hazitoi kinga kubwa dhidi ya maambukizi.

Barakoa aina ya N95 ni barakoa za kitabibu zenye utendaji kazi wa kiwango cha juu ambazo wafanyakazi wengi wa afya huzivaa kwenye chumba cha kulaza wagonjwa mahututi. Zinaweza kuchuja virusi lakini zinaweza zikafanya iwe vigumu kwa aliyezivaa kupumua.

Kwa matumizi sahihi ya barakoa za N95, ni muhimu kujifunza awali namna sahihi ya kuzivaa na kuzitumia. Haijalishi ni aina gani ya barakoa unayovaa, kushika uso wako kabla ya kuitakasa mikono yako kunaongeza athari ya kuambukizwa.

Kwa upande mwingine, zikivaliwa na mtu aliyeambukizwa virusi vya korona, barakoa zinasemekana kupunguza kwa kiasi kikubwa athari ya mtu kueneza virusi hivyo kwa wengine.

Hadi sasa, inafahamika kuwa virusi vya korona kimsingi vinaambukizwa kupitia vitone vinavyotokana na upumuaji. Pia inafahamika kwamba mtu aliyeambukizwa virusi vya korona hutoa kiasi kikubwa cha virusi hivyo kuanzia takribani siku mbili kabla ya kuanza kuonyesha dalili, hadi mara tu baada ya kuonyesha dalili za virusi hivyo.

Inasemekana kuwa uvaaji wa barakoa huzuia kwa kiasi kikubwa kutawanyika kwa vitone vinavyotokana na kukohoa na kupiga chafya, pamoja na vitone vidogo zaidi ambavyo ni chembe ndogo sana zinazotolewa wakati watu wanapozungumza.

Omi Shigeru ni naibu mkuu wa jopo la wataalam la serikali ya Japani. Akiongea na waandishi wa habari mwezi Mei mwaka huu, Omi alisema anataka kila mmoja bila kujali ikiwa wana dalili za maambukizi au la, kuvaa barakoa ili kupunguza athari ya kuenea kwa virusi hivyo.

Alisema ingawa pamekuwepo na maoni mbalimbali kuhusiana na matumizi ya barakoa, makubaliano ya jumla yanaafikiwa katika mataifa mengine na pia kwenye Shirika la Afya Duniani.

Usahihi wa taarifa hii ni wa kufikia hadi Julai 3.

54. Kuna uhusiano wowote kati ya iwapo mtu ana kingamwili ama la na iwapo mtu huyo kwa sasa ana virusi vya korona au la kwenye kipimo cha PCR?

Kwanza tutupie macho juu ya kipimo cha kingamwili. Upimaji kingamwili hufanyika kubaini iwapo mtu anayo aina ya protini iitwayo “kingamwili,” zinazotengenezwa kwa seli za kujikinga kwenye damu pale zinapopambana na virusi vinavyoathiri damu. Katika upimaji, matone machache ya damu huchukuliwa, na sampuli hiyo huwekwa kwenye kifaa cha kupimia. Hata hivyo, unapaswa kufahamu kwamba kutengenezwa kwa kingamwili huchukua muda na haziwezi kugunduliwa mapema baada ya kuambukizwa.

Taasisi ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi ya Japani ilichunguza sampuli za damu za wale walioambukizwa virusi vya korona kwa kutumia vifaa vya kupimia kingamwili vinavyouzwa madukani. Walibaini kuwa katika sampuli nyingi ilikuwa si chini ya wiki mbili baada ya mhusika kuanza kuonyesha dalili za kuambukizwa ndipo kingamwili zilibainika.

Sasa hebu tuangazie kipimo cha PCR. Kipimo hiki kinabaini iwapo umeambukiwa ama la. Iwapo kipimo kitasema umeambukizwa, hiyo itamaanisha una virusi hivyo mwilini mwako. Hata hivyo, mara nyingi hutokea kwamba kingamwili huwa hazibainiki kwa kuwa huwa hazijatengenezwa bado. Kwa upande mwingine, kipimo cha PCR kikisema hakuna virusi, hiyo kwa kiasi kikubwa humaanisha hujaambukizwa bado. Ama inaweza kumaanisha kwamba virusi vimeondoshwa kutoka mwilini mwako baada ya kuwa uliambukizwa. Kwa kisa cha virusi kuondolewa mwilini kuna uwezekano wa kubainika kuwepo kwa kingamwili mwilini mwako katika kipimo cha kingamwili.

Wakati huo huo, aina mpya ya kipimo imekuwa ikitengenezwa. Aina hii mpya ya kipimo inatarajiwa kubaini aina nyingine ya kingamwili inayoafahamika kuonekana kwenye damu, mara tu baada ya mwili kuambukizwa virusi. Matumaini yapo juu kwamba kitakapotumika, huenda kikachukua nafasi ya kipimo cha PCR. Hata hivyo, kipimo hicho kinakabiliwa na vikwazo kidogo vya kutatua kwa upande wa usahihi.

Taarifa hii ni sahihi hadi Julai 2.

52. Mbu wanaweza kueneza virusi vya korona?

Tovuti ya Shirika la Afya Duniani WHO imeelezea wazi kuwa “virusi vipya vya korona haviwezi kuenezwa na mbu.” Inaelezea kuwa hadi leo, kumekuwa hakuna taarifa ama ushahidi unaoashiria kuwa virusi vinaweza kuenezwa na mbu.

Shirika hilo la afya duniani linasema “Virusi vipya vya korona ni virusi vya mfumo wa upumuaji ambavyo vinasambaa hasa kupitia matone madogo yanayotoka pale mtu aliyeathirika anapokohoa ama kupiga chafya, ama kupitia matone madogo ya mate ama mafua yanayotoka puani.”

Shirika hilo linashauri, “Ili kujilinda, safisha mikono yako mara kwa mara kwa kutumia dawa za kuua vijidudu ama safisha kwa maji safi yanayotiririka na sabuni. Pia epuka kuwa karibu na yeyote ambaye anakohoa ama kupiga chafya.”

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Juni 30 na inapatikana kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK WORLD JAPAN.

49. Nimesikia kwamba mafua ya Kihispania yalitokea katika mawimbi matatu. Tafadhali nisimulie mengi zaidi kuhusiana na mafua hayo.

Janga la mafua la mwaka 1918 linalofahamika pia kama mafua ya Kihispania lilisababishwa na aina mpya ya virusi vya mafua. Shirika la Afya Duniani, WHO linasema takriban watu milioni 500 au takriban robo ya idadi ya watu duniani wakati huo waliambukizwa mafua hayo na milioni 40 kuaga dunia.

Mafua ya Kihispania kwanza yalienea duniani kuanzia msimu wa machipuo wa mwaka 1918 na kupungua wakati wa msimu wa joto. Lakini wimbi la pili la maambukizi lilitokea wakati wa msimu wa pukutizi mwaka huo wa 1918 na kisha wimbi la tatu kujiri mwanzoni mwa mwaka 1919.

Wimbi la pili linaaminika kusababisha vifo vya watu wengi zaidi vikiwa ni vya watu wasiopungua milioni 20 kote duniani.

Nchini Japani, mlipuko wa mafua ya Kihispania ulitokea katika mawimbi matatu kati ya msimu wa pukutizi mwaka 1918 na msimu wa machipuo mwaka 1921. Rekodi zilizohifadhiwa na Wizara ya Mambo ya Ndani wakati huo zinaonyesha kuwa kwa jumla, takriban watu milioni 23.8 waliambukizwa mafua hayo na watu 390,000 kuaga dunia.

Japani ilikumbwa na mlipuko mkubwa wakati wa wimbi la kwanza lililoanza msimu wa pukutizi mwaka 1918 huku watu milioni 21.2 wakiambukizwa mafua hayo na watu 260,000 kufariki. Wimbi la pili lililoanza msimu wa pukutizi mwaka 1919 lilisababisha mlipuko mdogo huku visa milioni 2.4 vya maambukizi vikiripotiwa na watu 130,000 kufariki. Hata hivyo, kiwango cha waliofariki kilikuwa juu zaidi wakati wa wimbi la pili.


Hii leo, wataalam wanaonya kuwa virusi vipya vya korona huenda pia vikawa na wimbi la pili na la tatu sawia tu na mafua ya Kihispania.

Usahihi wa taarifa hii wa kufikia Juni 24 mwaka huu.

48. Ni katika mazingira gani ambapo virusi vipya vya korona huzaliana tena? Je, huzaliana tu vikiwa ndani ya miili yetu?

Tulimuuliza Profesa Kunishima Hiroyuki kutoka Shule ya Tiba ya Chuo Kikuu cha Mtakatifu Marianna ambaye ni mtaalam wa magonjwa ambukizi. Kunishima anasema virusi na bakteria ni baadhi ya vijidudu vidogo sana au vidubini. vinavyosababisha magonjwa.

Bakteria ni viumbehai vya tangu zamani sana vitokanavyo na seli moja. Vinaweza kujizalisha vyenyewe.

Virusi ni vidogo zaidi kuliko bakteria. Vinahusisha jeni au asidi za kiini cha chembe na kufunikwa kwa kiambata cha ulinzi lakini havina seli. Virusi haviwezi kujizalisha vyenyewe. Vinaweza kufanya hivyo tu vikiwa ndani ya seli hai za binadamu au wanyama walioambukizwa.

Hii inamaanisha kuwa virusi vipya vya korona haviwezi kuzaliana kwenye kuta ama sehemu za juu za vitu vinavyovichafua. Lakini tunatambua kuwa virusi hudumisha uwezo wake wa kuambukiza kwenye maeneo kama hayo kwa muda fulani.

Profesa Kunishima anasema kwamba huwa tuna kawaida ya kushika maeneo kama hayo yenye virusi, ikiwemo vitasa vya milango na papi za ngazi, tunapokuwa nje ya makazi yetu. Anasema ili kuzuia maambukizi unapaswa kusafisha mikono yako kwa maji safi yanayotiririka ama kwa kutumia dawa za kuulia vijidudu pale unaporejea nyumbani ama kuwasili ofisini au kabla ya kula.

Taarifa hii ni sahihi kabla ya Juni 24.

47. Unaweza kuambukizwa kwa kubadilishana fedha?

Profesa Mikamo Hiroshige wa Chuo Kikuu cha Tiba cha Aichi ambaye amebobea katika kudhibiti maambukizi anasema hali inategemea uwingi wa virusi. Anasema lakini ikiwa mtu ana virusi kwenye mikono yake na wakazigusa noti ama sarafu , ni bora kudhani kwamba virusi vitabaki kwenye fedha hizo kwa muda kidogo. Ili kuzuia maambukizi, ni muhimu kuosha mikono yako na sabuni ama dawa ya kuua vijidudu kabla ya kugusa mdomo ama pua yako. Profesa pia anashauri hatua hizi baada ya kugusa chochote ambacho umenunua.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Juni 23 na inapatikana kwenye tovuti na mitandao ya kijamii ya NHK WORLD JAPAN.

46. Ni kwa muda gani virusi vipya vya korona vinaweza vikaishi kwenye uso wa vitu?

Ripoti moja iliyotayarishwa na watafiti katika Taasisi ya Taifa ya Afya nchini Marekani na mashirika mengine, inasema virusi hivyo kwa kiasi kikubwa hutoweka kutoka kwenye uso wa vitu kadiri muda unavyosonga. Kulingana nao, virusi hivyo havikutambuliwa kwenye shaba nyekundu baada ya saa nne, na wala havikutambuliwa kwenye kadibodi baada ya saa 24.

Hata hivyo, virusi hivyo vilisalia kwenye uso wa plastiki kwa saa 72, na kwenye uso wa chuma cha pua kwa saa 48.

Usahihi wa taarifa hii ni wa kufikia Juni 22.

45. Ni kitu gani kitatokea kwa virusi vitakapogandishwa?

Tulizungumza na Sugawara Erisa, profesa katika Shule ya Uzamili ya Chuo Kikuu cha huduma ya Afya cha Tokyo ambaye amebobea kwenye uzuiaji wa maambukizi.

Wakati kukiwa bado kuna sintofahamu nyingi kuhusiana na tabia za virusi vipya vya korona, tafiti za kimataifa juu ya virusi vya SARS, aina nyingine inayofanana na virusi vya korona, tayari zimefanyika.

Kwa mujibu wa tafiti hizo, wakati virusi vya SARS viliuliwa pale vilipowekwa kwenye mazingira yenye joto kubwa kidogo la nyuzi 56 za selsiasi, kirusi hicho kiliweza kuishi katika nyuzijoto ya chini ya chini ya sifuri ya hasi 80 kwa takribani wiki tatu.

Utafiti huo unaashiria kuwa virusi vipya vya korona huenda vikawa dhaifu dhidi ya joto huku vikiwa na nguvu kidogo katika halijoto ya chini.

Sugawara anasema, ikiwa kwa mfano, virusi vipya vya korona vinapatikana katika sehemu ya juu ya mbogamboga na matunda, vinadhaniwa kuishi katika friji kwa muda mrefu. Hivyo watu wanashauriwa kuua vijidudu nje ya vifaa vya kufungashia kabla ya kuviweka kwenye friji, na kunawa mikono yao vizuri kabla na baada ya kupika. Sugawara anasema bidhaa nyingi zinaweza kuliwa salama ikiwa zitapashwa moto.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Juni 19.

44. Ikiwa chakula kilichofungashwa kimeathirika na virusi, je, tunaweza kuvitokomeza virusi kwa kukipasha moto chakula hicho kwenye oveni ya mikrowevu?

Oveni za mikrowevu hutumia mawimbi ya sumaku umeme kuzungusha molekuli za maji ndani ya chakula ili kukipasha moto.

Profesa Sugawara Erisa wa Shule ya Uzamili ya Chuo Kikuu cha Huduma ya afya cha Tokyo, mtaalam wa kuzuia maambukizi, anasema chakula chenyewe ni salama kukila ikiwa kimepashwa moto vya kutosha ndani ya oveni ya mikrowevu. Lakini anagusia kuwa hakuna ushahidi kwamba oveni hupasha moto sehemu ya juu ya kifungasho cha chakula kiasi cha kutoka kusababisha virusi kwenye kifungasho hicho kupoteza uwezo wa kuambukiza.

Sugawara anasema ni muhimu kunawa mikono mara kwa mara kabla na baada ya kupika na kula.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Juni 18.

43. Ni kweli kwamba nchi ambazo zimetumia chanjo ya kifua kikuu ya BCG zina vifo vichache vya virusi vya korona?

Chanjo ya BCG imetengenezwa kutokana na uzao dhaifu wa bakteria wanaosababisha kifua kikuu kwa ng’ombe na ni sawa na bakteria wanaosababisha ugonjwa huo kwa binadamu. Nchini Japani, watoto wote wanapata chanjo hiyo ya kifua kikuu kabla ya kutimiza mwaka mmoja. Sera za chanjo ya BCG zinatofautiana nchi na maeneo. Marekani na Italia ni miongoni mwa nchi zisizo na mpango wa kila mtu wa chanjo ya BCG.

Baadhi ya watafiti nje ya Japani wamedokeza kwamba maeneo yenye utaratibu wa kutoa chanjo ya BCG yana vifo vichache vya virusi vya korona. Majaribio ya kitabibu yanaendelea Australia na Uholanzi kutafiti ikiwa chanjo ya BCG inahusiana na uzuiaji wa maambukizi ya virusi vya korona na kuzuia dalili kuwa kali.

Aprili 3 mwaka huu, Jumuiya ya Japani ya Masuala ya Chanjo iliwasilisha mtazamo wake kuhusiana na suala hilo.

Jumuiya hiyo inasema ufanisi wa chanjo ya BCG dhidi ya virusi vya korona bado haujathibitishwa kisayansi na kwamba kwa wakati huu haipendekezi chanjo hiyo kama njia ya kuzuia virusi hivyo.

Jumuiya hiyo inasema baadhi ya watu wa kizazi cha nyuma kidogo ambao hawakupata chanjo hiyo wanaomba kupatiwa sasa kama ulinzi dhidi ya virusi vya korona. Lakini jumuiya hiyo inasema BCG ni chanjo kwa ajili ya watoto wachanga na usalama na ufanisi wake kwa wazee haujathibitishwa.

Aidha jumuiya hiyo pia inasema kuna haja ya kuepuka ongezeko la matumizi ya BCG nje ya maombi yaliyokusudiwa, ambayo yanaweza kuvuruga usambazaji thabiti wa chanjo hiyo kwa watoto wachanga.

Taarifa hii ni sahihi kufikia Juni 17.

42. “Ni kitu gani kitatokea kwa virusi kwenye ngozi ya binadamu?” na “Je virusi vinakaa kwenye mwili bila ya mtu kuonyesha dalili?”

Tulimuuliza Profesa Kunishima Hiroyuki ambaye amebobea katika magonjwa ya kuambukiza kwenye Shule ya Kitabibu ya Chuo Kikuu cha St. Marianna. Anasema virusi haviwezi kuongezeka isipokuwa vikiingia na kuathiri seli za mnyama aliye hai.

Virusi vya korona vinafahamika hasa kuathiri watu kupitia tando zilizo kwenye pua ama midomo yao na kuzaliana katika seli za koo, mapafu ama maeneo mengine ya wanyama. Virusi haviwezi kuzaliana ikiwa vipo juu ya mkono ama mguu wa mtu.

Lakini ikiwa mtu ana virusi kwenye mikono yake na kisha akagusa macho, pua ama mdomo wake, wanaweza kuathirika. Virusi kwenye ngozi ya mtu vinaweza kuondolewa kwa sabuni, hivyo watu wanapaswa kuwa safi kwa kuosha vizuri mikono yao ama kwa kutumia vitakasa kama vile vya kileo kabla ya kugusa nyuso zao.

Baadhi ya virusi kama vile vinavyosababisha ugonjwa wa malengelenge ya neva ngozini vinabaki kwenye mwili wa binadamu hata baada ya mtu huyo kupona. Lakini kawaida, virusi vya korona ni tofauti, hivyo ikiwa mtu ameambukizwa na kuonyesha dalili, hatimaye, mfumo wa kinga ya mwili wa mtu huyo unafanya kazi na virusi vitatoweka mwilini.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Juni 15.

41. Je, miali ya urujuani ya jua ama gesi ya ozoni kwa ajili ya kuua bakteria ina ufanisi wa kuua virusi vipya vya korona?

Tulizungumza na Profesa Ohge Hiroki kutoka Chuo Kikuu cha Hiroshima ambaye ni mtaalam wa magonjwa ya kuambukiza. Ohge anasema kuna matarajio kuwa miali mikali ya urujuani kwa muda mrefu maalum dhidi ya virusi na bakteria, ambayo inasababisha magonjwa mengi ni njia yenye ufanisi katika kupunguza uwezo wao wa kuambukiza.

Kuna matarajio kuwa vifaa tayari vinavyotumika ambavyo vinatoa miali mikali ya urujuani vitakuwa vinafaa kukabiliana na virusi vipya vya korona. Kifaa kimoja kinachotumika kwenye hospitali ya Chuo Kikuu cha Hiroshima, katika vyumba vya hospitali vya wagonjwa wa virusi vya korona ambao wameruhusiwa kuondoka, ambapo miali hiyo inatolewa kwenye chumba chote.

Katika hatua nyingine, mwanga wa jua unaaminika kuwa haufai katika kuua virusi kama hivyo ambavyo vinaweza kuangamizwa na vifaa vilivyotajwa awali. Wakati mwanga wa jua ni miali ya urujuani, mwanga huo una miali ya nguvu za aina mbalimbali na haina nguvu kama miali inayotengenezwa na vifaa hivyo.

Kuhusiana na gesi ya ozoni, kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa mwezi Mei na kikundi cha watafiti kutoka vyuo vikuu nchini Japani, walibaini kuwa uwezo wa kuambukiza wa virusi vipya vya korona ulipungua baada ya virusi hivyo kuwekwa kwenye gesi ya ozoni kwa takribani saa moja. Ohge anasema gesi ya ozoni iliyotumika kwa ajili ya jaribio hilo ilikuwa na ujazo wa kati ya 1ppm na 6ppm ambayo inadhaniwa kuwa ina madhara kwa binadamu.

Vifaa vinavyotumia gesi ya ozoni kwa ajili ya kuua bakteria na kuondoa harufu ambavyo vinauzwa kwa matumizi ya kawaida, havitumii gesi ya ozoni katika ujazo mkubwa kama huo. Lakini bado haijathibitishwa ikiwa gesi ya ozoni kwenye ujazo mdogo kama huo inafaa katika kupambana na virusi vipya vya korona.

Shirika la Japani la Masuala ya Mlaji linatoa wito kwa watumiaji kuthibitisha na makampuni ya utengenezaji ikiwa wana msingi wa kisayansi wa kudai kuwa bidhaa zao, ikiwa ni pamoja na zile zinazotumia gesi ya ozoni, zinafaa kupambana na virusi vya korona.

40. Je, ni tahadhari zipi zinazopaswa kuchukuliwa wakati unapovaa barakoa wakati wa msimu wa joto?

Ncha ya Kaskazini mwa Dunia inakaribia kushuhudia joto kali la msimu wa joto. Wizara ya Afya, Kazi na Ustawi nchini Japani inasema tahadhari zaidi inapaswa kuchukuliwa ili kuepuka kukumbwa na ugonjwa wa kuzirai unaosababishwa na joto kali mwaka huu, kwani watu wengi wanavaa barakoa kama hatua ya kuepukana na maambukizi ya virusi vya korona.

Wizara hiyo inawashauri watu kuvua barakoa zao ikiwa wamedumisha hali itakikanayo ya kutokaribiana na watu, ambayo inapaswa kuwa mita zisizopungua mbili. Kadhalika wizara hiyo inatoa wito kwa watu kuepukana na kazi za sulubu au kufanya mazoezi wakati wakiwa wamevalia barakoa. Isitoshe, wizara hiyo inawashauri watu kunywa maji mara kwa mara hata ikiwa hawahisi kiu.

Yokobori Shoji ni Profesa wa Shule ya Uzamili ya Tiba ya Chuo Kikuu cha Nippon aliyetaalamika kuhusiana na masuala ya ugonjwa wa kuzirai unaosababishwa na joto kali. Anasema si lazima kwamba uvaaji wa barakoa unaweza ukamfanya mtu kuwa katika hatari ya kukumbwa na ugonjwa huo. Lakini anasema uvaaji wa barakoa hufanya iwe vigumu kwa mtu kupumua. Kuna takwimu inayoonyesha kuwa mapigo ya moyo na kiwango cha kupumua viliongezeka kwa asilimia 10, wakati watu walipovalia barakoa. Profesa Yokobori anasema mzigo wa ziada wa kufanya mazoezi au ongezeko la halijoto vinaongeza athari ya kukumbwa na ugonjwa wa kuzirai unaosababishwa na joto kali.

Kulingana na Profesa Yokobori, ni muhimu kuzuia uenezaji wa virusi vya korona kupitia vitone vinavyosalia hewani, lakini wazee au watu wanaoishi peke yao, wanapaswa hasa kutahadhari zaidi inapokuja kwa swala la ugonjwa huo. Wanapokuwa nje, Profesa Yokobori anawashauri watu kuvua barakoa zao na kupumzikia katika maeneo yasiyokuwa na misongamano ya watu, kama vile chini ya mti. Aidha anapendekeza ubadilishaji wa barakoa baada ya kutokwa na jasho, kwani hewa kidogo hupitia kwenye unyevuunyevu wa barakoa.

Taarifa iliyowasilishwa kwenye ripoti hii ni ya hadi kufikia Juni 11.

39. Je, tunapaswa kuwa waangalifu kuhusiana na nini wakati tunapotumia viyoyozi?

Wakati msimu wa joto unapoanza kwenye ncha ya kaskazini mwa dunia, huenda baadhi ya watu wakawa na wasiwasi kuhusiana na upitishaji wa hewa safi katika sehemu ambazo kiyoyozi kinatumiwa kupoesha hewa. Viyoyozi vingi vya kutumiwa nyumbani huzungusha tena hewa iliyo ndani ya nyumba na havitekelezi majukumu ya upitishaji hewa safi. Kuna uwezekano watu wengi hufunga madirisha ya nyumba zao wakati wanapotumia viyoyozi.

Yamamoto Yoshihide ni Profesa mshiriki katika Chuo Kikuu cha Ufundi Anuwai cha Tokyo na pia mwanachama wa Taasisi ya Usanifu Majengo nchini Japani. Nyanja yake ya utaalam inajumuisha upitishaji wa hewa safi kwenye majengo. Profesa Yamamoto anapendekeza kutumiwa kwa pamoja kwa viyoyozi na upitishaji hewa safi.

Katika maeneo yenye misimu minne, Profesa Yamamoto anapendekeza kufunguliwa kwa madirisha ili kwa kiasi fulani kuruhusu hewa safi kutoka nje wakati unapotumia viyoyozi mwanzoni mwa msimu wa joto, wakati joto si kali sana. Wakati chumba chako kinapokuwa na joto kali, poesha hewa hiyo kwa kufunga madirisha kwa muda mfupi au kuyafungua lakini uache nafasi ndogo tu ya kupitisha hewa safi.

Katikati ya msimu wa joto wakati athari ya ugonjwa wa kuzirai unaosababishwa na joto kali inapoongezeka, Profesa Yamamoto anapendekeza kutumiwa mno kwa feni za kuingiza hewa safi kwenye nyumba kama zitumiwazo chooni au jikoni, badala ya kufungua madirisha. Hali sawia pia inapaswa kutumika katika maeneo ya kitropiki.

Makazi mengi yamesanifiwa kupitisha hewa safi kutoka nje wakati feni za kupitisha hewa safi zinapotumika. Hii itaongeza mtiririko wa hewa kati ya ndani na nje ya jengo hata ikiwa madirisha yamefungwa. Tafadhali tafuta ushauri wa wataalam ili kubaini namna upitishaji wa hewa safi unavyofanya kazi nyumbani kwako.

Usahihi wa taarifa hii ni wa kufikia Juni 10.

38. Maswali kutoka kwa wakazi wa kigeni nchini Japani -3-

Swali la kwanza ni “ikiwa nitakumbwa au kushuhudia unyanyapaa unaohusiana na COVID-19, nani ninapaswa kuwasiliana naye?”

Tafadhali wasiliana na kituo cha ushauri cha lugha mbalimbali, cha Yorisoi Hotline, kupitia tovuti yake:
https://www.since2011.net/yorisoi/n2/

Nambari yake ya simu bure ni 0120-279-338.
0120-279-226 kwa mikoa ya Iwate, Miyagi, Fukushima.
Au ukurasa wake wa Facebook ni:
https://www.facebook.com/yorisoi2foreign

Swali la pili ni: “ninanyanyaswa na mwenza wangu, nizungumze na nani kwa usaidizi?”

Waathiriwa wa unyanyasaji wa majumbani wana vyanzo vingi vya msaada, ikiwa pamoja na kutafuta ushauri kwa njia ya simu na mitandao ya kijamii. Pia unaweza kupata huduma ya mtandaoni iliyofasiriwa na taarifa za makazi ya muda.

■Ushauri kupitia mitandao ya kijamii unapatikana kwa saa 24 katika lugha 11. Tafadhali tembelea
https://soudanplus.jp/language .

■Kituo cha Utoaji Ushauri na Usaidizi kwa Dhuluma za Wanandoa
Namba ya simu ni 0570-0-55210 kwa lugha ya Kijapani pekee. Kinakuunganisha na kituo cha ushauri cha jirani nawe.

■Domestic Violence Hotline Plus:
Tafadhali piga 0120-279-889 lakini Kijapani pekee.

Swali la tatu na la mwisho ni: “Nina ujauzito, ninapaswa kuwa na mashaka?”

Wakati ushahidi unaashiria kwamba wajawazito hawapo kwenye hatari kubwa ya kuugua mno kuliko watu wazima wenye afya, maambukizi ya virusi vya korona wakati wa miezi mitatu ya mwishoni ya ujauzito yanaweza kuwa na maendeleo na hali mbaya sawa na wanawake wasio wajawazito. Takwimu zinaonesha Kuwa huhitajiki kuwa na wasiwasi kupindukia kuhusu COVID-19 wakati wa ujauzito. Lakini unapaswa kuendelea kuchukua tahadhari kama vile kuepuka mikusanyiko, kunawa mikono mara kwa mara, na kuzingatia afya yako ya kila siku ya mwili na hisia.

Kwa mengi zaidi, tembelea linki ifuatayo ya lugha mbalimbali:
https://share.or.jp/english/news/for_pregnant_womencovid-19_countermeasures.html

Bonyeza linki ifuatayo kwa kipindi chetu cha runinga cha
Heart Net TV kwa Kijapani rahisi:
https://www.nhk.or.jp/heart-net/article/339

37. Maswali kutoka kwa wakazi wa kigeni nchini Japani -2-

Nchini Japani, raia wa kigeni wanaongezewa muda wa miezi mitatu kutuma maombi ya kupewa viza mpya, kwa ajili ya mabadiliko ya hadhi ya ukazi na kuongezwa muda wa kuishi nchini Japani. Swali la kwanza wanauliza, “Naweza nikaendelea kufanya kazi nchini Japani kwa muda wa nyongeza ya miezi mitatu kuishi nchini Japani hata ikiwa muda wa viza yangu umekamilika?”

Jibu la swali hilo ni “Ndio.” Unaweza ukaendelea kufanya kazi chini ya masharti fulani. Shirika la Huduma za Uhamiaji liliitaarifu NHK World Juni 2 kwamba wakati wa kipindi hiki maalum cha kuongeza muda, una idhini ya kufanya kazi chini ya masharti sawa ya hadhi yako ya ukazi ya awali. Hata hivyo, ikiwa utahitaji kubadilisha masharti yoyote ikiwa ni pamoja na aina ya kazi na mwajiri, ni sharti kwanza utafute ushauri kutoka kwa Shirika la Huduma za Uhamiaji.

Swali linalofuata linauliza, “Je, naweza nikapoteza hadhi yangu ya ukazi ya kufanya kazi au kuwa mwanafunzi nikiwa na kibali cha muda cha kufanya kazi ikiwa siwezi nikafanya kazi au kusoma?”

Jibu la swali hilo ni “Hapana.” Hadhi yako haitafutwa ikiwa umeshindwa kufanya kazi au kusoma kutokana na athari ya virusi vya korona. Lakini ni sharti uthibitishe kuwa umeathiriwa na mojawapo wa mambo yafuatayo:

1. Mwajiri wako au kampuni yako sharti isitishe operesheni zake za kibiashara kwa muda.

2. Unapaswa kuwa umestaafu na unatafuta ajira kupitia mtandaoni, au una kazi unayotarajia kuanza kufanya lakini huwezi ukafika kwenye kampuni husika.

3. Ikiwa taasisi ya elimu ulioandikishwa imefungwa, ikiwa ni pamoja na hali ambapo taasisi ambayo umepangiwa kujiunga nayo imefungwa.

4. Ikiwa taasisi ambayo uliandikishwa itafungwa na haiwezi ikatimiza taratibu zinazohitajika kwa ajili ya wewe kujiunga na taasisi nyingine.

5. Ikiwa kipindi cha kulazwa kwako hospitalini kutokana na ugonjwa vikiwemo virusi vipya vya korona kitakuwa kirefu na kukulazimu kuchukua likizo.

Ikiwa unataka maelezo zaidi, tafadhali itazame tovuti ifuatayo, lakini maelezo yametolewa kwa lugha ya Kijapani pekee, na ikiwa utakuwa na tashwishi kuhusiana na suala lolote unaweza ukathibitisha suala hilo kwa kuwasiliana na Shirika la Huduma za Uhamiaji. Tovuti yenyewe ni http:www.moj.go.jp/content/001319592

Usahihi wa taarifa hii ni wa kufikia hadi Juni 5.

36. Maswali kutoka kwa wakazi wa kigeni nchini Japani -1-

Katika swali la kwanza wanauliza, ‘Nini kinafanyika ikiwa hadhi yangu ya ukazi ya “mgeni wa muda” itamalizika lakini siwezi nikarejea nchini mwangu?’

Katika hali kama hiyo, utaongezewa muda wa siku 90. Ili kupata maelezo ya kina kuhusiana na suala hilo, tafadhali tembelea tovuti ya Wizara ya Sheria ambayo ni:
http://www.moj.go.jp/content/001316293

Katika swali la pili wanauliza, “ikiwa muda wa viza yangu utamalizika kati ya mwezi Machi na Julai mwaka huu, je, muda wake wa matumizi utaongezwa moja kwa moja kwa kipindi kingine cha miezi mitatu?”

Jibu la swali hilo ni la hasha. Lakini raia wa kigeni wanaongezewa muda wa miezi mitatu kwa maombi ya kubadilishiwa upya viza, inapokuja kwa suala la kubadilisha hadhi ya ukazi na kuongezwa kwa muda wa kukaa nchini Japani. Hatua hiyo inalenga kusaidia kupunguza msongamano kwenye vituo vya uhamiaji. Hatua hii ikiwa inafaa tu kwa watu ambao muda wa viza zao unamalizika kati ya mwezi Machi na Julai mwaka huu wa 2020, inatoa nyongeza ya kipindi cha kutuma maombi cha miezi mitatu kutoka tarehe ya kumalizika kwa kipindi cha kuishi nchini Japani. Yaani, ikiwa muda wa kutumika kwa viza yako utamalizika Mei 11, utakuwa na hadi Agosti 11 kutuma maombi ya kuongezewa muda.

Ili kupata taarifa katika lugha mbalimbali, tafadhali tembelea tovuti ya Wizara ya Sheria ya Japani ambayo ni:
http://www.moj.go.jp/content/001316300

Usahihi wa taarifa hii ni wa kufikia hadi Juni 4.

Taratibu za kutuma maombi ya viza hubadilika, hasa wakati huu wa janga la virusi vya korona.
Ikizingatiwa hali zinazomkumba mtu binafsi huwa ni tofauti, tafadhali wasiliana na ofisi ya uhamiaji ikiwa una maswali yoyote.

35. Virusi vya korona vinaweza kuwa hai kwenye halijoto ya hadi kiwango gani, na kupika chakula kunaviua?

Watafiti wanasema virusi vipya vya korona vinaweza kuwa hai kwenye nyuzi joto 37 la selisiasi kwa siku moja lakini joto la nyuzi 56 za selisiasi huua virusi hivyo ndani ya dakika 30. Walibaini virusi hivyo vinakuwa havigunduliki ndani ya dakika 5 kwenye joto la nyuzi 70.

Sugawara Erisa wa Jumuiya ya Kupambana na Kuzuia Maambukizi Japani anasema hamna kisa kilichothibitishwa kuhusiana na kula chakula chenye virusi bila kujali iwapo chakula kilipikwa, na kwamba kupika kwa joto stahiki kutaua virusi hivyo.

Taarifa hii ni sahihi hadi kufikia Juni mosi.

30. Je, tunapaswa kufanya nini pale tunaposhindwa kuhisi ladha ya chakula?

Mtaalamu wa magonjwa ambukizi Sakamoto Fumie kutoka Hospitali ya Kimataifa ya Mtakatifu Luka ya hapa Japani, anasema takribani asilimia 30 ya wagonjwa wa virusi vya korona, wamekuwa wakisema kuwa walipatwa na dalili za kushindwa kuhisi ladha au harufu ya chakula.

Kama mtu unapatwa na dalili kama hizo, kuna uwezekano wa kuwa umeathiriwa na virusi hivyo. Lakini dalili kama hizo pia zinaweza kutokea pale unapokuwa umeathiriwa na maradhi mengine. Baada ya dalili hizo kuendelea kwa muda fulani, angalia uwezekano wa kuonana na daktari kama utaendelea kupatwa na homa au kupumua kwa shida.

29. Ni hatari zipi zinaweza kutokana na hatua ya kuwaruhusu watoto kwenda nje kucheza na wenzao wakati huu wa janga la virusi vya korona?

Mtaalamu wa magonjwa ambukizi Sakamoto Fumie kutoka Hospitali ya Kimataifa ya Mtakatifu Luka ya hapa Japani, anasema kuwa baadhi ya shule za msingi na sekondari za chini za hapa Japani, zimefungua tena viwanja vya michezo ili kuwaruhusu watoto kucheza na wenzao wakati huu ambapo shule zimefungwa kwa muda mrefu kote nchini humo.

Anasema wazazi wengi wanaweza kuwa wanajiuliza iwapo hatua hiyo inaweza kusababisha hatari ya maambukizi, japokuwa wanapenda kuwaona watoto wao wakicheza na marafiki zao ili kupunguza msongo wa mawazo unaosababishwa na kukaa ndani kwa siku nyingi.

Sakamoto anasema inaonekana hakuna matatizo makubwa kwa sasa, kama wazazi watazingatia masuala muhimu kama vile kupunguza kadiri iwezekanavyo idadi ya watoto wanaocheza pamoja, na kuhakikisha michezo hiyo inamalizika ndani ya muda mfupi. Pia wanapaswa kuhakikisha watoto wao wananawa mikono yao baada ya kurejea nyumbani.

28. Je, hatari zipi tunakabiliwa nazo tunapokuwa nje tukifanya mazoezi ya kutembea au kukimbia?

Waziri mkuu wa Japani, Abe Shinzo aliusihi umma kujiepusha na shughuli zisizo na umuhimu au zisizo za lazima alipofanya mkutano na wanahabari kutangaza hali ya dharura. Abe pia alisema kuwa sio tatizo kama watu wataenda nje kwa ajili ya mazoezi ya kutembea au kukimbia, jambo ambalo huenda lilitukanganya.

Lakini Mtaalamu wa magonjwa ambukizi Sakamoto Fumie kutoka Hospitali ya Kimataifa ya Mtakatifu Luka anasema kuwa hatupaswi kusahau lengo kuu la tangazo hilo, ambalo ni kuwahamasisha watu kujitenga na wengine kwa kiasi fulani. Kama utakimbia wakati unaongea na mtu mwinginge, vijitone vinaweza kusambaa kati ya mtu mmoja na mwingine, jambo ambalo linapaswa kuepukwa.

Lakini ukikimbia nje ukiwa peke yako na hakuna mtu mwingine karibu yako inafaa zaidi kwa sababu hakuna hatari yoyote kubwa inayoweza kutokea.

27. Je, ni namna gani tunaweza kuwa makini, wakati tunaponunua vitu katika maduka makubwa ya manunuzi?

Mtaalamu wa magonjwa ambukizi Sakamoto Fumie kutoka Hospitali ya Kimataifa ya Mtakatifu Luka ya hapa Japani anasema kuwa tunapaswa kukumbuka kusafisha mikono bila kusahau viganja, ncha za vidole na vifundo vya mikono kwa kutumia vitakasa vilivyowekwa nje kabla ya kuingia ndani ya maduka makubwa ya manunuzi. Anaongeza kuwa, ni vyema kwenda kwenye maduka hayo wakati ambao watu wanakuwa sio wengi.

25. Je, ni kwa namna gani tunaweza kuwa makini na kujiepusha na maambukizi ya virusi vya korona kwenye viwanja vya mchezo wa gofu?

Mtaalamu wa magonjwa ambukizi Sakamoto Fumie, kutoka Hospitali ya Kimataifa ya Mtakatifu Luka jijini Tokyo, anasema kwamba baadhi ya watu wanaweza kudhani kuwa mchezo wa gofu hauna athari ya maambukizi kwa sababu ni mchezo unaochezwa nje. Lakini uchezaji wa mchezo huo unaojumuisha idadi kubwa ya watu ni hatari sana.

Viwanja vya mchezo wa gofu vyenyewe vipo wazi nje na havipo kwenye maeneo yaliyofungwa.

Lakini kutumia vyumba vya kubadilishia nguo ama kupata mlo kwenye viwanja hivyo kunakohusisha watu wengi kunafanya hatari ya maambukizi kuwa kubwa.

Kando na hilo, tunapaswa kuwa makini juu ya hatari ya maambukizi baada ya kugusa nyuso zetu kwa mikono bila kujua, ilhali mikono hiyo imegusa maeneo yanayoguswa na watu wengi wasiofahamika.

24. Je, natakiwa kufanyaje wakati ambapo wale wanaoishi pamoja kwenye “nyumba ya pamoja ama Share House” wameambukizwa virusi vya korona?

Mtaalamu wa magonjwa ambukizi Sakamoto Fumie, kutoka Hospitali ya Kimataifa ya Mtakatifu Luka jijini Tokyo, anasema, katika “Share House” kila mtu ana chumba chake binafsi cha kulala, lakini wapangaji wanatumia jiko na choo kwa pamoja.

Sakamoto anashauri kwamba kitu muhimu cha kufanya ni kuzisafisha sehemu zinazoshikwa mara kwa mara, kama vile mabomba ya maji au swichi za kuwasha taa za umeme kwa kutumia dawa au sabuni zilizozimuliwa, au ikiwa zinapatikana, unaweza ukatumia visafishaji vya kuua viini vya kileo.

23. Je, tunatakiwa kuzingatia mambo gani pale tunapokuwa ndani ya lifti?

Mtaalamu wa magonjwa ambukizi Sakamoto Fumie, kutoka Hospitali ya Kimataifa ya Mtakatifu Luka jijini Tokyo, anasema wengi wetu hatuwezi kupanda ngazi kwenda hadi ghorofa ya 10 au ya 20 kwenye majengo. Tunachoweza kufanya ili kuepuka maambukizi ni kutotumia lifti pamoja na watu wengi, na kuepuka kuongea na watu wengine tunapokuwa ndani ya lifti.

Hatua kama hizo zinaweza kupunguza uwezekano wa kuambukizwa.

Sakamoto anaongeza kuwa ni muhimu kutogusa uso wako kwa kutumia kidole ulichotumia kubonyeza vitufe vya lifti.

Baada ya kushika vitufe hivyo, pia ni muhimu kunawa mikono yako kwa maji na sabuni.

22. Je, ukoje ufanisi wa barakoa zinazotumiwa mara moja tu, na zile zilizotengenezwa kwa pamba ambazo zinaweza kufuliwa na kuvaliwa tena?

Mtaalamu wa magonjwa ambukizi Sakamoto Fumie, kutoka Hospitali ya Kimataifa ya Mtakatifu Luka jijini Tokyo, anasema majaribio mbalimbali yamekuwa yakifanyika juu ya ufanisi wa barakoa katika kukabiliana na virusi vya korona.

Majaribio hayo yanaonyesha kuwa barakoa aina yoyote kati ya hizo mbili ina ufanisi kwa kiasi fulani katika kuzuia matone yasitawanyike pale unapokohoa au kupiga chafya.

Sakamoto anasema hata hivyo, ufanisi wa barakoa yoyote kati ya hizo mbili sio timilifu, na kiwango kidogo cha matone kinaweza kupita na kusambaa.

Kwa hiyo ni vyema kujiepusha kwenda nje pale unapokuwa unakohoa au kupiga chafya.

21. Naomba kujua juu ya wagonjwa wa virusi vya korona ambao hawaonyeshi dalili zozote, licha ya kuwa vipimo vinaonyesha kuwa wameambukizwa virusi hivyo.

Mtaalamu wa magonjwa ambukizi Sakamoto Fumie, kutoka Hospitali ya Kimataifa ya Mtakatifu Luka jijini Tokyo, anasema kuwa baadhi ya wagonjwa wanaweza wakapona bila ya kuonyesha dalili zozote. Timu ya utafiti nchini China iliripoti kuwa nusu ya wagonjwa waliohojiwa hawakuonyesha dalili kabisa au walikuwa na dalili kidogo.

Lakini Sakamoto anasema tunapaswa kuendelea kufuatilia hali za wagonjwa kwa takribani wiki moja kwa sababu baadhi yao hali zao hubadilika taratibu na wanaweza kuugua kupita kiasi.

20. Je, ninaweza kutumia pombe kali kama vitakasa mbadala?

Wizara ya Afya ya Japani imeamua kuruhusu matumizi ya vinywaji vyenye asilimia kubwa ya kileo vitumike kama mbadala wa vitakasa, ili kufidia usambazaji mdogo uliosababishwa na janga la virusi vya korona. Uamuzi huo unalenga kujibu wito kutoka kwenye taasisi za tiba na vituo vya makazi maalum kwa wazee ambavyo vimekuwa vikihangaika kuweza kupata vitakasa vilivyotengenezwa kwa kileo, yaani alcohol-based sanitizers.

Mwezi Aprili, Wizara ya Afya iliviambia vituo hivyo kuwa vinywaji vyenye asilimia kubwa ya kileo, vilivyotengenezwa na makampuni ya vinywaji vinaweza kutumika kama itakuwa vigumu kupata vitakasa maalum.

Kwa hiyo vinywaji vyenye kileo cha kati ya asilimia 70 na 83 vinaweza kutumika. Baadhi ya aina fulani za vodka zipo kwenye kipengele hiki. Maafisa wa Wizara ya Afya pia wanagusia kuwa vinywaji vyenye asilimia zaidi ya hizo vina uwezo mdogo wa kutakasa, kwa hiyo vinapaswa kuchanganywa na maji.

Maafisa wanasisitiza kuwa hiyo ni hatua ya kipekee kwa ajili ya kukabiliana na uhaba wa vitakasa vyenye kileo, hususan katika vituo vya tiba.

Wanatoa wito kwa umma kuendelea kunawa mikono kwa umakini majumbani ili kuzuia kuenea kwa virusi vya korona.

Data hizi ni za hadi tarehe 27, Aprili mwaka huu.

※Msikilizaji kumbuka kwamba kunywa pombe kali ama vitakasa haikusaidii kuzuia maambukizi ya virusi hivyo bali ni kuhatarisha maisha yako. Idara ya Zimamoto ya Tokyo inatoa tahadhari kuwa vitakasa vya kusafisha mikono vinaweza kuwa chanzo cha moto, basi usitumie karibu na moto kwani vinaweza kulipuka na kuleta madhara makubwa.

16. Kwa kiasi gani dawa ya Avigan inafaa katika kutibu virusi vipya vya korona?

Avigan inayofahamika pia kama Favipiravir, ni dawa ya kutibu influenza iliyotengenezwa na kampuni moja ya kutengeneza dawa nchini Japani miaka sita iliyopita.

Kumekuwa na athari za dawa hiyo zilizoripotiwa kwenye majaribio ya wanyama ya maabara, kwa hivyo serikali ya Japani haijaidhinisha matumizi yake kwa baadhi ya watu kama vile kina mama wajawazito. Dawa hiyo sasa itatumika kuwatibu wagonjwa walioambukizwa virusi vipya vya korona katika visa tu vilivyoidhinishwa na serikali.

Kwa wakati huu, hakuna dawa zingine zinazofahamika zinazofaa kwa matibabu ya wagonjwa wa virusi vipya vya korona, lakini Avigan inatarajiwa kuwa bora katika kutibu virusi hivyo, vinavyozaliana kwa hali sawa na virusi vya influenza. Utafiti juu ya athari za dawa hii unafanyika katika maeneo mengi duniani.

Serikali ya China imetangaza matokeo ya utafiti wa kitabibu uliofanyika kwenye taasisi mbili za tiba. Mojawapo ni iliyopo Mjini Shenhzen kwenye Jimbo la Guangdong ukiwahusisha wagonjwa 80.

Wale ambao hawakutibiwa na dawa ya Avigan walichukua nambari ya katikati ya siku 11 kabla ya matokeo ya majaribio yao kubadilika kutoka kuwa chanya hadi kuwa hasi. Nambari ya katikati ya siku kwa wale waliotibiwa na dawa hiyo ilikuwa nne.

Picha za eksirei zilionyesha kuwa hali ya mapafu ya asilimia 62 ya wagonjwa ambao hawakutibiwa na dawa ya Avigan iliimarika, ilhali asilimia 91 ya wale waliotibiwa na dawa hiyo walipata nafuu.

Serikali ya China imetangaza kwamba matokeo hayo yaliichochea kuijumuisha rasmi dawa ya Avigan kama mojawapo wa dawa za kuwatibu wagonjwa walioambukizwa virusi vipya vya korona.

Nchini Japani, utafiti wa kitabibu unaohusisha wagonjwa 80 wenye dalili zisizokuwa kali ama wale wasioonyesha dalili, umekuwa ukiendelea kwenye taasisi kama vile Chuo Kikuu cha Afya cha Hospitali ya Fujita mkoani Aichi tangu mwezi Machi mwaka huu. Watafiti wanaangazia ni kwa kiasi gani dawa hiyo inaweza ikapunguza wingi wa virusi hivyo.

Kampuni ya Japani inayozalisha dawa ya Avigan imetangaza kwamba imeanzisha majaribio ya kitabibu ili iweze kupata idhini ya serikali. Ikiwa kufaa na usalama wa dawa hiyo vinaweza vikathibitishwa, kampuni hiyo inapanga kutuma ombi la kutaka serikali kuiidhinisha.

Taarifa zilizowasilishwa hapa ni za hadi Aprili 6.

15. Je, virusi hivyo hujibadili muundo wake wa jeni?

Mwanzoni mwa mwezi Machi, kundi la watafiti la nchini China lilitathmini jeni za virusi vya korona kutoka kwa waathirika zaidi ya 100 wa virusi hivyo kutoka kote duniani. Timu hiyo ya watafiti ilibaini tofauti za kijenetiki walizoziweka kwenye aina mbili za virusi vya korona, aina ‘L’ na ‘S’.

Timu hiyo ilibaini kuwa virusi vya aina ya ‘S’ vina muundo wa jeni unaokaribiana kufanana na ule unaopatikana kwenye popo. Virusi aina ‘L’ vilibainika kwa wagonjwa wengi wa kutoka nchi nyingi za Ulaya na vinaaminika kuwa ni aina mpya kulinganisha na vile vya aina ‘S’.

Profesa Ito Masahiro wa Kitengo cha Sayansi ya Uhai cha Chuo Kikuu cha Ritsumeikan anayetafiti juu ya tabia za virusi, anasema virusi vya korona vinabadilika jeni zake kirahisi na vinaaminika kubadilika kupitia kwa watu wengi wanaoambukizwa na kurejelewa kuenea kwa maambukizi ya virusi hivyo.

Katika hatua nyingine, kuhusu uwezekano wa virusi kubadili jeni zake ili kuweza kuwa rahisi kuambukiza, Ito anasema virusi hivyo bado vipo katika hatua ambayo muundo wake wa kijenitiki haujabadilika kwa kiasi kikubwa. Hata kama kuna tofauti ya jeni kati ya aina ‘S’ na ‘L’, bado kuna uhaba wa taarifa juu ya aina ipi ya virusi inayoweza kusababisha dalili kali. Ito anasema wakati ukali wa ugonjwa na viwango vya vifo vikitofautiana miongoni mwa mataifa, inaaminika kutofautiana huko kunasababishwa na watu wenyewe, ikiwemo tofauti ya uwiano wa idadi ya wazee kwenye nchi husika, tamaduni na utamaduni wa chakula.

Taarifa zilizowasilishwa hapa ni za hadi Aprili 3.

14. Je, vijana huugua zaidi pale wanapoambukizwa?

Wataalam huwa wanasema kuwa wazee na wale wenye magonjwa yanayosumbua kwa muda mrefu huwa na kawaida ya kuonyesha dalili kali zaidi pale wanapoambukizwa virusi hivyo.

Lakini mwezi Machi, 2020, vyombo vya habari viliripoti kwamba mwanamke mwenye umri wa miaka 21 nchini Uingereza na msichana wa miaka 16 huko Ufaransa, waliokuwa hawana magonjwa mengine, walipoteza maisha baada ya kuambukizwa virusi vipya vya korona.

Visa vya hivi karibuni vinaonyesha kwamba baadhi ya vijana wanaweza pia kusumbuliwa sana na maradhi.

Japani pia imeshuhudia visa vya vijana wakiumwa sana. Kutsuna Satoshi wa Kituo cha Kitaifa cha Afya Duniani na Tiba alisema miongoni mwa wagonjwa zaidi ya 30 aliowatibu, mwanaume mwenye umri wa miaka ya mwanzoni ya 40 ambaye hakuwa na ugonjwa mwingine wa muda mrefu alionyesha dalili kali za maradhi hayo.

Kutsuna anasema mwanaume huyo alikuwa akisumbuliwa na maradhi ya homa na kukohoa tu katika siku kadhaa za mwanzo lakini baada ya juma moja alianza kusumbuliwa sana na homa ya mapafu na alihitaji kifaa cha kumsaidia kupumua kutokana na kuzorota kwa uwezo wake wa kupumua.

Alisema baadaye hali ya mgonjwa huyo iliimarika. Kutsuna alituambia kuwa vijana hawapaswi kudhani kwamba hawawezi kuathirika kwani wao pia wanaweza kuumwa sana.

Shirika la Afya Duniani lilionya kuwa kuna visa vingi vya watu wenye umri wa miaka chini ya 50, kulazwa hospitalini.

Kituo cha Marekani cha Udhibiti na Uzuiaji wa Magonjwa kiliripoti kuwa asilimia 2 hadi 4 ya walioambukizwa wenye umri wa kati ya miaka 20 na 44 wapo kwenye chumba cha wagonjwa walio mahututi.

Taarifa zilizowekwa hapa ni za hadi Aprili mbili.

13. Maambukizi ya virusi vipya vya korona yatasambaa kupitia maji machafu yaliyovuja kutoka kwenye mabomba ya kupitisha maji ya mvua na yale ya maji machafu. Ni kweli?

Virusi vipya na vile vya SARS vyote vinatoka katika familia moja ya korona. Virusi vya korona vilivyosababisha SARS vinajulikana kwa kuzaliana mara nyingi si tu kwenye koo na mapafu bali pia kwenye utumbo.

Pale virusi vya SARS vilipoenea miongoni mwa watu kwenye maeneo mengi duniani mnamo mwaka 2003, maambukizi ya watu wengi yaliripotiwa kwenye majengo yaliyo makazi ya watu huko Hong Kong.

Ilishukiwa kuwa maambukizi ya halaiki yalisababishwa na matone ya maji yenye virusi yaliyovuja kutoka kwenye mabomba yaliyozeeka ya kupitisha maji ya mvua na yale ya maji machafu.

Profesa Kaku Mitsuo wa Chuo Kikuu cha Tiba na Dawa cha Tohoku, mtaalam wa hatua za kuzuia maambukizi, anasema kuwa kuna hatari kidogo ya virusi kuenea kupitia mabomba hayo kwenye nchi zenye kiwango cha juu kiasi cha usafi.

Lakini anasema inawezekana kwa virusi kujipandikiza kwenye vyoo na maeneo ya kukizunguka na unaweza kupatwa na maambukizi kwa kugusa maeneo hayo kwa mikono yako.

Alisema watu wanapaswa kufunika mfuniko wa choo kabla ya kumwaga maji ya kusafisha baada ya kujisaidia na kuhakikisha kuwa wamenawa vema mikono yao baada ya kutoka chooni.

Anasema watu wanapaswa kuhakikisha wanadumisha hali ya usafi kwenye maisha yao ya kila siku, kama vile kwa kusafisha koki za maji, sehemu za kunawia mikono na vitasa.

Taarifa zilizowasilishwa hapa ni za hadi Aprili Mosi.

11. Je, ukinawa mikono kwa kutumia sabuni, matokeo ni sawa na yale ya kutumia vitakasa vya kileo?

Sakamoto Fumie ni mtaalamu wa udhibiti wa maambukizi kutoka Hospitali ya Kimataifa ya Mtakatifu Luka jijini Tokyo. Anasema matumizi ya sabuni ni bora kwa kiasi fulani.

Kulingana naye, hii ni kwa sababu sabuni ya kunawia mikono kwa kawaida huwa na kemikali, yaani surfactants zinazoharibu utando wa mafuta unaozingira virusi vya korona. Anasema hii inamaanisha virusi hivyo vinaweza vikaharibiwa kwa kiasi fulani.

Sakamoto anasema vitakasa vya kileo pia ni bora, lakini ikiwa mikono yako ni michafu, wakati mwingine ni vigumu kwa vitakasa hivyo kuingia ndani ya sehemu zilizoambukizwa virusi hivyo.

Sakamoto anawasihi watu kunawa mikono mara kwa mara wakitumia sabuni.

8. Japani imepata dawa bora ya kuzuia au kutibu maambukizi ya virusi vipya vya korona?

Kwa bahati mbaya, hakuna dawa zilizothibitishwa kuwa bora katika kutibu virusi vipya vya korona kama vile dawa za Tamiflu na Xofluza zinazotumiwa kutibu influenza. Kama tu katika mataifa mengine, madaktari nchini Japani wanaangazia kutibu dalili kama vile kumsaidia mgonjwa kupumua kwa kumuwekea gesi ya oksijeni na dripu za kumuongezea maji.

Ingawa dawa bora ya kutibu virusi hivyo bado haijaendelezwa, madaktari nchini Japani na kote duniani wanawatibu wagonjwa wa virusi hivyo kwa kutumia dawa zilizopo za kutibu magonjwa mengine kwa sababu zinaweza zikatumika kutibu virusi hivyo.

Mojawapo wa dawa kama hiyo ni ile ya Avigan, hii ikiwa dawa ya kutibu mafua iliyotengenezwa na kampuni moja ya kutengeneza dawa ya Japani miaka 6 iliyopita. Mamlaka za China zinasema dawa hiyo ni bora katika kutibu virusi vya korona.

Kituo cha Kitaifa cha Japani cha Afya Duniani na Tiba kinasema kilitumia dawa moja ya kupambana na virusi inayotumika kuzuia kuanza kwa ugonjwa wa UKIMWI kwa mgonjwa mmoja aliyeambukiziwa virusi vya korona. Maafisa wa kituo hicho wanasema homa ya mgonjwa huyo ilipungua, na uchovu na tatizo la kupumua kuimarika.

Juhudi za kutafuta dawa ya kutibu virusi vya korona zinaendelea katika nchi kadhaa. Kundi moja la watafiti kutoka kwenye Kituo cha Marekani cha Udhibiti na Uzuiaji wa Magonjwa limeripoti kutumia dawa ya kupambana na virusi inayoendelezwa ili kutibu ugonjwa wa Ebola, kumtibu mwanamume mmoja aliyeugua nimonia kutokana na virusi vipya vya korona. Watafiti wamesema dalili za mwanamume huyo zilianza kuimarika siku moja baada ya kupewa dawa hiyo. Walisema aliondolewa kwenye mashine ya kumsaidia kupumua kwa kuwekewa gesi ya oksijeni na homa yake kupungua.

Wizara ya Afya nchini Thailand imesema matumizi ya pamoja ya dawa za kutibu mafua na ugonjwa wa UKIMWI ziliboresha hali ya mgonjwa ambaye alipona kutokana na virusi vipya vya korona.

Hata hivyo katika hali zote, wataalam wanasema utafiti zaidi wa kitabibu unahitajika ili kubaini usalama na ubora wa dawa hizo.

Taarifa zilizowasilishwa hapa ni za hadi Machi 25.

7. Watoto wanaweza wakaonyesha dalili kali ikiwa wataambukizwa virusi vipya vya korona?

Hakuna ripoti yoyote kutoka China kuwa watoto wanaweza wakaonyesha dalili kali ikiwa wataambukizwa virusi vipya vya korona. Tathmini moja iliyofanywa na timu ya wataalam kutoka Kituo cha China cha Udhibiti na Uzuiaji wa Magonjwa iliyohusisha watu 44,672 nchini humo walioambukizwa virusi hivyo kufikia Februari 11 inaonyesha kuwa hakuna mtoto aliye na umri wa miaka 9 au chini ya hapo alifariki kutokana na maambukizi ya virusi hivyo. Ni kifo kimoja tu kilichoripotiwa kati ya wagonjwa walio na umri wa chini ya miaka 20.

Kundi moja la watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Wuhan na taasisi zingine waliripoti kuwa watoto 9 wachanga wenye umri wa kati ya mwezi mmoja na miezi 11 walibainika kuambukizwa virusi hivyo China bara kufikia Februari 6. Wanasema hakuna yeyote aliyezidiwa na ugonjwa.

Profesa Morishima Tsuneo kutoka Chuo Kikuu cha Tiba cha Aichi ni mtaalam wa magonjwa ambukizi ya watoto. Profesa Morishima alisema virusi vipya vya korona ni sawia na aina za sasa za virusi vya korona kwa namna fulani na kwamba watoto wanaougua mafua ya kawaida wanaweza wakawa na kiwango fulani cha kinga dhidi ya virusi hivyo.

Hata hivyo Profesa Morishima aliongeza kuwa tunapaswa kuwa na tahadhari kwa sababu maambukizi hayo huonekana kuenea haraka shuleni na kwenye shule za chekechea. Alisema walezi wanapaswa kuhakikisha watoto wananawa mikono yao ipasavyo na kuhakikisha vyumba wanamoishi vina hewa safi.

Taarifa zilizowasilishwa hapa ni za hadi Machi 24.

6. Nani ambaye huonyesha dalili kali ikiwa ataambukizwa virusi vya korona?

Shirika la Afya Duniani, WHO linasema vingi vya vifo vilivyosababishwa na virusi hivyo ni vya watu walio na matatizo ya kiafya yanayodhoofisha mfumo wa kinga mwilini ikiwa ni pamoja na shinikizo la juu la damu, ugonjwa wa sukari na ule wa moyo.

Ili kuwa na uhakika, watu walio na mfumo dhaifu wa kinga za mwili wanapaswa hasa kuwa waangalifu siyo tu dhidi ya virusi vipya vya korona, lakini pia maambukizi ya kawaida kama vile influenza ya msimu.

Wanajumuisha watu walio na matatizo ya kiafya kama vile shinikizo la juu la damu, ugonjwa wa sukari, ule wa moyo, wale wanaotumia dawa za ushinikizaji wa kinga ya mwili mathalan ili kutibu rumatizimu na wazee.

Watafiti bado hawajabaini jinsi uhatari wa matatizo ya kiafya ya kudumu ya mgonjwa yanavyohusiana na ukali wa dalili zao.

Inapokuja kwa suala la kina mama wajawazito, hakuna takwimu inayoashiria wako kwenye kategoria iliyo kwenye hali hatari ya kuambukizwa virusi vya korona. Lakini kwa ujumla, huwa wanakabiliwa na uwezekano wa kuambukizwa virusi na ikiwa watapata nimonia, kuna uwezekano mkubwa wa wao kukumbwa na dalili kali.

Hakuna takwimu kuhusiana na ni aina gani ya dalili zinazosababishwa na virusi vya korona kwa watoto wachanga. Lakini ikizingatiwa kuwa hawawezi wakachukua hatua za kujilinda kama vile kunawa mikono na kuepukana na sehemu palikofurika watu, walezi wao wanatakiwa kufanya kila wawezalo kuwalinda watoto hao.

5. Ni dalili zipi huonyeshwa na mtu aliyeambukiziwa virusi vipya vya korona?

Kuna ripoti kuhusiana na suala hili iliyochapishwa na timu ya pamoja ya wataalam ikijumuisha wataalam wa Shirika la Afya Duniani, WHO. Timu hiyo ilifanya tathmini ya kina iliyohusu dalili ya watu 55,924 waliothibitishwa kuambukizwa virusi vya korona nchini China Februari 20 mwaka huu.

Ripoti hiyo inasema asilimia 87.9 ya wagonjwa walikuwa na homa, asilimia 67.7 walikuwa wanakohoa, asilimia 38.1 walilalamikia uchovu, na asilimia 33.4 walikuwa na kikohozi. Dalili zingine zinajumuisha kupungukiwa na pumzi, koo linalowasha na kichwa kuuma. Wale walioambukizwa walianza kuonyesha dalili katika wastani wa siku 5 hadi 6.

Takriban asilimia 80 ya watu walioambukizwa walikuwa kwa kiasi fulani na dalili zisizokuwa kali. Baadhi hawakupatwa na nimonia. Kati ya watu wote walioambukizwa virusi hivyo, asilimia 13.8 walizidiwa mno na ugonjwa na kutatizika kupumua.

Watu wenye umri wa miaka 60 au zaidi na wale waliokuwa na matatizo mengine ya kiafya kama vile shinikizo la juu la damu, ugonjwa wa sukari, matatizo ya moyo, magonjwa ya kudumu ya pumzi na saratani walikuwa na uwezekano mkubwa wa kukumbwa na dalili hatari au zinazoweza zikasababisha maafa. Kuna ripoti chache za watoto kuambukiziwa virusi hivyo au kuzidiwa sana na ugonjwa. Ni asilimia 2.4 pekee ya idadi jumla ya walioambukizwa waliokuwa na umri wa miaka 18 kurudi chini.

Daktari Kutsuna Satoshi wa Kituo cha Kitaifa cha Afya Duniani na Tiba amewatibu wagonjwa waliobainika kuambukizwa virusi vipya vya korona nchini Japani. Daktari Kutsuna alisema wagonjwa aliowaona walikuwa wanatiririkwa na makamasi, walikuwa wanawashwa koo na kukohoa. Alisema wote walikuwa wamechoka na homa ya nyuzi 37 au zaidi iliyodumu kwa karibu wiki moja. Kulingana naye, baadhi yao walipatwa na homa kali baada ya wiki moja, na kwamba dalili huonekana kukaa kwa muda kuliko visa vya mafua ya msimu au magonjwa ambukizi ya virusi na mengine.

Taarifa zilizowasilishwa hapa ni za hadi Machi 19.

4. Tunawezaje tukaua virusi kwenye nguo zetu?

Katika kujibu swali hili, Sugawara Erisa kutoka Chama cha Kuzuia na Kudhibiti Maambukizi nchini Japani anasema hakuna haja ya kutumia vitakasa vyenye vileo. Sugawara anaeleza kuwa virusi vingi huoshwa kutoka kwenye nguo zetu kupitia michakato ya kawaida ya uoshaji nguo, ingawa hili bado halijathibitishwa inapokuja kwa suala la virusi vipya vya korona.

Kuhusiana na bidhaa unazohisi zipo hasa kwenye hatari ya kuambukizwa virusi hivyo kama vile hanchifu iliyotumiwa kufunika mdomo unapokohoa au kupiga chafya, Sugawara anapendekeza uviloweshe kwenye maji yanayochemka kwa kati ya dakika 15 hadi 20.

3. Kina mama wajawazito wanapaswa kujitahadhari na kitu gani?

Huku kukiwa na mlipuko wa virusi vipya vya korona, Chama cha Wakunga na Wanajikolojia cha Magonjwa Ambukizi nchini Japani kilitoa waraka ukiwashauri kina mama wajawazito na wanawake wanaotazamia kuwa wajawazito.

Chama hicho kinasema hadi kufikia sasa, hakujakuwa na taarifa kuwa kuna uwezekano mkubwa wa wanawake wajawazito kukumbwa na dalili hatari kutokana na virusi vipya vya korona, au kuwepo kwa ripoti za virusi hivyo kusababisha matatizo kwa mtoto ambaye bado hajazaliwa.

Lakini chama hicho kinaonya kuwa kwa ujumla, wanawake wajawazito wanaweza wakawa hatarini ikiwa wataugua nimonia.

Chama hicho kinawashauri wanawake wajawazito kuchukua tahadhari kama vile kunawa mikono ipasavyo kwa kutumia sabuni hasa baada ya kutoka nje na kabla ya maakuli, na kutumia vitakasa mikono vyenye vileo.

Tahadhari zingine zilizopendekezwa zinajumuisha kuepuka kutangamana na watu walio na mafua na wanaokohoa, kuvaa barakoa na kuepuka kugusa pua na mdomo kwa kutumia mikono yako.

Waraka huo ulitayarishwa na Profesa Hayakawa Satoshi wa Shule ya Tiba ya Chuo Kikuu cha Nihon. Profesa Hayakawa anasema anaelewa wakati kina mama wajawazito wanapokuwa na hofu. Lakini amewataka wanawake kuchukua hatua iliyojikita kwa taarifa sahihi na ya kuaminika kwa sababu aina zote za upotoshaji huenea wakati wa mlipuko wa ugonjwa ambukizi.

2. Ni kwa njia zipi mtu anaweza akaambukizwa virusi hivyo na kujizuia kuambukizwa?

Wataalam wanaamini kuwa virusi vipya vya korona huambukizwa kupitia vitone vya mate au kugusa sehemu iliyo na virusi hivyo kama tu hali inavyokuwa kwa mafua ya msimu au homa. Hii inamaanisha kuwa virusi hivyo huenea kupitia vitone vinavyozalishwa wakati watu walioambukizwa wanapokohoa au kupiga chafya. Mtu pia anaweza akaambukizwa kwa kugusa vitasa vya mlango vilivyo na virusi hivyo, au kanda zinazoning’inia kwenye mabehewa ya treni na kisha kugusa pua au mdomo kwa kutumia mkono uliochafuka. Virusi vya korona vinaaminika kuwa na kiwango sawa cha maambukizi kama mafua ya msimu.

Hatua za msingi za kuzuia maambukizi ya virusi vya korona ni sawa na zile zinazochukuliwa dhidi ya mafua ya msimu. Hizi ni kunawa mikono na kuwa na adabu unapokohoa.

Unaponawa mikono, mtu anashauriwa kutumia sabuni na kuosha kila sehemu ya mikono hadi kwenye kifundo kwa sekunde zisizopungua 20. Au, mtu anaweza akatumia kitakasa mikono chenye kileo. Kuwa na adabu unapokohoa ni njia muhimu ya kudhibiti kuenea kwa maambukizi. Mtu yeyote yule anashauriwa kufunika pua na mdomo kwa kutumia shashi au kiwiko ili kuzuia kuwanyunyizia watu wengine vitone vilivyo na maambukizi. Njia zingine madhubuti ni kuepuka maeneo yaliyosongamana watu, na wakati unaposalia ndani ya nyumba, kufungua madirisha kila wakati ili kuruhusu hewa safi kuingia kwenye nyumba hiyo.

Nchini Japani, kila kampuni ya treni itaamua ikiwa itafungua madirisha ya mabehewa ya abiria yaliyojaa watu. Watalaam wanasema mabehewa hayo tayari yamewekewa hewa safi kwa kiwango fulani kwa sababu milango ya treni hizo itafunguka wakati zinaposimama kituoni na abiria kuingia au kushuka kwenye treni.

1. Virusi vya korona ni nini hasa?

Virusi vya korona ni virusi wanavyoambukizwa binadamu na wanyama wengine. Kwa ujumla, virusi hivyo huenea miongoni mwa watu na kusababisha dalili sawa na zile za homa kama vile kukohoa, mafua na kutokwa na makamasi. Aina zingine kama vile Ugonjwa wa Mashariki ya Kati Unaoathiri Mfumo wa Upumuaji, almaarufu MERS uliothibitishwa nchini Saudia mwaka 2012, zinaweza zikasababisha nimonia au dalili zingine hatari.

Virusi vya korona ambavyo vimesababisha janga duniani ni vya aina mpya. Watu walioambukizwa hukumbwa na dalili kama vile mafua, vikohozi, uchovu, kupungukiwa na pumzi, koo zinazowasha na vichwa kuuma. Asilimia ya wagonjwa wapatao 80 hupona baada ya kukumbwa na dalili zisizokuwa hatari. Karibu asilimia 20 hukumbwa na dalili hatari kama vile nimonia au hata viungo vingi vya mwili kushindwa kufanya kazi. Watu walio na zaidi ya umri wa miaka 60, au walio na matatizo mengine kama vile kiwango cha juu cha msukumo wa damu, ugonjwa wa kisukari, ule wa moyo, matatizo ya kupumua au saratani wana uwezekano wa kukumbwa na hali hatari au kufariki. Maambukizi machache yameripotiwa miongoni mwa watoto na dalili zao kwa kiasi fulani si hatari.
TOP